Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Panga Ratiba na Kuifuata

Panga Ratiba na Kuifuata

Hatua ya 5

Panga Ratiba na Kuifuata

Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watu wengi wazima hufuata ratiba. Watu wengi hufanya kazi, huabudu, na kuburudika wakati fulani hususa. Wazazi watakuwa wakiwanyima watoto wao jambo fulani wasipowafundisha kupanga wakati wao na kufuata ratiba. Kwa upande mwingine, “uchunguzi unaonyesha kwamba kuwa na sheria na kufuata ratiba kunamfanya mtoto ahisi salama na kumfunza kujidhibiti na kujitegemea,” anasema Dakt. Laurence Steinberg, profesa wa saikolojia.

Tatizo: Maisha yana pilikapilika nyingi. Wazazi wengi wanafanya kazi kwa saa nyingi, hivyo kwa kawaida hawana wakati mwingi wa kuwa na watoto wao. Kupanga na kudumisha ratiba kunahitaji kujidhabihu na jitihada nyingi hasa mwanzoni mtoto anapokataa kufuata ratiba.

Suluhisho: Tumia kanuni ya shauri hili la Biblia: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Kwa mfano, watoto wakiwa bado wachanga, wazazi wengi wanaweka saa hususa za kwenda kulala. Hata hivyo, watoto wanapaswa kufurahia kipindi hicho. Tatiana anayeishi Ugiriki na ambaye ana binti wawili, anasema: “Watoto wakiingia kitandani, mimi huwapapasa-papasa na kuwaambia kile ambacho nilifanya walipokuwa shuleni. Kisha ninawauliza ikiwa wangependa kuniambia mambo ambayo wao wamefanya siku hiyo. Wanatulia. Mara nyingi wao huniambia yaliyo moyoni mwao.”

Kostas, mume wa Tatiana, huwasomea wasichana wao hadithi. Anasema: “Wao hutaja mambo fulani kuhusu hadithi hiyo na mara nyingi wao huanza kuzungumzia mahangaiko yao. Nikiwalazimisha wanieleze mahangaiko yao, hawataniambia.” Bila shaka, watoto wanapozidi kukua itakubidi ubadilishe saa zao za kulala. Lakini ukidumisha utaratibu huo, inaelekea watoto wako wataendelea kutumia wakati huo kukueleza mahangaiko yao.

Isitoshe, familia zinapaswa kuwa na zoea la kula angalau mlo mmoja kwa siku pamoja. Ili kudumisha utaratibu huo, huenda mkahitaji kubadili wakati wa kula. Charles ambaye ana binti wawili anasema: “Nyakati nyingine mimi hurudi nyumbani nikiwa nimechelewa. Ingawa nyakati nyingine mke wangu huwapa watoto chakula chepesi ili kutuliza njaa, kila mtu husubiri hadi tule pamoja tukiwa familia. Sisi huzungumzia utendaji wa siku hiyo, tunapitia Andiko moja, tunazungumzia matatizo, na kucheka pamoja. Lazima nikiri kwamba utaratibu huo umechangia sana kuwa na familia yenye furaha.”

Ili ufanikiwe katika hatua hii, usiruhusu kufuatia vitu vya kimwili kuvuruge ratiba ya familia yako. Fuata shauri hili la Biblia: ‘Hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’—Wafilipi 1:10.

Ni jambo gani lingine ambalo wazazi wanaweza kufanya ili kuboresha mawasiliano pamoja na watoto wao?

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 Wakorintho 14:40