Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Sisi Huogopa Kifo?

Kwa Nini Sisi Huogopa Kifo?

Kwa Nini Sisi Huogopa Kifo?

“Kifo ndicho kitu kibaya zaidi kwani huo ndio mwisho.”—Aristoto.

WENGI walimwona kuwa mwanamke mcha-Mungu, muumini wa kweli. Wengine hata walimwita “nguzo ya kanisa lake.” Alifundishwa kwamba kifo si mwisho, bali ni njia ya kuingia katika maisha mengine. Hata hivyo, alipokaribia kufa alishikwa na hofu kubwa. Akiwa na mashaka mengi, mwanamke huyo alimuuliza hivi mshauri wake wa kiroho, ‘Kuna mafundisho mengi kuhusu kinachotupata tunapokufa; utajuaje ni fundisho gani la kweli?’

Karibu katika kila dini na jamii, watu wamefundishwa kwamba wanadamu huendelea kuishi, au wataishi tena, baada ya kufa. Kati ya mafundisho hayo yote, ni lipi lililo la kweli? Watu wengi hutilia shaka kwamba watu huendelea kuishi baada ya kufa. Namna gani wewe? Je, umefundishwa kwamba mtu huendelea kuishi baada ya kufa? Je, unaamini hivyo? Je, unaogopa kifo?

Kuogopa Kutokuwapo

Wachunguzi hufafanua hofu ya kifo kuwa “wasiwasi kuhusu kifo.” Katika miaka ya karibuni vitabu vingi na ripoti za kisayansi zimeandikwa kuhusu hali hiyo. Hata hivyo, bado watu wengi hawapendi kufikiria kuhusu kifo. Lakini wakati fulani tunalazimika kufikiria jambo hilo. Uhai wa mwanadamu ni mfupi sana kwani zaidi ya watu 160,000 hivi hufa kila siku! Kila mwanadamu bila kubagua, anaweza kufa na uhakika huo unawatisha wengi.

Wataalamu wanasema kwamba watu huwa na wasiwasi kuhusu kifo kwa sababu nne. Sababu hizo zinatia ndani hofu ya maumivu, hofu ya mambo yasiyojulikana, hofu ya wapendwa wetu kufa, na hofu ya jinsi kifo chetu kitakavyowaathiri wapendwa wetu.

Jambo linalowatia watu wasiwasi sana kati ya sababu hizo nne ni hofu ya kutokuwapo tena. Haidhuru wana imani gani ya kidini, wazo la kwamba kifo ndio mwisho wa maisha huwaogopesha watu wengi. Nayo sayansi huchochea hofu hiyo. Sasa utendaji mwingi wa mwili wa mwanadamu unaweza kuelezwa kupitia sayansi. Kwa kweli, hakuna mwanabiolojia, mwanafizikia, au mwanakemia ambaye amewahi kugundua ndani yetu kitu fulani kisichoonekana ambacho kinaweza kuendelea kuishi baada ya mwili kufa. Kwa hiyo, wanasayansi wengi hueleza kifo cha mwanadamu kuwa utendaji wa kibiolojia.

Kwa hiyo, haishangazi kwamba watu wengi ambao wanaonekana kuwa na imani yenye nguvu kuhusu uhai baada ya kifo, huenda wakawa wanaogopa kufa na kutokuwapo tena. Kwa kushangaza, katika maandishi yake, Mfalme Sulemani wa kale alieleza kifo cha mwanadamu kuwa mwisho, jambo ambalo huenda watu fulani wakaona kuwa lenye kuogopesha.

Je, “Mavumbi” Ndio Mwisho wa Mambo Yote?

Katika kitabu cha Mhubiri kilichoandikwa miaka 3,000 iliyopita, Sulemani aliandika hivi: “Walio hai wanajua kwamba kifo kitawapata, lakini wafu hawajui lolote, nao hawana thawabu tena, kwa sababu hawana kumbukumbu tena. Upendo wao na chuki yao na wivu wao umekwisha.” Aliongeza kusema: “Chochote kilicho katika uwezo wa mkono wako, kifanye kwa nguvu zako zote, kwa kuwa hakuna kazi, wala wazo, wala ujuzi, wala hekima mahali pa wafu ambapo wewe unaenda.”—Mhubiri 9:5, 6, 10, The Bible in Basic English.

Pia, Sulemani akiongozwa na roho alisema kwamba “mwisho wa binadamu na mwisho wa mnyama ni uleule. Jinsi anavyokufa binadamu ndivyo anavyokufa mnyama. . . . binadamu si bora kuliko mnyama. . . . Wote hufa na kwenda mahali pamoja. Wote wametoka mavumbini, na wote watarudi mavumbini.”—Mhubiri 3:19, 20, Biblia Habari Njema.

Ingawa maneno hayo yaliyoonyeshwa juu yaliandikwa na Mfalme Sulemani, yaliongozwa na roho ya Mungu na ni sehemu ya Biblia, Neno lake lililoandikwa. Maandiko hayo, pamoja na mengine mengi katika Biblia, hayaungi mkono imani ambayo watu wengi wanayo kwamba kitu fulani ndani yetu huendelea kuishi katika umbo fulani baada ya sisi kufa. (Mwanzo 2:7; 3:19; Ezekieli 18:4) Je, basi Mungu anatuambia kwamba “mavumbi,” au kutokuwapo, ndio mwisho kabisa wa wanadamu wote? Bila shaka la!

Biblia haifundishi kwamba sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Hata hivyo, inatoa tumaini la wazi kwa ajili ya wote wanaokufa. Makala inayofuata itaonyesha kwa nini hupaswi kuogopa kuwa kifo ndio mwisho kabisa wa maisha ya mwanadamu.

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

ADUI ASIYEWEZA KUEPUKIKA

Kifo kimetajwa kuwa adui ya mwanadamu. Ni adui halisi, na kuna uthibitisho wa kutosha. Kulingana na kadirio moja, watu milioni 59 hivi hufa kila mwaka, wastani wa watu 2 kila sekunde. Hebu ona tarakimu zifuatazo kuhusu kifo.

▪ Mtu mmoja hufa kwa sababu ya vita kila sekunde 102.

▪ Mtu mmoja huuawa kila sekunde 61.

▪ Mtu mmoja hujiua kila sekunde 39.

▪ Mtu mmoja hufa kutokana na aksidenti ya barabarani kila sekunde 26.

▪ Mtu mmoja hufa kutokana na njaa kila sekunde tatu.

▪ Mtoto mmoja wa chini ya umri wa miaka mitano hufa kila sekunde tatu.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

UTAFITI USIO NA MATOKEO YOYOTE

Novemba 9, 1949 (9/11/1949), James Kidd, mchimba shaba mwenye umri wa miaka 70, alitoweka katika milima ya Arizona, Marekani. Miaka kadhaa baadaye, kifo chake kilipotangazwa rasmi, wosia wake ulipatikana pamoja na pesa na hati za hisa zenye thamani ya mamia ya maelfu ya dola. Katika wosia wake, Kidd alisema kwamba pesa zake zitumiwe katika utafiti wa kutafuta “uthibitisho wa kisayansi kwamba kuna nafsi katika mwili wa mwanadamu ambayo hutoka mtu anapokufa.”

Muda mfupi baadaye, zaidi ya watu 100 waliodai kuwa watafiti na wanasayansi waliomba wapewe pesa hizo. Hoja zao zilisikilizwa mahakamani kwa miezi mingi na maelfu ya madai yalitolewa kuonyesha kwamba kuna nafsi isiyoweza kuonekana. Mwishowe, hakimu aliyapa mashirika mawili ya utafiti yenye sifa nzuri pesa hizo. Hata hivyo, zaidi ya miaka 50 baadaye, bado watafiti hao hawajatoa “uthibitisho wa kisayansi kwamba kuna nafsi katika mwili wa mwanadamu ambayo hutoka mtu anapokufa.”