Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anapaswa Kulaumiwa?

Je, Mungu Anapaswa Kulaumiwa?

Je, Mungu Anapaswa Kulaumiwa?

“MUNGU ni upendo,” Biblia inasema. (1 Yohana 4:8) Pia, yeye ni mwenye haki na huruma. “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Kwa kuwa yeye ni Muumba, Yehova Mungu ana uwezo wa kuona mapema vitu vyote vinavyoweza kusababisha madhara, naye ana nguvu za kuingilia mambo. Kwa kufikiria mambo hayo na sifa za Mungu katika Biblia, inaeleweka kwamba wengi huuliza, “Kwa nini Mungu huruhusu misiba ya asili itukie?” * Mamilioni ya watu ambao wameuliza swali hilo wamegundua kwamba Mungu mwenyewe anatoa jibu linalopatana na akili katika Neno lake lililoandikwa. (2 Timotheo 3:16) Tafadhali fikiria mambo yafuatayo.

Walikataa Upendo wa Mungu

Biblia inatuambia kwamba Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza kila kitu walichohitaji ili waishi kwa furaha na usalama. Isitoshe, kadiri ambavyo wao na watoto wao wangeendelea kutii amri ya Mungu ya ‘kuzaa na kuwa wengi, waijaze dunia,’ familia ya wanadamu ingeweza kutazamia kwamba Mungu angeendelea kuwatunza.—Mwanzo 1:28.

Hata hivyo, kwa kusikitisha Adamu na Hawa walimwasi kimakusudi Muumba wao kwa kutomtii na kuchagua kutomtegemea. (Mwanzo 1:28; 3:1-6) Kwa wazi wanadamu wengi wamefuata kielelezo chao. (Mwanzo 6:5, 6, 11, 12) Kwa ufupi, wanadamu wamechagua kujiongoza na kuimiliki dunia bila kuongozwa na Mungu. Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye upendo ambaye anaheshimu hiari ya watu wake, Yehova hawalazimishi wanadamu wajitiishe chini ya enzi yake kuu, hata ikiwa kuikaidi kunaweza kuwaletea madhara. *

Hata hivyo, Yehova hakuiacha familia ya wanadamu. Hadi leo “yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Kwa kuongezea, Mungu alimpa mwanadamu uwezo wa kujifunza kuhusu dunia na mizunguko yake, na kwa kadiri fulani ujuzi huo umewasaidia wanadamu kutabiri hali mbaya sana ya hewa na hatari nyingine, kama vile milipuko ya volkano.

Pia, wanadamu wamegundua ni sehemu gani za dunia ambazo hukabiliwa zaidi na matetemeko mabaya ya nchi au hali mbaya sana ya hewa. Katika nchi fulani ujuzi huo umesaidia kuokoa uhai kwa kuwaelimisha watu na vilevile umefanya mbinu bora zaidi za ujenzi na mifumo ya kutoa maonyo iweze kugunduliwa. Hata hivyo, idadi ya misiba ya asili inayoripotiwa kila mwaka imekuwa ikiongezeka. Kuna sababu nyingi zenye kutatanisha zinazofanya mambo hayo yatukie.

Kuishi Katika Maeneo Hatari

Uharibifu wa msiba hautegemei hasa nguvu za asili ni kubwa kadiri gani. Mara nyingi msiba hutokea kwa sababu ya watu wengi sana kuwa katika eneo lililoathiriwa. Kulingana na ripoti iliyochapishwa na Benki ya Dunia, katika zaidi ya nchi 160, zaidi ya robo ya watu huishi katika maeneo yenye hatari zaidi ya kufa kutokana na misiba ya asili. “Kwa sababu ya watu wengi zaidi kuwa mahali [penye hatari], tukio la asili linaweza kugeuka kuwa msiba,” anasema mwanasayansi Klaus Jacob wa Chuo Kikuu cha Columbia nchini Marekani.

Mambo mengine yanayofanya hali iwe mbaya ni watu kuhamia katika majiji haraka na bila mpango, ukataji wa miti, na kufunika kwa saruji sehemu kubwa ya ardhi ambayo kwa kawaida ingefyonza maji. Mambo hayo mawili yaliyotajwa mwisho yanaweza kusababisha maporomoko ya matope na mafuriko makubwa.

Shughuli za wanadamu zinaweza pia kufanya matetemeko ya nchi kuwa misiba mikubwa, kwani si nguvu za tetemeko zinazosababisha vifo na majeraha mengi bali ni majengo yanayoanguka. Haishangazi kwamba wataalamu wa kuchunguza matetemeko ya nchi husema: “Matetemeko ya nchi hayawaui watu. Majengo ndiyo yanayowaua watu.”

Idadi ya vifo huongezeka kwa sababu serikali haitimizi majukumu yake. Katika nchi moja ya Amerika Kusini, matetemeko ya nchi yameharibu mji mkuu mara tatu katika miaka 400 iliyopita. Na tangu tetemeko la mwisho, mnamo 1967, idadi ya watu imeongezeka kuwa milioni tano. “Lakini huenda hakuna sheria za ujenzi ambazo zinaweza kuwalinda watu au hakuna anayehakikisha zinafuatwa,” linasema gazeti New Scientist.

Maneno hayo ya mwisho yanaeleza hali iliyotokea katika jiji la New Orleans, Louisiana, Marekani, lililojengwa katika eneo la chini ambako mafuriko yanaweza kutokea. Licha ya kuwapo kwa mabomba ya kuzuia maji na pampu, msiba ambao wengi walikuwa wakihofia mwishowe ulitokea mnamo 2005 Tufani Katrina ilipopiga. “Maonyo ya muda mrefu” yalipuuzwa au “hayakuchukuliwa kwa uzito,” inasema ripoti moja katika gazeti USA Today.

Itikio kama hilo limeonekana kuhusu kuongezeka kwa kiwango cha joto, ambako wanasayansi wengi wanaamini kutaongeza misiba mingi inayohusiana na hali ya hewa na kuinua kiwango cha maji baharini. Kwa wazi, tunapaswa kufikiria mambo ya kisiasa, ya kijamii, na ya kiuchumi, ambayo hayakuanzishwa na Mungu. Mambo hayo yaliyoanzishwa na wanadamu yanatukumbusha ukweli wa maneno ya Biblia kwamba mwanadamu hana uwezo wa “kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Sababu nyingine ni mtazamo wa watu kuelekea maonyo ya kiasili na yale yanayotolewa na wenye mamlaka.

Jifunze Kutambua Dalili

Mwanzoni lazima tukubali kwamba misiba ya asili inaweza kutokea bila onyo. Mhubiri 9:11 inasema: “Wakati na tukio lisilotazamiwa [hutupata sote].” Lakini mara nyingi, kunakuwa na maonyo, ya kiasili au kutoka kwa wenye mamlaka, kwamba hatari inakaribia. Hivyo, watu wanapotambua dalili, wanaweza kupata nafasi ya kuokoka.

Tsunami ilipopiga kisiwa cha Simeulue huko Indonesia, mnamo 2004, ni watu saba tu waliokufa kati ya maelfu ya watu. Kwa sababu wakazi wa eneo hilo wanajua kwamba maji yanaposonga mbali sana kutoka ufuoni kwa njia isiyo ya kawaida, inamaanisha kwamba tsunami iko karibu kutokea, wengi wao walikimbia walipoona hilo likitukia. Vivyo hivyo, watu wamepona dhoruba kali na milipuko ya volkano kwa kutii maonyo. Kwa sababu nyakati nyingine maonyo ya kiasili huwa yameanza mapema kabla ya maonyo kutoka kwa wenye mamlaka, ni jambo la hekima kufahamiana na yote, hasa ikiwa unaishi katika eneo ambalo misiba hutokea sana.

Hata hivyo, inasikitisha kwamba “watu wana mwelekeo wa kupuuza hatari hata wakati inapoonekana wazi,” anasema mtaalamu wa masuala ya volkano. Hilo ni kweli hasa kunapokuwa na maonyo ya uongo au mahali ambapo misiba ya kiasili ilitokea zamani sana. Wakati mwingine watu hawapendi kuacha mali zao za kimwili, hata inapokuwa wazi kwamba msiba utatokea.

Katika maeneo mengi watu ni maskini sana hivi kwamba inakuwa vigumu kwao kuhamia maeneo yenye usalama. Hivyo badala ya kudhani kwamba Muumba ndiye msababishaji wa misiba, umaskini unafunua kushindwa kwa wanadamu. Kwa mfano, mara kwa mara serikali hutumia pesa nyingi kununua silaha na kutumia kiasi kidogo kusaidia wenye uhitaji.

Hata hivyo, msaada wa kadiri fulani unapatikana kwa ajili ya watu wote bila kujali wana hali gani. Hilo linawezekanaje? Kwa sababu Mungu kupitia Neno lake, Biblia Takatifu, ametoa kanuni nzuri ambazo zikifuatwa zinaweza kuokoa uhai.

Kanuni Zinazookoa Uhai

Usimjaribu Mungu. Kumbukumbu la Torati 6:16 inasema hivi: “Msimjaribu Yehova Mungu wenu.” Wakristo wa kweli hawaamini kwa ushirikina kwamba Mungu atawalinda dhidi ya madhara yote yanayoweza kuwapata. Hivyo, kunapokuwa na hatari, wao hutii shauri lifuatalo katika Neno la Mungu: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.”—Methali 22:3.

Thamini uhai kuliko vitu vya kimwili. “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Ni kweli kwamba vitu vya kimwili vina sehemu yake, lakini haviwezi kutumiwa na mtu aliyekufa. Hivyo, watu wanaopenda uhai na wanaothamini pendeleo la kumtumikia Mungu, hawajihatarishi ili kulinda vitu vya kimwili.—Zaburi 115:17.

Mnamo 2004, Tadashi, anayeishi Japani, alitoka kwenye nyumba yake mara tu tetemeko la nchi lilipotukia hata kabla ya mamlaka kutoa maelekezo. Uhai wake ulikuwa na thamani sana kuliko vitu vya kimwili. Akira, ambaye anaishi katika eneo hilohilo aliandika kwamba “kiwango halisi cha uharibifu kinategemea si mali zilizopotea, bali mtazamo wa mtu mwenyewe. Niliona msiba huo kuwa nafasi nzuri ya kurahisisha maisha yangu.”

Sikiliza maonyo yanayotolewa na serikali. ‘Jitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa.’ (Waroma 13:1) Wenye mamlaka wanapotoa amri ya kuhama au ya kufuata hatua fulani za kiusalama, ni vizuri kutii. Tadashi alikaa mbali na eneo la hatari ili atii amri ya kuhama na hivyo akaepuka kujeruhiwa au kufa kutokana na matetemeko madogo baada ya tetemeko kubwa kutokea.

Kunapokuwa hakuna maonyo kutoka kwa wenye mamlaka kuhusu msiba unaokaribia lazima watu wajiamulie watatendaje, wakifikiria mambo yote yanayohusika. Katika maeneo fulani, serikali zinaweza kutoa miongozo inayofaa ili kuokoka msiba. Ikiwa miongozo kama hiyo inapatikana katika eneo lenu je, unaifahamu? Na je, umeizungumzia na familia yako? (Ona sanduku lililo katika ukurasa huu.) Katika sehemu nyingi za ulimwengu kwa kufuata mwelekezo wa ofisi ya tawi, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yamepanga utaratibu wa kufuata kunapokuwa na hali ya dharura, na miongozo hiyo imesaidia sana.

Onyesha upendo wa Kikristo. “Ninawapa ninyi amri mpya,” akasema Yesu, “kwamba mpendane, kama vile ambavyo nimewapenda ninyi.” (Yohana 13:34) Watu ambao hujidhabihu na kuonyesha upendo kama wa Kristo hufanya kila kitu wanachoweza ili kusaidiana kujitayarisha kwa ajili ya msiba wa asili na kukabiliana nao. Kwenye makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, wazee hufanya kazi kwa bidii ili kuwasiliana na washiriki wote wa kutaniko na kuhakikisha kwamba wako salama au wanaweza kufika mahali salama. Pia, wazee huchunguza ili kuhakikisha kwamba kila mmoja ana mahitaji ya lazima kama vile maji safi ya kunywa, chakula, mavazi, na dawa zinazohitajika. Familia za Mashahidi katika maeneo salama huwakaribisha Mashahidi wenzao wanaohitaji msaada. Kwa kweli upendo kama huo ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.

Je, misiba ya asili itakuwa mibaya zaidi kama watu fulani wanavyotabiri? Huenda ikawa hivyo, lakini si kwa muda mrefu. Kwa nini? Kwa sababu muda wa mwanadamu kuishi bila kumtegemea Mungu unakaribia kwisha. Baada ya hapo, dunia yote na wakazi wake itakuwa chini ya utawala wenye upendo wa Yehova, kukiwa na hali nzuri kama tutakavyoona sasa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Matetemeko ya nchi, hali mbaya ya hewa, milipuko ya volkano, na mambo mengine kama hayo hayawezi kusemwa kuwa ni misiba. Mambo hayo huitwa misiba ya asili yanapoathiri maisha ya wanadamu na kuharibu mali.

^ fu. 6 Ili kupata habari zaidi kuhusu sababu za Mungu za kuruhusu kuteseka na uovu, tafadhali ona makala zenye kichwa “‘Kwa nini?’—Kujibu Swali Gumu Zaidi,” zilizo katika Amkeni! la Novemba (Mwezi wa 11) 2006 na vilevile sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

JE, UKO TAYARI KUKIMBIA?

Ofisi ya Kukabiliana na Hali ya Dharura ya New York City, inapendekeza kwamba kila nyumba iwe na mpango wa kuhama kwa kutayarisha “mfuko wa dharura,” yaani mfuko imara, uliowekwa mahali panapofikika kwa urahisi, unaoweza kubebwa kwa urahisi, ulio na vifaa muhimu kwa ajili ya hali ya dharura. Vitu vifuatavyo vinaweza kuwekwa humo: *

▪ Nakala ya hati muhimu zikiwa ndani ya kifaa kisichoingiza maji

▪ Kishada cha ziada cha funguo za gari na nyumba

▪ Kadi za benki na pesa

▪ Maji ya kunywa na chakula kisichoharibika

▪ Tochi, redio inayoshika mawimbi ya AM/FM, simu ya mkononi (ikiwa unayo), betri za ziada

▪ Dawa za angalau juma moja, mwelekezo wa kuzitumia, cheti chenye maandishi ya daktari, na majina ya madaktari na namba zao za simu. (Hakikisha kwamba umeweka dawa mpya kabla muda wa zile ulizo nazo haujapita)

▪ Kisanduku cha huduma ya kwanza

▪ Viatu imara vinavyofaa na mavazi kwa ajili ya mvua

▪ Habari kwa ajili ya familia yako ya jinsi mtakavyowasiliana, na mahali pa kukutana na pia ramani ya eneo lenu

▪ Mahitaji ya mtoto mchanga

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 35 Ingawa mambo haya yametolewa kutoka kwenye orodha rasmi, tumetia ndani mabadiliko machache. Huenda si kila kitu kilichoonyeshwa kikafaa hali yako au sehemu unayoishi. Na pia huenda ukahitaji kuongeza vitu fulani. Kwa mfano, wazee na walemavu wana mahitaji yao ya pekee.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

USGS, David A. Johnston, Cascades Volcano Observatory