Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tambua Hisia za Mtoto Wako

Tambua Hisia za Mtoto Wako

Hatua ya 6

Tambua Hisia za Mtoto Wako

Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watoto wanataka na wanahitaji watu muhimu zaidi maishani mwao, yaani, wazazi wao wajue wanavyohisi. Ikiwa wazazi wana zoea la kuwapuuza watoto wanapowaeleza hisia zao, huenda watoto wakasita kuwaeleza hisia zao na hata wakaanza kutilia shaka uwezo wao wa kuhisi na kufikiri.

Tatizo: Huenda watoto wakatilia chumvi wanapoeleza fikira na hisia zao. Ni kweli kwamba baadhi ya mambo ambayo watoto wanasema humshtua mzazi. Kwa mfano, mtoto aliyekata tamaa anaweza kusema, “Maisha yangu yamenichosha.” * Mzazi akisikia hilo anaweza kusema, “Hujui unalosema!” Huenda wazazi wakaogopa kwamba kutambua hisia hizo zisizofaa za mtoto kunamaanisha kuwa unakubaliana nazo.

Suluhisho: Fuata shauri la Biblia la kuwa “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” (Yakobo 1:19) Kumbuka kwamba Yehova Mungu alitambua hisia zisizofaa za watumishi wake wengi waaminifu na akaruhusu ziandikwe katika Biblia. (Mwanzo 27:46; Zaburi 73:12, 13) Kwa mfano, Ayubu alipokuwa akipatwa na majaribu makali, alisema anataka kufa.—Ayubu 14:13.

Ni wazi kwamba mawazo na hisia fulani za Ayubu zilihitaji kurekebishwa. Lakini badala ya kupuuza hisia za Ayubu au kumnyamazisha, Yehova alimtendea Ayubu kwa heshima kwa kumruhusu kwa subira aumimine moyo wake. Baadaye tu ndipo Yehova alipomsahihisha kwa fadhili. Baba mmoja Mkristo alisema hivi, “Kwa kuwa Yehova ananiruhusu nimmiminie moyo wangu katika sala, nafikiri inafaa pia niwaruhusu watoto wangu wanimiminie hisia zao zinazofaa na zisizofaa.”

Ukihisi kwamba unataka kumwambia mtoto wako “Sidhani kama unajua unachosema,” kumbuka sheria hii maarufu ya Yesu: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Kwa mfano, wazia kwamba umenyanyaswa au kutamaushwa kazini kwa sababu labda ulifanya kosa fulani. Unamweleza rafiki yako wa karibu hisia zako na kumwambia kwamba huwezi kuendelea na kazi hiyo. Ungependa rafiki yako afanye nini? Je, ungetaka akuambie kwamba haumaanishi unachosema na kwamba umejiletea tatizo hilo mwenyewe? Au je, ungependa rafiki yako akuambie: “Lazima iwe ilikuwa vigumu kushughulika na hali hiyo. Inaonekana leo umeshinda vibaya”?

Watoto na vilevile watu wazima wanaweza kukubali mashauri ikiwa wanahisi kwamba yule anayeyatoa anawaelewa vizuri na anaelewa matatizo wanayokabili. “Moyo wa mtu mwenye hekima hukifanya kinywa chake kionyeshe ufahamu, na kwenye midomo yake huongeza ushawishi,” lasema Neno la Mungu.—Methali 16:23.

Unaweza kuhakikishaje kwamba shauri lolote unalotoa linachukuliwa kwa uzito?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Usiwapuuze watoto wako wanapozungumza kuhusu kujiua.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

‘Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu kwake.’—Methali 18:13