Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuwa na Mtazamo Mzuri Kunaweza Kuboresha Afya Yako?

Je, Kuwa na Mtazamo Mzuri Kunaweza Kuboresha Afya Yako?

Je, Kuwa na Mtazamo Mzuri Kunaweza Kuboresha Afya Yako?

“Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri,” ndivyo alivyoandika mfalme mwenye hekima wa Israeli miaka 3,000 hivi iliyopita. (Methali 17:22) Leo, madaktari wanatambua hekima ya maneno hayo yaliyoongozwa kwa roho. Hata hivyo, kwa wengi wetu si rahisi kuwa na “moyo wenye shangwe.”

Ni wachache kati yetu wanaoweza kuepuka shida za kila siku ambazo huwafanya watu wakate tamaa na watazamie mabaya. Hata hivyo, uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba licha ya matatizo inafaa kuwa na mtazamo mzuri.

Mtu mwenye mtazamo mzuri ana “tumaini na mwelekeo wa kutazamia matokeo mazuri.” Mtu kama huyo akipata kipingamizi, anafanyaje? Hakubali kushindwa kabisa. Hilo halimaanishi kwamba anapuuza ukweli wa mambo. Badala yake, anakubali na kuchunguza jambo hilo. Kisha, hali zinapomruhusu, yeye huchukua hatua za kubadili au kuboresha mambo.

Kwa upande mwingine, mara nyingi mtu aliye na mtazamo mbaya anajilaumu kwa sababu ya hali mbaya. Anafikiri kwamba hali mbaya zitadumu na zinasababishwa na ujinga wake, kukosa ustadi, au kwa sababu havutii. Kwa hiyo, hajaribu kuboresha hali yake.

Je, kuwa na mtazamo mzuri kunaweza kuboresha afya yetu? Ndiyo. Katika uchunguzi uliofanyiwa zaidi ya wagonjwa 800 kwa muda wa miaka 30 na Kliniki ya Mayo ya Rochester, Minnesota huko Marekani, wanasayansi waligundua kwamba watu wenye mtazamo mzuri walikuwa na afya nzuri na waliishi muda mrefu zaidi. Pia, wachunguzi hao waliona kwamba watu wenye mtazamo mzuri walikabiliana vizuri zaidi na mfadhaiko na ilikuwa vigumu kwao kushuka moyo.

Hata hivyo, kuwa na mtazamo mzuri si rahisi katika ulimwengu ambao matatizo yanazidi kuongezeka. Haishangazi kwamba watu wengi huona ni vigumu kuwa na mtazamo mzuri. Tatizo hilo linaweza kutatuliwaje? Sanduku lililo katika ukurasa huu lina mapendekezo yanayoweza kukusaidia.

Ingawa kuwa na mtazamo mzuri hakutatatua matatizo yote, kunaweza kumfanya mtu awe na afya njema na maisha yenye kuridhisha zaidi. Biblia inasema: “Kwa mtu mwenye huzuni kila siku ni yenye uovu, kwa moyo wenye shangwe kila siku ni sikukuu.”—Methali 15:15, The Jerusalem Bible.

[Sanduku/ Picha katika ukurasa wa 26]

Mapendekezo ya Kuwa na Mtazamo Mzuri *

▪ Ukijikuta unafikiria kwamba hutafurahia jambo fulani au hutafanikiwa, kataa wazo hilo. Kazia fikira mambo mazuri.

▪ Jaribu kufurahia kazi yako. Haidhuru unafanya kazi gani, tafuta mambo ambayo yanakufurahisha.

▪ Tafuta marafiki walio na mtazamo mzuri.

▪ Shughulika na hali unazoweza kukabiliana nazo na uachane na zile ambazo huziwezi.

▪ Kila siku, andika mambo matatu mazuri yaliyotendeka.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Baadhi ya mambo yaliyoorodheshwa yametolewa kwenye kitabu kilichoandikwa na Kliniki ya Mayo.