Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza kuzuiaje porojo?

Ninaweza kuzuiaje porojo?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza kuzuiaje porojo?

“Pindi moja nilienda kwenye karamu fulani, na siku iliyofuata fununu zilienea kwamba nilifanya ngono na mvulana mmoja. Huo ulikuwa uwongo mtupu!”—Linda. *

“Nyakati nyingine mimi husikia fununu kwamba nina mchumba ingawa simfahamu mtu huyo! Watu wengi ambao hupiga porojo hawachunguzi ikiwa wanayosema ni kweli.” —Mike.

POROJO inaweza kufanya maisha yako yawe na mambo mengi ya ajabu kuliko hata ya sinema yenye kusisimua. Unahitaji tu kumwuliza Amber aliye na umri wa miaka 19. Anasema hivi: “Watu wameeneza porojo nyingi kunihusu. Walisema eti nilikuwa mjamzito, kwamba nilitoa mimba, na kwamba ninanunua, kuuza, na kutumia dawa za kulevya. Kwa nini watu waseme mambo hayo yote kunihusu? Kwa kweli, sijui kwa nini wanasema hivyo!”

Kutumia Teknolojia Kueneza Porojo

Wazazi wako walipokuwa vijana, porojo ilienezwa hasa kwa mdomo. Lakini siku hizi porojo huenezwa kwa teknolojia ya kisasa. Kwa kuwa kuna barua-pepe na njia za kutuma ujumbe haraka, kijana aliye na nia mbaya anaweza kupaka jina lako matope bila hata kufungua mdomo. Anahitaji tu kuandika ujumbe mfupi na porojo mbaya sana isambae kwa watu wengi.

Inasemekana kuwa siku hizi watu wanapendelea zaidi kutumia Intaneti kueneza porojo kuliko kutumia simu. Katika visa fulani, kituo cha Intaneti kimeanzishwa ili tu kumwaibisha mtu. Mara nyingi vituo vya kibinafsi, ambavyo huwa na habari za kibinafsi za mtu, hujazwa porojo ambayo mtu huyo hangeweza kusema mwenyewe. Kwa kweli, asilimia 58 ya vijana katika uchunguzi mmoja walisema kwamba angalau wakati mmoja mambo mabaya kuwahusu yameandikwa katika Intaneti.

Lakini je, nyakati zote ni vibaya kuzungumza kuhusu watu wengine? Na je, kuna kitu kama . . .

Porojo Nzuri?

Tia alama katika sentensi ifuatayo.

Hakuna porojo nzuri. Kweli Si kweli

Ni jibu gani lililo sahihi? Inategemea unavyoelewa neno “porojo.” Ikiwa neno hilo linamaanisha mazungumzo ya kawaida, kuna pindi ambapo inafaa. Kwa kweli, Biblia inatuambia ‘tupendezwe na maisha ya wengine.’ (Wafilipi 2:4, New Century Version) Hilo halimaanishi kwamba tujiingize katika mambo ambayo hayatuhusu. (1 Petro 4:15) Lakini mara nyingi mazungumzo ya kawaida hutoa habari muhimu, kama vile, nani anaoa au kuolewa, nani amejifungua mtoto, na ni nani anayehitaji msaada wa aina fulani. Ukweli wa mambo ni kwamba hatuwezi kusema tunawajali wengine ikiwa hatuzungumzi kamwe kuwahusu.

Hata hivyo, mazungumzo ya kawaida tu yanaweza kwa urahisi kugeuka na kuwa porojo mbaya. Kwa mfano, mtu akisema “Bob na Sue wanaweza kufaana sana katika ndoa” maneno hayo yanaweza kurudiwa na kuwa “Bob na Sue wanachumbiana,” hata ikiwa Bob na Sue hawana uhusiano wowote. Huenda ukasema, ‘Maneno hayo hayana ubaya wowote.’ Lakini namna gani ikiwa maneno hayo yanasemwa kukuhusu?

Julie, aliye na umri wa miaka 18, anasema kwamba aliumia sana porojo ya aina hiyo ilipoenezwa kumhusu. “Nilikasirika,” anasema, “na ilinifanya nianze kuhisi kwamba siwezi kuwatumaini watu.” Jane, mwenye umri wa miaka 19, alikuwa katika hali kama hiyo. “Mwishowe nilimwepuka mvulana ambaye ilisemekana tunachumbiana,” anasema huku akiongezea, “Hiyo haikuwa sawa, kwa sababu tulikuwa marafiki nami nilihisi kwamba tunapaswa kuzungumza bila mtu yeyote kuanzisha uvumi kutuhusu.”

Ni wazi, porojo mbaya hutokeza madhara. Hata hivyo, wengi ambao wameumizwa na porojo watakuambia kwamba wao pia wamejihusisha katika porojo. Ukweli ni kwamba kunapokuwa na mazungumzo ya kumdhihaki mtu mwingine ni rahisi kushawishiwa kujiunga na mazungumzo hayo. Kwa nini? Phillip mwenye umri wa miaka 18 anasema: “Ni njia ya kuhepa. Watu hupendezwa zaidi kuzungumza kuhusu matatizo ya wengine kuliko yao.” Basi unaweza kufanya nini ikiwa mazungumzo ya kawaida yanageuka kuwa porojo mbaya?

Badili Mazungumzo kwa Busara!

Wazia ustadi unaohitajiwa ili kuendesha gari kwenye barabara yenye magari mengi. Bila kutarajiwa, hali fulani inaweza kukulazimu kutoka barabara moja kwenda nyingine, kupunguza mwendo, au kusimama. Ukiwa chonjo na unajali usalama, utatambua ni nini kiko mbele na kutenda kwa njia inayofaa.

Hali ni hiyo pia katika mazungumzo. Mara nyingi unaweza kujua iwapo mazungumzo yanaelekea kuwa porojo mbaya. Hilo linapotukia, je, unaweza kutoka kwenye hiyo barabara? Usipofanya hivyo, porojo inaweza kutokeza madhara. Mike anaeleza hivi: “Nilisema kitu fulani kisichofaa kumhusu msichana mmoja, kwamba anapenda sana wavulana. Mtu fulani alimwambia nilichosema. Sitasahau kamwe sauti yake alipozungumza nami, jinsi alivyoumizwa na maneno niliyosema bila kufikiri. Tulitatua jambo hilo, lakini sikujihisi vizuri kujua kwamba nilikuwa nimemwumiza mtu mwingine kwa njia hiyo!”

Ni kweli, unahitaji ujasiri kukatiza mazungumzo ambayo yameanza kuwa porojo. Carolyn mwenye umri wa miaka 17 anasema: “Unahitaji kuwa mwangalifu unasema nini. Ikiwa hujasikia jambo kutoka kwa chanzo kinachoaminika, unaweza kuwa unaeneza uwongo.”

Ili uepuke porojo mbaya, fuata mashauri ya maandiko ya Biblia yafuatayo:

“Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa, lakini anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” (Methali 10:19) Kadiri unavyozungumza, ndivyo kunavyokuwa na uwezekano wa kusema jambo ambalo utajutia baadaye. Afadhali watu wakuone kuwa mtu mnyamavu kuliko mtu mwenye maneno mengi!

“Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu, lakini kinywa cha waovu hububujika mambo mabaya.” (Methali 15:28) Fikiri kabla ya kuzungumza!

“Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) Kabla ya kusimulia jambo, hakikisha kwamba ni la kweli.

“Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Hata kama habari kumhusu mtu fulani ni sahihi, jiulize hivi kabla ya kuisimulia, ‘Ningehisije ikiwa mtu angesema habari kama hizi kunihusu?’

“Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Waroma 14:19) Hata habari sahihi inaweza kudhuru ikiwa haijengi.

‘Fanyeni iwe shabaha yenu kuishi kwa utulivu na kukazia akili mambo yenu wenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Usijiingize sana katika mambo ya watu wengine. Kuna njia nzuri zaidi za kutumia wakati wako.

Porojo Zikienezwa Kukuhusu

Ni kweli kwamba unapaswa kudhibiti ulimi na kuepuka kupiga porojo kuhusu watu wengine. Lakini ikiwa porojo zinaenezwa kukuhusu, unaweza kuchukua jambo hilo kwa uzito sana. “Nilihisi kama sitakuwa tena na marafiki,” anasema Joanne mwenye umri wa miaka 16, ambaye wakati fulani porojo mbaya zilienezwa kumhusu. “Nyakati nyingine nililia sana usiku hadi nilipolala. Nilihisi kwamba jina langu lilikuwa limechafuliwa!”

Lakini unaweza kufanya nini porojo zisizo na msingi zinapoenezwa kukuhusu?

Jiulize ni nini kilichowafanya watu waseme mambo hayo. Jaribu kuelewa kinachowachochea watu kupiga porojo. Wengine hutaka kuonwa kuwa maarufu wakijaribu kuonekana kuwa wanajua mengi. “Hawataki kuonekana kuwa washamba kwa hiyo wao huzungumza kuhusu watu wengine,” anasema Karen, mwenye umri wa miaka 14. Vijana fulani wanaweza kuwadhihaki wengine ili tu wahisi vizuri. Renee, mwenye umri wa miaka 17 anasema, “Watu wamechoshwa na maisha, ndiyo sababu wangependa kuanzisha porojo ili wafanye maisha yawe yenye kuchangamsha zaidi.”

Dhibiti Hisia Zako. Mtu ambaye ameumizwa na porojo mbaya akishindwa kudhibiti hisia za kuaibishwa na za chuki, anaweza kutenda kwa njia itakayomfanya asikitike baadaye. “Yule anayekasirika upesi atatenda upumbavu,” inasema Methali 14:17. Ingawa si rahisi, huu ndio wakati wa kujidhibiti sana. Ukifaulu, utaepuka kuingia katika mtego ambao ulimnasa yule aliyeeneza porojo kukuhusu.

Elewa sababu ya porojo. Jiulize maswali yafuatayo: ‘Je, nina hakika kwamba mambo hayo yalisemwa dhidi yangu? Je, ni fununu au ni kukosa kuelewana? Je, ninachukua mambo kwa uzito kupita kiasi?’ Ni kweli hakuna sababu ya kutetea porojo mbaya. Lakini, kukasirika kupita kiasi kunaweza kuharibu sifa yako kuliko porojo yenyewe. Kwa hiyo, jitahidi kuwa na maoni kama ya Renee ambaye anasema, “Mimi huumizwa mtu anaposema jambo fulani baya kunihusu, lakini mimi hujaribu kutolichukua kwa uzito sana. Huenda juma lijalo watakuwa wakizungumza kuhusu mtu au kitu kingine.” *

Ulinzi Wako Mkuu

Biblia inasema waziwazi kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi,” kisha inaongeza hivi: “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Hivyo, si jambo la hekima kuchukua kwa uzito sana kila jambo linalosemwa kutuhusu. Mhubiri 7:22 inasema: “Moyo wako mwenyewe unajua vema kwamba hata mara nyingi wewe, naam hata wewe, umewalaani wengine.”

Unaposikia porojo mbaya kukuhusu, ulinzi wako mkuu ni mwenendo wako. Yesu alisema: “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mathayo 11:19) Hivyo, jaribu kudumu ukiwa mwenye urafiki na upendo. Huenda ukashangaa jinsi utakavyomaliza porojo hizo, au labda utakavyoweza kuvumilia madhara yake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 33 Katika visa fulani huenda ikafaa kutafuta njia yenye busara ya kuzungumza na anayepiga porojo hizo. Hata hivyo, mara nyingi si lazima kufanya hivyo, kwani “upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Petro 4:8.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unaweza kuepukaje kueneza porojo kuhusu wengine?

▪ Utafanya nini mtu akipiga porojo kukuhusu?