Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

WATU wengi hawapendi kuzungumza kuhusu suala la kuwatendea watoto vibaya. Kufikiria tu kuhusu jambo hilo huwaogopesha wazazi wengi! Hata hivyo, hayo ni mambo yenye kuogopesha na yasiyopendeza katika ulimwengu wa leo, na watoto huathiriwa sana nayo. Je, inafaa kufikiria kuhusu jambo hilo? Ungetoa kitu gani ili kumlinda mtoto wako? Haigharimu chochote kujifunza kuhusu athari za kutendewa vibaya kingono. Kujua mambo hayo kunaweza kukusaidia kuwalinda watoto wako.

Usiache tatizo hilo likulemee na ukose ujasiri wa kukabiliana nalo. Hata ukihisi umelemewa, una nguvu ambazo mtoto wako hana, kwani mtoto wako anahitaji miaka mingi au hata makumi ya miaka ili awe na uwezo kama huo. Umepata ujuzi, uzoefu, na hekima kadiri ambavyo miaka imepita. Ili ufaulu unapaswa kutumia uwezo huo kumlinda mtoto wako. Tutazungumzia hatua tatu za msingi ambazo kila mzazi anaweza kuchukua. Hatua hizo ni: (1) Uwe ngao ya mtoto wako dhidi ya kutendewa vibaya, (2) mfundishe mtoto wako mambo yanayohitajika, na (3) mfundishe mtoto wako hatua za kuchukua anapokabiliwa na mambo hayo.

Je, Wewe Ni Ngao?

Wazazi ndio wenye daraka la kuwalinda watoto wao dhidi ya kutendewa vibaya kingono, si watoto. Hivyo, wazazi wanapaswa kuelimishwa kabla ya watoto. Ikiwa wewe ni mzazi, kuna mambo machache unayopaswa kujua kuhusu suala la kuwatendea watoto vibaya kingono. Unahitaji kujua ni watu wa aina gani wanaowatendea watoto vibaya na mbinu wanazotumia. Mara nyingi wazazi hufikiri kwamba watu wanaowatendea watoto vibaya kingono ni watu wasiojulikana ambao huvizia gizani, wakitafuta njia za kuwateka nyara au kuwalala kwa nguvu watoto wao. Ni kweli kwamba kuna watu kama hao. Mara nyingi tunasikia kuwahusu katika vyombo vya habari. Hata hivyo, watu kama hao ni wachache. Asilimia 90 hivi ya visa vya watoto kutendewa vibaya kingono, hufanywa na mtu ambaye tayari mtoto anamfahamu na kumtumaini.

Kiasili hupendi kuamini kwamba jirani mzuri, mwalimu, mfanyakazi wa huduma za afya, kocha, au mtu wa ukoo anaweza kuwa na uchu kumwelekea mtoto wako. Ni kweli, watu wengi hawako hivyo. Hakuna sababu ya kumtilia shaka kila mtu aliye karibu nawe. Hata hivyo, unaweza kumlinda mtoto wako kwa kujifunza jinsi watu wanaowatendea watoto vibaya kingono wanavyotenda.—Ona  sanduku kwenye ukurasa wa 6.

Kujua mbinu hizo kunaweza kukusaidia wewe mzazi, uwe tayari kuwa ngao kwa ajili ya mtoto wako. Kwa mfano, mtu fulani anayependezwa sana na watoto kuliko watu wazima akianza kumkazia uangalifu mtoto wako na kumpa zawadi au akijitolea kubaki nyumbani na mtoto wako au kwenda matembezi na mtoto wako, utafanya nini? Je, utafikiri kwamba mtu huyo anataka kumtendea mtoto wako vibaya kingono? La. Usikate kauli haraka. Si lazima tabia kama hiyo iwe na dosari. Hata hivyo, inaweza kukusaidia kuwa macho. Biblia inasema: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Kumbuka kwamba mtu akikuambia atakufanyia mengi kuliko ilivyo kawaida, kuna uwezekano mkubwa kwamba hana nia nzuri. Mchunguze kwa uangalifu mtu yeyote anayejitolea kutumia wakati akiwa peke yake na mtoto wako. Mjulishe mtu kama huyo kwamba utakuwa ukienda kumwona mtoto wako wakati wowote. Melissa na Brad, wazazi walio na wavulana watatu, ni waangalifu sana kuhusu kumwacha mtoto peke yake na mtu mzima. Mtoto wao mmoja alipotaka kujifunza muziki nyumbani, Melissa alimwambia mwalimu huyo: “Nitakuwa nikiingia mara kwa mara katika chumba hiki muda wote utakapokuwa hapa.” Huenda kufanya hivyo kukaonekana kuwa ulinzi unaopita kiasi, lakini wazazi hao wanaona inafaa kufanya hivyo kuliko kujuta baadaye.

Jihusishe sana katika utendaji wa mtoto wako, wafahamu rafiki zake, na upendezwe na kazi zake za shuleni. Anapoenda matembezi na mtu mwingine fahamu mambo yote watakayofanya. Mtaalamu mmoja wa afya ya akili ambaye ametumia miaka 33 akichunguza visa vya watu kutendewa vibaya kingono anasema kwamba ameona visa vingi ambavyo vingeweza kuzuiwa ikiwa tu wazazi wangekuwa macho. Anamnukuu mtu mmoja ambaye alihukumiwa kwa kuwatendea watoto vibaya kingono aliyesema: “Ni kana kwamba wazazi wenyewe hutuletea watoto wao. . . . Kwa kweli walifanya iwe rahisi sana kwangu.” Kumbuka, watu wengi wanaowatendea watoto vibaya kingono hutafuta mawindo rahisi. Wazazi wanaojihusisha sana katika maisha ya watoto wao hufanya iwe vigumu watoto wao kushambuliwa.

Kuwa msikilizaji mzuri ni njia nyingine unayoweza kuwa ngao ya mtoto wako. Si rahisi kwa mtoto kueleza waziwazi kwamba ametendewa vibaya kingono. Mara nyingi wao huaibika sana na kuhangaishwa na jinsi utakavyoitikia. Hivyo, sikiliza kwa makini uone kama kuna ujumbe fulani uliofichika. * Kama mtoto wako anakueleza jambo linalokuhangaisha, kwa utulivu uliza maswali ili kuufikia moyo wake. Ikiwa mtoto anakueleza kwamba hamtaki mlezi fulani, muulize ni kwa nini. Iwapo atakuambia ya kwamba mtu mzima fulani anacheza naye michezo ya ajabu-ajabu, muulize: “Hiyo ni michezo ya aina gani? Anafanya nini?” Akilalamika kwamba mtu fulani alimtekenya, muulize, “Alikutekenya sehemu gani?” Usipuuze majibu ya mtoto wako. Watu wanaowatendea vibaya watoto wanawaambia kwamba hakuna mtu atakayewaamini, na kwa kusikitisha mara nyingi hilo ndilo hutukia. Ili mtoto aliyetendewa vibaya kingono apone haraka anahitaji kuhisi kwamba anaaminiwa na ana utegemezo wa mzazi.

Uwe ngao ya mtoto wako

Wafundishe Watoto Wako Mambo Yanayohitajika

Kitabu fulani kinachozungumzia watoto kutendewa vibaya kilimnukuu mtu mmoja aliyehukumiwa kwa kuwatendea watoto vibaya akisema: “Ukinipa mtoto ambaye hajui chochote kuhusu ngono, utakuwa umenipa mtoto mwingine wa kumtendea vibaya.” Maneno hayo yanayotia hofu ni kikumbusha kinachofaa kwa wazazi. Inakuwa rahisi zaidi kuwadanganya watoto ambao hawajui chochote kuhusu ngono. Biblia inasema kwamba mtu anapokuwa na ujuzi na hekima anaweza kulindwa “kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu.” (Methali 2:10-12) Bila shaka hilo ndilo jambo unalotaka kwa ajili ya mtoto wako. Jambo la pili muhimu katika kumlinda mtoto wako, ni kumweleza waziwazi kuhusu suala hilo muhimu.

Unaweza kuwaelezaje mambo hayo? Wazazi wengi huaibika kuzungumza na watoto wao kuhusu ngono. Huenda mtoto wako akaaibika zaidi na hivyo huenda asije kuzungumza nawe kuhusu jambo hilo. Kwa hiyo, chukua hatua ya kwanza. Melissa anasema: “Tulianza mapema, kwa kuwafundisha majina ya viungo vya mwili. Tulitumia majina halisi, si majina ya badala, ili kuwaonyesha hakuna jambo la kuchekesha au la kuaibisha kuhusu viungo vyovyote vya miili yao.” Baada ya kufanya hivyo ni rahisi kuzungumza kuhusu kutendewa vibaya kingono. Wazazi wengi huwaeleza watoto wao kwamba viungo ambavyo hufichwa na chupi ni vya siri na vya pekee.

Heather aliyetajwa katika makala inayotangulia anasema: “Mimi na Scott tulimweleza mwana wetu kwamba uume wake ni kiungo cha siri na si kitu cha kuchezewa. Hakuna mtu anayepaswa kukichezea, iwe ni Mama, au Baba, au hata daktari. Tunapompeleka kwa daktari, mimi humweleza kwamba daktari atachunguza ikiwa ana ugonjwa wowote na hiyo ndiyo sababu huenda atakigusa kiungo hicho.” Wazazi wote wawili hushiriki katika mazungumzo hayo mara kwa mara, nao humhakikishia kwamba anaweza kuwaendea wakati wowote iwapo mtu yeyote atamgusa kwa njia isiyo sawa au kwa njia itakayomfanya ajihisi vibaya. Wataalamu wa kutunza watoto na kuzuia kutendewa vibaya kingono wanapendekeza kwamba wazazi wote wawe na mazungumzo kama hayo na watoto wao.

Watu wengi wameona kwamba kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu * kimewasaidia sana wanapowafundisha watoto jambo hilo. Sura ya 32, “Jinsi Yesu Alivyolindwa,” kina mashauri ya moja kwa moja lakini yanayofariji kwa ajili ya watoto kuhusu hatari za kutendewa vibaya na umuhimu wa kujilinda. Melissa anasema: “Kitabu hicho kimetusaidia kukazia mambo ambayo tayari tumewaeleza watoto wetu.”

Katika ulimwengu wa leo, watoto wanahitaji kujua kwamba kuna watu ambao wanapenda kuwashika-shika watoto au kuwafanya watoto wawashike katika njia zisizofaa. Maonyo hayo hayapaswi kuwajaza hofu watoto au kuwafanya wasiwaamini watu wazima wote. “Ni ujumbe tu wa tahadhari,” anasema Heather. “Hilo ni onyo moja kati ya maonyo mengi ambayo watoto wanapewa, mengi kati ya maonyo hayo hayahusiani na kutendewa vibaya kingono. Hayajafanya mtoto wangu awe na hofu.”

Mafunzo unayompa mtoto wako yanapaswa kutia ndani maoni yaliyosawazika kuhusu utii. Ni jambo muhimu na gumu kumfundisha mtoto kutii. (Wakolosai 3:20) Hata hivyo, mafundisho hayo hayapaswi kupita mpaka. Ikiwa mtoto atafundishwa kwamba wakati wote anapaswa kumtii mtu mzima yeyote, hata hali iweje, ni rahisi kwake kutendewa vibaya. Watu wanaowatendea watoto vibaya kingono hugundua haraka watoto wanaotii kila jambo. Wazazi wenye busara wanawafundisha watoto wao kwamba utii unapaswa kuwa wa kadiri. Hilo si jambo gumu kwa Wakristo. Wao huwaambia tu watoto: “Mtu yeyote akikuambia ufanye jambo ambalo Yehova Mungu anasema ni kosa, hupaswi kulifanya. Hata Mama au Baba hapaswi kukuambia ufanye jambo ambalo Yehova anasema ni kosa. Nawe unapaswa kumwambia Mama au Baba wakati wowote ambapo mtu atajaribu kukulazimisha ufanye jambo baya.”

Mwishowe, hakikisha kwamba mtoto wako anaelewa kuwa hakuna mtu anayepaswa kumwambia akufiche jambo lolote. Mwambie kwamba ikiwa mtu yeyote anamwambia akufiche jambo lolote, anapaswa kuja na kukujulisha. Haidhuru aambiwe nini, hata ikiwa atatishwa sana au ikiwa yeye wenyewe amefanya kosa fulani, sikuzote ni sawa kumwendea Mama au Baba na kumwambia jambo hilo. Mafundisho haya hayapaswi kumwogopesha mtoto wako. Unaweza kumhakikishia kwamba watu wengi hawafanyi mambo kama hayo, yaani, kumshika-shika sehemu asizopaswa, kumwambia asimtii Mungu, au kumwambia afiche jambo fulani. Kama tu mtu anayepanga njia ambayo atatumia ili kukimbilia moto unapozuka, mafundisho hayo kuhusu kutendewa vibaya kingono ni tahadhari tu ambazo huenda hazitahitajika.

Mfundishe mtoto wako mambo yanayohitajika

Mfundishe Mtoto Wako Hatua za Kujilinda

Hatua ya tatu ambayo tutazungumzia ni kumfundisha mtoto mambo rahisi ya kufanya mtu anapojaribu kumtumia vibaya wakati ambapo haupo. Njia moja ambayo hupendekezwa mara nyingi ni kama mchezo. Wazazi huuliza “Vipi ikiwa . . . ?” kisha mtoto anajibu. Unaweza kumwuliza, “Vipi ikiwa tulikuwa sokoni kisha tupoteane? Ungenitafutaje?” Huenda jibu la mtoto lisiwe lile ulilotazamia, lakini unaweza kumwelekeza kwa kutumia maswali ya ziada, kama vile “Je, unaweza kufikiria njia salama zaidi?”

Unaweza kutumia maswali kama hayo kumwuliza mtoto njia salama zaidi anayoweza kutumia mtu akijaribu kumshika-shika sehemu isiyofaa. Ikiwa mtoto anashtushwa na maswali kama hayo, unaweza kusimulia hadithi inayomhusu mtoto mwingine. Kwa mfano: “Msichana fulani ana mtu wa ukoo ambaye anampenda, lakini mtu huyo anajaribu kumshika-shika sehemu isiyofaa. Unafikiri anapaswa kufanya nini ili awe salama?”

Mfundishe mtoto wako hatua za kujilinda

Unapaswa kumfundisha mtoto wako afanye nini katika hali kama hiyo iliyotajwa? Mwandishi mmoja anasema hivi: “Kusema ‘Sitaki!’ kwa ujasiri au ‘Usifanye hivyo!’ au ‘Niache!’ humwogopesha sana mtu anayejaribu kumshawishi na kumfanya aache kumlazimisha.” Msaidie mtoto wako aonyeshe kwa ufupi jinsi atakavyofanya ili awe na ujasiri wa kukataa kwa sauti, kukimbia, na kukueleza yaliyotukia. Mtoto ambaye anaonekana ameelewa mazoezi hayo anaweza kusahau baada ya majuma au miezi michache. Kwa hiyo uwe na kawaida ya kurudia mazoezi hayo.

Watu wote wanaomlea mtoto huyo, kutia ndani wa kiume, iwe ni baba, baba wa kambo, au wanaume wengine wa ukoo, wanapaswa kuhusishwa katika mazungumzo hayo. Kwa nini? Kwa sababu ni kama wote wanaohusika katika mafundisho hayo wanamwahidi mtoto kwamba hawatawahi kumtendea vibaya kwa njia hiyo. Kwa kusikitisha, mara nyingi watu wanaowatendea watoto vibaya kingono huwa watu wa familia. Makala inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kuifanya familia yako iwe salama katika ulimwengu uliopotoka.

^ fu. 10 Wataalamu wanasema kwamba watoto wengi ambao wanatendewa vibaya kingono, hutoa ishara zinazoonyesha kwamba kuna tatizo bila kuzungumza. Kwa mfano, mtoto akianza kurudia tabia alizokuwa ameacha kama vile, kukojoa kitandani, kila wakati kutaka kuwa karibu na wazazi wake, au kuogopa anapoachwa peke yake, anaweza kuwa akitoa ishara ya kwamba ana tatizo kubwa. Dalili kama hizo si uthibitisho wa kwamba anatendewa vibaya kingono. Kwa utulivu muulize mtoto wako ikiwa kuna tatizo linalomsumbua ili uweze kumfariji, kumhakikishia kwamba utamtegemeza, na kumlinda.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.