Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tutunze Mazingira?

Kwa Nini Tutunze Mazingira?

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Tutunze Mazingira?

HUENDA shughuli za wanadamu zinaidhuru sayari yetu sasa kuliko wakati mwingine wowote. Matatizo kama vile kuongezeka kwa joto duniani yanapozidi kuwa mabaya, wanasayansi, serikali, na viwanda vinazidisha jitihada za kukabiliana na hali hiyo.

Je, sisi mmoja-mmoja tuna wajibu wa kusaidia kutunza mazingira? Ikiwa ndivyo, tunaweza kusaidia kwa kadiri gani? Biblia inatoa sababu nzuri kwa nini tunapaswa kufanya mambo yenye manufaa kwa dunia. Pia inatusaidia tuwe na usawaziko katika jitihada zetu.

Kutenda Kupatana na Kusudi la Muumba

Yehova Mungu aliumba dunia iwe makao ya bustani kwa ajili ya wanadamu. Alisema kwamba kila kitu alichokuwa amefanya kilikuwa “chema sana” na akampa mwanadamu mgawo wa ‘kuilima na kuitunza dunia.’ (Mwanzo 1:28, 31; 2:15) Mungu anahisije kuhusu hali ya sasa ya dunia? Kwa wazi, yeye anachukizwa sana mwanadamu anapokosa kuitunza dunia, kwa kuwa Ufunuo 11:18 inatabiri kwamba ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ Kwa hiyo, hatupaswi kupuuza hali ya dunia.

Biblia inatuhakikishia kwamba uharibifu wote ambao mwanadamu amesababisha utarekebishwa Mungu ‘atakapofanya vitu vyote kuwa vipya.’ (Ufunuo 21:5) Hata hivyo, hatupaswi kukata kauli kwamba kwa kuwa Mungu atarekebisha hali duniani, si lazima tujali sana tunafanya nini sasa. Matendo yetu ni muhimu! Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna maoni kama ya Mungu kuhusu sayari yetu na kwamba tunaunga mkono mapenzi yake kwamba igeuzwe kuwa paradiso?

Kusaidia Kuisafisha Dunia

Shughuli za kawaida za wanadamu hutokeza kiasi fulani cha takataka. Kwa hekima Yehova alibuni mizunguko ya asili ya dunia ili kuondoa takataka hizo, kusafisha hewa, maji, na ardhi. (Methali 3:19) Mambo tunayofanya yanapaswa kupatana na mizunguko hiyo. Hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu tusishiriki katika kuharibu zaidi mazingira ya dunia. Utunzaji kama huo unaonyesha kwamba tunawapenda majirani zetu kama sisi wenyewe. (Marko 12:31) Fikiria mfano katika nyakati za Biblia.

Mungu aliagiza taifa la Israeli lizike kinyesi cha wanadamu “nje ya kambi.” (Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Hilo lilifanya kambi iwe safi na uchafu ulioza haraka. Vivyo hivyo, leo Wakristo hujitahidi kutupa takataka upesi na kwa njia inayofaa. Tahadhari kubwa inapaswa kuchukuliwa tunapotupa vifaa vyenye sumu.

Takataka nyingi zinaweza kuboreshwa ili zitumiwe tena. Ikiwa sheria inasema kwamba takataka zitumiwe tena basi kutii sheria kama hizo ni sehemu ya kumlipa “Kaisari vitu vya Kaisari.” (Mathayo 22:21) Huenda jitihada nyingi zaidi zikahitajika ili kutumia tena takataka, lakini kufanya hivyo kunaonyesha kuwa mtu anatamani kuona dunia ikiwa safi.

Kuhifadhi Maliasili za Dunia

Ili kutimiza mahitaji yetu ya chakula, makao, na mafuta, na hivyo kuendeleza uhai wetu, lazima tutumie maliasili za dunia. Kutambua kwetu kwamba mali hizo ni zawadi kutoka kwa Mungu kutaonekana tunapotumia mali hizo. Waisraeli walipotamani nyama jangwani, Yehova aliwapa kware wengi sana. Pupa iliwafanya watumie vibaya na kwa ubinafsi zawadi hiyo, nao wakamkasirisha sana Yehova Mungu. (Hesabu 11:31-33) Mungu hajabadilika tangu wakati huo. Kwa sababu hiyo, Wakristo wenye dhamiri nzuri huepuka kutumia maliasili vibaya kwani kufanya hivyo kunaweza kuwa ishara ya pupa.

Huenda wengine wakaona kuwa wana haki ya kutumia nishati au mali nyingine za asili kupita kiasi. Lakini, maliasili hazipaswi kutumiwa vibaya eti kwa sababu tunaweza kuzigharimia au ziko kwa wingi. Baada ya Yesu kulisha umati mkubwa, alielekeza kwamba samaki na mikate iliyosalia ikusanywe. (Yohana 6:12) Alijitahidi asipoteze kile ambacho Baba yake alikuwa ameandaa.

Kuwa na Usawaziko

Kila siku sisi hufanya maamuzi yanayoathiri mazingira. Je, tuchukue hatua za kupita kiasi kama vile kujitenga na jamii ya wanadamu ili kuepuka kuidhuru dunia? Biblia haipendekezi mahali popote jambo kama hilo. Fikiria mfano wa Yesu. Alipokuwa duniani, aliishi maisha ya kawaida ambayo yalimwezesha kutimiza kazi aliyopewa na Mungu ya kuhubiri. (Luka 4:43) Isitoshe, Yesu alikataa kujihusisha katika siasa ili kutatua shida za jamii ya wakati huo. Alisema hivi waziwazi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.

Hata hivyo, ni muhimu kwetu kufikiria jinsi tunavyodhuru mazingira tunapofanya maamuzi fulani kama vile kununua vifaa vya nyumbani, kusafiri, na kujihusisha na tafrija. Kwa mfano, wengine huamua kununua vitu ambavyo vimeundwa au vinavyotumika katika njia ambayo haiharibu sana mazingira. Wengine hujitahidi kupunguza muda wanaotumia katika utendaji unaochangia uchafuzi au unaotumia vibaya maliasili.

Hakuna haja kwa mtu yeyote kuwalazimisha wengine wafuate maamuzi yake kuhusu kutunza mazingira. Hali hutofautiana ikitegemea mtu binafsi na eneo analoishi. Lakini sisi sote tunawajibika kibinafsi kwa sababu ya maamuzi tunayofanya. Kama Biblia inavyosema, “kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.”—Wagalatia 6:5.

Muumba aliwapa wanadamu daraka la kutunza dunia. Kuthamini mgawo wetu na kumheshimu Mungu na kazi zake za uumbaji kwa unyenyekevu kunapaswa kutuchochea tufanye maamuzi ya akili na ya kudhamiria kuhusu jinsi tunavyoitunza dunia.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, Mungu atachukua hatua ili kurekebisha mazingira yetu?—Ufunuo 11:18.

▪ Mungu amewakabidhi wanadamu daraka gani kuhusu dunia?—Mwanzo 1:28; 2:15.

▪ Yesu Kristo aliweka mfano gani wa kuepuka kutumia vitu vibaya?—Yohana 6:12.