Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ambavyo Jina la Mungu Limejulishwa

Jinsi Ambavyo Jina la Mungu Limejulishwa

Jinsi Ambavyo Jina la Mungu Limejulishwa

MTUNGA-zaburi wa Biblia, Daudi, aliimba hivi: “Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo.” Daudi alilijua jina la Mungu, na katika wimbo wake alihimiza hivi: “Na abarikiwe Yehova . . . Jina lake tukufu na libarikiwe.” (Zaburi 69:30; 72:18, 19) Jina la Mungu linalotumiwa sana katika Kiswahili ni Yehova, ambalo limetafsiriwa kutokana na jina la Kiebrania יהוה, linalopatikana mara 7,000 hivi katika Biblia.

Katika karne za karibuni, jina la Mungu limetumiwa pia mahali pengine pengi. Kwa mfano, maneno ya Kilatini, Benedictus Sit Iehova Deus,  ambayo yanamaanisha “Yehova Mungu na Asifiwe,” yanapatikana katika sarafu za dhahabu zilizotengenezwa kwa miaka mingi huko Uswisi [1]. Kwa kweli, kwa kipindi cha mamia ya miaka iliyopita, jina la Mungu katika Kiebrania na Kilatini limeonekana katika maelfu ya sarafu na medali.

Ni nini kilichofanya jina la Mungu litumiwe sana kama vile mifano iliyo katika ukurasa huu na unaofuata inavyoonyesha?

Kwa Nini Jina la Mungu Lilitumiwa?

Kuanzia karne ya 16, vita vya kidini kati ya Wakatoliki na Waprotestanti vilizuka kotekote Ulaya Magharibi. Majimbo kadhaa yaliyomilikiwa na Hispania yalijiondoa kutoka katika Kanisa Katoliki ambayo ndiyo iliyokuwa dini kubwa, badala yake, yakapendelea kujiunga na Dini ya Kiprotestanti. Hilo lilisababisha vita vya kidini vya wenyewe kwa wenyewe. Sarafu na picha zilizokuwa juu ya sarafu hizo zilitumiwa kupitisha ujumbe kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono upande mmoja au mwingine katika vita hivyo.

Jinsi Jina la Mungu Lilivyotumiwa

Watu wanaotia nakshi kwenye vyuma waliandika jina la Mungu, Yehova, kwa kutumia herufi nne za Kiebrania zinazoitwa Tetragramatoni. Herufi hizo hutafsiriwa katika Kiswahili kuwa JHVH au YHWH. Kwa ujumla, watia nakshi na watu wa kawaida hawakujua kusoma Kiebrania. Kwa hiyo, Tetragramatoni ziliponakiliwa tena na tena, herufi hizo nne za Kiebrania za jina la Mungu ziliandikwa kwa njia tofauti.

Sweden ilitengeneza sarafu yake ya kwanza yenye jina la Mungu karibu mwaka wa 1568 [2], na Scotland ilifanya hivyo mnamo 1591. Mnamo 1600, Mfalme wa Sweden, Charles wa Tisa, aliandika jina la Mungu kwenye sarafu katika njia mbalimbali kama vile, Ihehova, Iehova, na Iehovah [3]. Alifanya sarafu ya aina moja itengenezwe kwa dhahabu. Sarafu hiyo ilikuwa na thamani ya mshahara wa miezi minne wa kibarua!

Kuna zaidi ya aina 60 za sarafu zilizoitwa eti za Yehova tangu wakati wa Christian wa Nne, aliyekuwa mfalme wa Denmark na Norway kuanzia 1588 hadi 1648. Kufikia katikati ya karne ya 17, “sarafu za Yehova” zilitengenezwa huko Poland na Uswisi, na pia zilitengenezwa huko Ujerumani.

Wakati wa vile Vita vya Miaka 30 ambavyo vilipiganwa huko Ulaya kuanzia 1618 hadi 1648 na ambavyo vilianza kama vita vya kidini, sarafu hizo zilitengenezwa kwa wingi. Baada ya vita vya ushindi huko Breitenfeld mnamo 1631, Mfalme wa Sweden, Gustav Adolph wa Pili aliagiza sarafu zilizokuwa na Tetragramatoni zitengenezwe [4]. Sarafu hizo zilitengenezewa katika mji ya Erfurt, Fürth, Mainz, na Würzburg. Wakati huohuo, majimbo yaliyokuwa yakimuunga mkono mfalme wa Sweden yalianza pia kutengeneza sarafu zenye jina la Mungu.

Katika kipindi cha miaka 150 hivi baada ya vile Vita vya Miaka 30, jina la Mungu liliendelea kuwekwa kwenye sarafu na medali. Sarafu hizo zilitengenezewa Austria, Mexico, Ufaransa, Urusi, na vilevile katika nchi nyingine. Hata hivyo, mapema katika karne ya 18, jina la Mungu lilitumiwa katika njia hiyo mara chache sana. Mwishowe, ni kana kwamba liliacha kuwekwa kwenye sarafu na mihuri.

Kufanya Jina la Mungu Lijulikane

Ingawa huenda jina la Mungu haliwekwi kwenye pesa leo, linatangazwa sana na kwa njia inayofaa. Miaka mingi iliyopita, Mungu alichagua watu ambao wangemtumikia, naye aliwaambia hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu.” (Isaya 43:12) Hakuna sarafu inayoweza kutimiza kazi hiyo muhimu. Wale waliotumia jina la Mungu kwenye sarafu zao walitoa ushahidi wa uwongo kumhusu Mungu kwa kuwa walidai kwamba alikuwa akiwaunga mkono katika vita vyao vikatili. Hata hivyo, leo wanadamu fulani wanawajulisha watu jina la Mungu katika njia anayokubali.

Mashahidi wa Yehova wanakutia moyo ujifunze mengi kumhusu Mungu wa kweli, Yehova, na maana ya jina lake. Mtunga-zaburi wa Biblia aliandika hivi kumhusu Yehova: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Ni muhimu kumjua Yehova kwa kuwa Mwana wake mpendwa alisema hivi katika sala: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Vifaa vya kutia nakshi kwenye sarafu

[Picha katika ukurasa wa 20 zimeandaliwa na]

Coin 1 and tools: Hans-Peter-Marquardt.net; coin 2: Mit freundlicher Genehmigung Sammlung Julius Hagander

[Picha katika ukurasa wa 21 zimeandaliwa na]

Coins 3 and 4: Mit freundlicher Genehmigung Sammlung Julius Hagander