Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Upendo Nyumbani

Onyesha Upendo Nyumbani

Hatua ya 2

Onyesha Upendo Nyumbani

Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watoto wanahitaji upendo na wanapoukosa, hawakui vizuri. Katika miaka ya 1950, M. F. Ashley Montagu, mtaalamu wa tabia na tamaduni za wanadamu aliandika hivi: “Mwanadamu anahitaji hasa upendo ili akue vizuri; upendo ndio chanzo cha afya nzuri hasa katika miaka sita ya kwanza.” Watafiti wa kisasa wanakubaliana na maneno ya Montagu aliposema kwamba “watoto huathiriwa sana wasipoonyeshwa upendo wa kutosha.”

Tatizo: Kuishi katika ulimwengu huu usio na upendo na wenye ubinafsi hufanya hali ya familia iwe ngumu. (2 Timotheo 3:1-5) Huenda wenzi wa ndoa wakaona kwamba mikazo ya kihisia na kifedha inayotokana na kuwalea watoto huongeza matatizo katika ndoa. Kwa mfano, wenzi wa ndoa ambao tayari wana shida ya kuwasiliana huongeza matatizo hayo wanapotofautiana kuhusu jinsi wanavyopaswa kuwatia nidhamu na kuwapa watoto wao zawadi.

Suluhisho: Panga muda wa kuwa pamoja na familia. Pia, wenzi wa ndoa wanahitaji kupanga wakati wao wa kuwa pamoja. (Amosi 3:3) Tumieni vizuri wakati mnaopata watoto wanapolala. Msiruhusu televisheni ichukue wakati huo muhimu. Endeleeni kuonyeshana upendo katika ndoa yenu. (Methali 25:11; Wimbo wa Sulemani 4:7-10) Badala ya “kutafuta makosa” wakati wote, tafuta njia za kumpongeza mwenzi wako kila siku.—Zaburi 103:9, 10; Methali 31:28.

Waambie watoto wako kwamba unawapenda. Yehova Mungu aliwawekea wazazi kielelezo kizuri kwa kumwonyesha Mwana wake, Yesu, upendo waziwazi. (Mathayo 3:17; 17:5) Fleck, baba anayeishi Austria, anasema: “Nimegundua kwamba watoto ni kama maua fulani. Kama vile mimea hiyo midogo hugeuka kuelekea jua ili kupata mwangaza na joto, watoto huwategemea wazazi wao ili wapate upendo na kuhakikishiwa kwamba wao ni washiriki wa familia wenye thamani.”

Uwe umeoa au kuolewa au wewe ni mzazi asiye na mwenzi, ukisaidia familia yako kupendana na kumpenda Mungu, maisha ya familia yako yatakuwa bora.

Lakini, Neno la Mungu linasema nini kuhusu wazazi kutumia mamlaka yao?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” —Wakolosai 3:14