Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Weka Sheria Zilizo Wazi na Utekeleze Adhabu Haraka

Weka Sheria Zilizo Wazi na Utekeleze Adhabu Haraka

Hatua ya 4

Weka Sheria Zilizo Wazi na Utekeleze Adhabu Haraka

Kwa nini hatua hii ni muhimu? Ronald Simons, mwanasosholojia katika Chuo Kikuu cha Georgia, anasema: “Ukweli wa mambo ni kwamba maisha ya watoto huwa mazuri wanapowekewa sheria zilizo wazi na kuadhibiwa kila mara wanapozivunja. Wazazi wasipofanya hivyo, watoto hujifikiria tu, huwa wenye ubinafsi, na wanakosa furaha, na hivyo wanafanya kila mtu akose furaha pia.” Neno la Mungu linasema hivi waziwazi: “Ikiwa unawapenda watoto wako, utawarekebisha.”—Methali 13:24, New Century Version.

Tatizo: Kuweka sheria zinazofaa kuhusu jinsi watoto wako wanavyopaswa kujiendesha na kutekeleza adhabu sheria hizo zinapovunjwa huchukua wakati, jitihada, na uvumilivu. Na watoto huwa na mwelekeo wa kutaka kuvunja sheria hizo. Mike na Sonia, ambao wana watoto wawili, wanasema hivi kuhusu tatizo hilo: “Watoto ni watu wadogo wenye akili na tamaa zao wenyewe na mwelekeo wa kiasili wa kufanya dhambi.” Wazazi hao wanawapenda sana binti zao. Lakini wanakiri hivi, “Nyakati nyingine, watoto wanaweza kuwa na vichwa vigumu na wenye ubinafsi.”

Suluhisho: Iga jinsi Yehova alivyoshughulika na taifa la Israeli. Njia moja ambayo Yehova aliwaonyesha watu wake upendo ilikuwa kwa kutaja waziwazi sheria ambazo alitaka wafuate. (Kutoka 20:2-17) Alionyesha wazi madhara ya kutotii sheria hizo.—Kutoka 22:1-9.

Hivyo, kwa nini usiandike orodha ya sheria unazotaka watoto wako watii. Wazazi fulani wanapendekeza orodha ya sheria chache tu, kama tano hivi. Ni rahisi kuhakikisha kwamba orodha ya sheria chache inafuatwa na ni rahisi vilevile kuzikumbuka. Kando ya sheria hizo, andika adhabu. Hakikisha kwamba adhabu haipiti kiasi na kwamba uko tayari kuitekeleza. Pitieni sheria hizo mara kwa mara ili nyote, kutia ndani Baba na Mama, mjue mnachopaswa kufanya.

Sheria zinapovunjwa, tekeleza adhabu haraka, na ufanye hivyo kwa utulivu, uthabiti, na kila mara kosa linapofanywa. Kumbuka: Usitoe adhabu ukiwa umekasirika; tulia kwanza. (Methali 29:22) Hata hivyo, usiiahirishe. Usijadiliane kuhusu adhabu utakayotoa. Ukiahirisha, mtoto wako atafikiri kwamba hahitaji kuchukua sheria hizo kwa uzito. Hilo linapatana na maneno haya ya Biblia: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.”—Mhubiri 8:11.

Ni katika njia gani nyingine unaweza kutumia mamlaka kuwasaidia watoto wako?

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”—Mathayo 5:37