Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ilinde Familia Yako

Ilinde Familia Yako

“WASIO na upendo wa asili.” Biblia inatumia maneno hayo yenye kusikitisha kuwafafanua watu wengi wa siku zetu, kipindi kinachoitwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1, 3, 4) Kuenea kwa visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono katika familia hutoa uthibitisho wa wazi kwamba unabii huo ni wa kweli. Kwa kweli, neno la awali la Kigiriki aʹstor·gos, linalotafsiriwa katika Kiswahili “wasio na upendo wa asili,” linadokeza kutokuwa na upendo ambao unapaswa kuwa kati ya washiriki wa familia, hasa upendo kati ya wazazi na watoto. * Na mara nyingi visa vya watoto kutendewa vibaya kingono hutukia ndani ya familia.

Watafiti fulani wanasema kwamba mtu anayewatendea watoto vibaya kingono mara nyingi ni baba au baba wa kambo. Pia, wanaume wengine wa ukoo huwatendea watoto vibaya mara nyingi. Ingawa wengi wa wanaotendewa vibaya ni wasichana, wavulana wengi pia hutendewa hivyo. Lakini wanawake wanaowatendea watoto vibaya si wachache kama unavyofikiri. Huenda visa vya kutendewa vibaya kingono ambavyo haviripotiwi mara nyingi ni vile vinavyofanywa kati ya kaka na dada, ambapo mtoto mkubwa au mwenye nguvu zaidi anamwonea au kumshawishi ndugu au dada yake mdogo afanye vitendo vya ngono naye. Ukiwa mzazi, bila shaka matendo yote kama hayo ni yenye kuchukiza.

Unaweza kufanya nini ili matatizo kama hayo yasitokee katika familia yako? Kwa wazi, kila mtu katika kila familia anapaswa kujifunza na kuthamini kanuni fulani zinazopaswa kuzuia mwenendo wa kuwatendea wengine vibaya. Mahali panapofaa zaidi pa kupata mwongozo kama huo ni katika Neno la Mungu, Biblia.

Neno la Mungu na Uhusiano wa Kimwili

Ili kuwa salama, kila familia inahitaji kukubali viwango vya Biblia vinavyohusu maadili. Biblia inataja mambo wazi inapozungumza kuhusu ngono. Inataja mambo kwa njia ya heshima lakini bila kuficha. Inaonyesha kwamba Mungu alipanga uhusiano wa kingono uwe baraka kwa mume na mke. (Methali 5:15-20) Hata hivyo, inashutumu mahusiano ya kingono nje ya mpango wa ndoa. Kwa mfano, Biblia inapinga waziwazi mahusiano ya kingono kati ya watu wa ukoo. Katika Mambo ya Walawi sura ya 18, kuna orodha inayokataza mahusiano mbalimbali ya kingono kati ya watu wa ukoo. Ona maneno haya: “Yeyote kati yenu asimkaribie mtu yeyote wa jamaa yake, wa kimwili, wa karibu ili kufunua uchi [kufanya ngono]. Mimi ni Yehova.”—Mambo ya Walawi 18:6.

Yehova aliorodhesha matendo hayo kati ya “mambo . . . yenye kuchukiza” ambayo mtu alipaswa kuhukumiwa kifo kwa sababu ya kuyafanya. (Mambo ya Walawi 18:26, 29) Ni wazi kwamba Muumba ana viwango vya juu sana kuhusiana na mambo hayo. Leo, serikali nyingi zimechukua hatua kama hiyo kwa kutunga sheria dhidi ya kuwatendea watoto vibaya kingono katika familia. Mara nyingi, sheria husema kwamba mtoto anayeshiriki katika kitendo cha ngono na mtu mzima amelalwa kwa nguvu. Kwa nini isemwe hivyo ikiwa nguvu haikutumiwa?

Serikali nyingi zimekuja kutambua kile ambacho Biblia imesema kwa muda mrefu kuwahusu watoto, kwamba hawawezi kufikiri kama watu wazima. Kwa mfano, andiko la Methali 22:15 linasema: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” Na mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa . . . nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.”—1 Wakorintho 13:11.

Mtoto hawezi kuelewa maana halisi ya vitendo vya ngono, wala hawezi kuwazia madhara yatakayotukia kadiri miaka inavyopita. Hivyo, inakubalika kwamba watoto hawana uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na akili kuhusu ngono. Kwa maneno mengine, mtu mzima (au kijana mwenye umri mkubwa kiasi) akifanya ngono na mtoto, mtu huyo hawezi kusema kwamba mtoto huyo hakukataa au kwamba mtoto huyo alikubali. Mtu huyo amemlala mtoto huyo kwa nguvu. Huo ni uhalifu ambao mara nyingi adhabu yake ni kifungo. Lawama humwangukia anayemlala mtoto kwa nguvu, si mtoto ambaye hakukubali.

Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba wahalifu wengi hawapewi adhabu yoyote na wenye mamlaka. Kwa mfano, nchini Australia inakadiriwa kwamba asilimia 10 pekee ya watu wanaofanya matendo hayo ndiyo wanaoshtakiwa, na ni wachache tu wanaoadhibiwa. Mambo yako hivyohivyo katika nchi nyingine. Ingawa serikali haziwezi kufanya mengi ili kuilinda familia ya Kikristo, kutumia kanuni za Biblia kunaweza kusaidia sana.

Wakristo wa kweli wanatambua kwamba Mungu aliyeagiza kanuni hizo ziandikwe katika Neno lake hajabadilika. Yeye huona mambo yote tunayofanya kutia ndani yale yasiyoonwa na wanadamu wengine. Biblia inasema: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.”—Waebrania 4:13.

Mungu atatutoza hesabu ikiwa tutavunja sheria zake na kuwaumiza wengine. Kwa upande mwingine, anatubariki tukitii sheria zake zinazohusiana na maisha ya familia. Ni zipi baadhi ya sheria hizo?

Familia Iliyounganishwa na Upendo

Biblia inasema, “Upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Biblia haifafanui upendo kama hisia tu. Inafafanua sifa hiyo kwa njia ambayo inawachochea watu, yaani, upendo unachochea matendo mazuri na kuwafanya watu waepuke matendo ambayo Biblia inakataza. (1 Wakorintho 13:4-8) Katika familia, kuonyesha upendo humaanisha kumtendea kila mshiriki kwa staha, heshima, na fadhili. Inamaanisha kuishi kulingana na jinsi Mungu anavyomtaka kila mshiriki wa familia aishi. Mungu anampa kila mmoja jukumu muhimu na lenye heshima.

Akiwa kichwa cha familia, baba anapaswa kuchukua hatua ya kwanza kuonyesha upendo. Anaelewa kwamba baba Mkristo hajapewa ruhusa ya kuwa dikteta, akitumia mamlaka vibaya dhidi ya mke au watoto. Badala yake, anaiga mfano wa Kristo akiwa kichwa chake. (Waefeso 5:23, 25) Kwa hiyo, yeye humtendea mke wake kwa wororo na upendo naye huwa mwenye subira na wororo anaposhughulika na watoto wake. Yeye huwalinda na kujitoa ili kuzuia chochote kinachoweza kuharibu amani, kujiheshimu, kutumainiana, au hali ya kujihisi salama katika familia.

Vivyo hivyo, mke ambaye pia ni mama ana jukumu muhimu lenye kuheshimika. Biblia inatumia hisi ya mama katika jamii ya wanyama kufananisha ulinzi ambao Yehova na Yesu wanaweza kutoa. (Mathayo 23:37) Pia, mama wa kibinadamu anapaswa kuwalinda sana watoto wake. Kwa upendo, anapaswa kutanguliza usalama na hali njema ya watoto wake. Hakuna mzazi anayepaswa kutumia mamlaka vibaya, kuonea, au kutisha anaposhughulika na mwenzake au watoto, wala hawapaswi kuwaruhusu watoto watumie mbinu kama hizo kati yao.

Kadiri kila mshiriki wa familia anavyomtendea mwingine kwa heshima na staha, ndivyo kunavyozidi kuwa na mawasiliano mazuri. Mwandishi William Prendergast anasema: “Wazazi wote wanapaswa kuwa na mawasiliano ya karibu, ya kila siku kwa kawaida na watoto au vijana wao.” Anaongezea: “Inaonekana kwamba hilo ndilo suluhisho bora zaidi kwa tatizo la kuwatendea watoto vibaya kingono.” Kwa kweli, Biblia inapendekeza aina hiyo ya mawasiliano ya kawaida na ya upendo. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mwongozo huo unapotumiwa, nyumbani panakuwa pahali ambapo kila mshiriki wa familia anaweza kuzungumza kutoka moyoni kwa uhuru na kwa usalama.

Ni kweli kwamba tunaishi katika ulimwengu mwovu na hatuwezi kuzuia mambo yote mabaya. Lakini familia yenye usalama inaweza kusaidia sana. Mtu yeyote katika familia anapoumizwa, anajua mahali anapoweza kukimbilia ili afarijiwe na kuhurumiwa. Nyumba kama hiyo ni kama ngome, mahali salama katika ulimwengu huu wenye taabu. Mungu na abariki jitihada zako za kuhakikisha kwamba kuna usalama katika familia yako!

^ fu. 2 Neno hilo la Kigiriki limefafanuliwa kuwa: “Moyo mgumu kuelekea watu wa familia.” Hivyo, tafsiri moja ya Biblia inatafsiri mstari huo hivi: “Hawatakuwa na upendo wa kawaida kuelekea familia zao.”