Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kutumia Njia za Kuzuia Uzazi?

Je, Ni Vibaya Kutumia Njia za Kuzuia Uzazi?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kutumia Njia za Kuzuia Uzazi?

UNAONAJE? Je, ni vibaya kwa watu waliofunga ndoa kutumia njia za kuzuia uzazi? Huenda jibu likategemea imani yako. Kanisa Katoliki linafundisha kwamba tendo lolote linalokusudiwa kuzuia uzazi “ni dhambi.” Kanisa Katoliki hufundisha kwamba kila mara wenzi wa ndoa wanapokuwa na mahusiano ya kingono, hakupaswi kuwa na chochote kinachoweza kuzuia uwezekano wa mimba kutungwa. Hivyo, kulingana na Kanisa Katoliki, kutumia njia yoyote ya kuzuia uzazi “ni marufuku.”

Watu wengi huona ni vigumu kukubali maoni hayo. Makala moja kuhusu suala hilo katika gazeti la Pittsburgh Post-Gazette, ilitaarifu kwamba “asilimia 75 ya Wakatoliki nchini Marekani wanasema kwamba kanisa linapaswa kuruhusu matumizi ya njia za kuzuia uzazi. . . . Na mamilioni kati yao hupuuza marufuku hiyo kila siku.” Mmoja wao, mama ya watoto watatu anayeitwa Linda, anakiri waziwazi kwamba yeye hutumia njia za kuzuia uzazi na anasema: “Siamini hata kidogo moyoni kwamba ninafanya dhambi.”

Neno la Mungu linasema nini kuhusu suala hilo?

Uhai Ni Wenye Thamani

Mungu huuona uhai wa mtoto kuwa wenye thamani, hata katika hatua za kwanza za ukuzi. Mfalme Daudi wa Israeli aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Uliniweka nikiwa nimekingwa katika tumbo la mama yangu. Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” (Zaburi 139:13, 16) Uhai huanza mimba inapotungwa, na kulingana na Sheria ya Musa, mtu angeweza kuchukuliwa hatua kwa kumuumiza mtoto ambaye hajazaliwa. Andiko la Kutoka 21:22, 23 linaonyesha wazi kwamba ikiwa mwanamke mja-mzito au mtoto wake ambaye hajazaliwa angekufa kwa sababu ya mapambano kati ya wanaume wawili, jambo hilo lilipaswa kuletwa mbele ya waamuzi. Wangekadiria hali na ni kwa kadiri gani jambo hilo lilifanywa kimakusudi, lakini malipo yangekuwa “nafsi kwa nafsi,” au uhai kwa uhai.

Kanuni hiyohiyo inatumika kuhusiana na njia za kuzuia uzazi kwa kuwa inaonekana kwamba baadhi ya njia hizo hutoa mimba. Njia hizo zinazotoa mimba hazipatani na kanuni ya Mungu ya kuheshimu uhai. Hata hivyo, njia nyingi za kuzuia uzazi hazitoi mimba. Je, ni vibaya kutumia njia hizo zisizotoa mimba?

Hakuna popote katika Biblia ambapo Wakristo wanaagizwa wazae. Mungu aliwaambia wenzi wawili wa kwanza na familia ya Noa hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” Lakini amri hiyo haikurudiwa kwa Wakristo. (Mwanzo 1:28; 9:1) Kwa hiyo, wenzi wa ndoa wanaweza kujiamulia wenyewe iwapo watapata watoto, idadi ya watoto, na wakati wa kuwapata. Pia, Maandiko hayashutumu njia za kuzuia uzazi. Hivyo, kulingana na Biblia, mume na mke wanaweza kujiamulia wenyewe iwapo watatumia njia fulani ya kuzuia uzazi isiyotoa mimba. Hata hivyo, kwa nini Kanisa Katoliki linashutumu njia za kuzuia uzazi?

Tofauti Kati ya Hekima ya Wanadamu na Hekima ya Mungu

Kichapo kimoja cha Kikatoliki kinaeleza kwamba katika karne ya pili W.K., wale waliodai kuwa Wakristo waliingiza katika dini kanuni ya Kistoiki ya kwamba kusudi pekee la ngono katika ndoa ni kuzaa. Hivyo basi, sababu ya kuchukua msimamo huo ilikuwa ya kifalsafa bali haikuwa ya kibiblia. Ilitegemea hekima ya wanadamu bali si ya Mungu. Falsafa hiyo iliendelezwa kwa karne nyingi na kufundishwa na wanatheolojia Wakatoliki. * Hata hivyo, fundisho hilo lilitokeza dhana ya kwamba kuwa na mahusiano ya kingono kwa kusudi tu la kujifurahisha ni dhambi, na hivyo kuwa na mahusiano ya kingono pasipo uwezekano wowote wa kuzaa ni kosa. Hata hivyo, hilo si fundisho la Kimaandiko.

Kitabu cha Biblia cha Methali kinatumia lugha ya kishairi kufafanua shangwe inayoweza kutokana na mahusiano ya kingono yanayofaa kati ya mume na mke: “Unywe maji ya birika lako mwenyewe, na maji yanayotiririka kutoka katikati ya kisima chako mwenyewe. Chemchemi yako ya maji na ibarikiwe, na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako, paa mwenye kupendeka na mbuzi wa milimani mwenye kuvutia. Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote. Upendo wake na ukufurahishe sikuzote.”—Met. 5:15, 18, 19.

Mahusiano ya kingono kati ya mume na mke ni zawadi kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, kusudi la mahusiano hayo si kuzaa tu. Mahusiano ya kingono huwapa wenzi wa ndoa nafasi ya kuonyeshana upendo. Kwa hiyo, wenzi wa ndoa wakiamua kuepuka kupata mimba kwa kutumia njia fulani ya kuzuia uzazi, huo ni uamuzi wao na hakuna mtu anayepaswa kuwahukumu.—Waroma 14:4, 10-13.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, kuna dhambi yoyote mume na mke kuwa na mahusiano ya kingono?—Methali 5:15, 18, 19.

▪ Wakristo wanapaswa kukumbuka nini iwapo watatumia njia za kuzuia uzazi?—Kutoka 21:22, 23.

▪ Wengine wanapaswa kuwaonaje wenzi wa ndoa wanaotumia njia za kuzuia uzazi?—Waroma 14:4, 10-13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Katika karne ya 13 Papa Gregori wa Tisa alipitisha ile ambayo kulingana na New Catholic Encyclopedia inaitwa “sheria ya watu wote iliyotolewa na papa inayokataza matumizi ya njia za kuzuia uzazi.”

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Mungu aliwaambia wenzi wa ndoa wa kwanza na familia ya Noa: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” Lakini amri hiyo haikurudiwa kwa Wakristo