Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Misiba Itakwisha Karibuni

Misiba Itakwisha Karibuni

Misiba Itakwisha Karibuni

MATETEMEKO ya nchi, vita, njaa, na magonjwa ni baadhi ya matukio ambayo Yesu alitabiri yangekuwa ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo” tunamoishi sasa. (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:7, 10, 11) Bila shaka, matukio hayo hayasababishwi na Mungu. Hatupaswi kumlaumu Yesu au Yehova Mungu, Baba yake, kwa sababu ya matukio hayo.

Lakini matukio hayo yaliyotabiriwa ni ishara ya mambo ambayo Mungu atafanya. Mungu atasimamisha Ufalme wake, yaani, serikali ya kimbingu mikononi mwa Yesu Kristo, na atawaangamiza wote wanaopinga enzi kuu ya Yehova. (Danieli 2:44; 7:13, 14) Baada ya hapo, dunia itakuwa mahali pa amani ambapo watu hawataogopa misiba ya asili. Ahadi hii ya Mungu itatimizwa kwa ukamili: “Watu wangu watakaa katika makao yenye amani na katika makao ya uhakika kamili na katika mahali pa kupumzika pasipo na usumbufu.”—Isaya 32:18.

Msikilize Mungu Ili Uishi!

Kama ilivyofafanuliwa katika makala iliyotangulia, kutii maonyo kunaweza kuokoa uhai. Kanuni hiyo inatumika hata zaidi katika maonyo ya Mungu yaliyotajwa katika Biblia. Mungu anaahidi: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kumsikiliza Mungu kwa kusoma kwa ukawaida Neno lake lililoongozwa kwa roho na kufuata mafundisho yake. Nao wanakutia moyo ufanye vivyo hivyo. Naam, wote ambao humsikiliza Yehova na kumtii, hawahitaji kuogopa wakati ujao au msiba utakaowapata waovu. Badala yake wanaweza kutazamia kupata uzima wa milele katika dunia Paradiso, ambapo “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

FARAJA KWA WANAOOMBOLEZA

Je, umempoteza mtu yeyote unayempenda katika kifo, labda kwenye msiba wa asili au kwa njia nyingine? Karibu miaka 2,000 hivi iliyopita, Lazaro aliyekuwa rafiki wa karibu wa Yesu alikufa. Alipojua kuhusu jambo hilo, Yesu alienda Bethania katika kijiji ambacho Lazaro alikuwa akiishi, naye akamfufua kutoka katika “usingizi” wa kifo.—Yohana 11:1-44.

Yesu hakufanya muujiza huo kuonyesha tu kwamba alimpenda Lazaro na familia yake, bali pia ili akazie ahadi yake ya kuwafufua “wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” wakati wa utawala wake. (Yohana 5:28, 29) Naam, katika Paradiso inayokuja Yesu ataondoa madhara yote ambayo yalisababishwa na uasi kule Edeni. *1 Yohana 3:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ili upate mashauri ya Kimaandiko ya jinsi unavyoweza kukabiliana na hali baada ya kumpoteza mpendwa wako kutia ndani habari zaidi kuhusu ahadi ya ufufuo, tafadhali ona broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

TETEMEKO LA NCHI LILIBADILISHA MAISHA YANGU

Mnamo 1971, nikiwa ningali msichana, nilikuwa na mtoto mchanga nami nilikuwa mwimbaji mashuhuri wa sauti ya soprano. Mnamo 1957, nilihama kutoka Winnipeg, Manitoba, Kanada ambako nilizaliwa na kwenda Hollywood, California, Marekani, ili kufuatilia kazi niliyopenda sana ya muziki.

Kila mwaka kwa miaka tisa, Mama, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, alisafiri kutoka Kanada ili kunitembelea. Alitumia pindi hizo kuzungumza nami kuhusu Biblia akiwa na hakika kwamba ilitoa mashauri bora zaidi kuhusu furaha na maisha ya familia. Nilimpenda Mama nami nilimsikiliza kwa sababu nilimheshimu. Hata hivyo, kila wakati alipoondoka nilitupa vichapo alivyokuwa akinipa nikiwa na uhakika kwamba maisha yangu yalikuwa yanaelekea mahali panapofaa.

Kisha mapema asubuhi ya Jumanne (Siku ya 2) Februari (Mwezi wa 2) 1971, niliamshwa na tetemeko la nchi lenye kipimo cha 6.6. Kulikuwa na kelele nyingi na mtikisiko mkubwa. Nikitetemeka kwa woga, nilimkimbilia mwanangu nami nikafurahi sana nilipomkuta akiwa salama kitandani. Mtikisiko huo ulipokoma, glasi zilizovunjika na vitu vilivyokuwa kabatini vilitapakaa sakafuni nayo maji yaliyokuwa ndani ya kidimbwi cha kuogelea yalikuwa yamemwagika kila mahali bustanini. Ingawa familia yangu ilikuwa salama usingizi wangu ulipotea.

Mama alikuwa amezungumza kuhusu “siku za mwisho,” ambazo zingekuwa na “matetemeko makubwa ya nchi.” (2 Timotheo 3:1; Luka 21:7-11) Mwaka huo mama alikuja kunitembelea kama kawaida yake lakini hakuwa na vichapo vyovyote vya Biblia. Baada ya kunihubiria kwa miaka tisa bila mafanikio, alikata kauli kwamba sipendezwi. Alikuwa amekosea sana! Alipofika tu, nilimuuliza maswali mengi sana. Mambo niliyoyaona kuwa muhimu maishani, yaani kuimba na umashuhuri, hayakuwa na umuhimu tena.

Juma hilohilo nilihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na Mama katika Jumba la Ufalme, na baada ya hapo nilihudhuria mikutano kwa ukawaida. Mama alipanga niwe na funzo la Biblia. Nilibatizwa mnamo 1973, na leo mimi hutumia saa 70 hivi kwa mwezi nikiwatangazia wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Badala ya kuvunja imani yangu katika Mungu, tetemeko la nchi lilinisaidia kuwa na imani.—Limesimuliwa na Colleen Esparza.