Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu na Kristo Wana Maoni Gani Kuhusu Wanawake?

Mungu na Kristo Wana Maoni Gani Kuhusu Wanawake?

Mungu na Kristo Wana Maoni Gani Kuhusu Wanawake?

TUNAWEZA kupataje picha kamili ya jinsi ambavyo Yehova Mungu huwaona wanawake? Njia moja ni kwa kuchunguza mtazamo na mwenendo wa Yesu Kristo, kwani yeye ndiye “mfano wa Mungu asiyeonekana,” naye huonyesha kikamili maoni ya Mungu kuhusu mambo mbalimbali. (Wakolosai 1:15) Jinsi ambavyo Yesu aliwatendea wanawake katika siku zake huonyesha kwamba Yehova na Yesu wanawaheshimu wanawake na hawaungi mkono kamwe ukatili dhidi ya wanawake ambao umeenea sana katika nchi nyingi leo.

Kwa mfano, fikiria pindi ambayo Yesu alizungumza na mwanamke kwenye kisima. Simulizi katika Injili ya Yohana linasema hivi: “Mwanamke mmoja wa Samaria akaja kuteka maji. Yesu akamwambia: ‘Nipe maji ninywe.’” Yesu alikuwa tayari kuzungumza na mwanamke Msamaria hadharani, hata ingawa Wayahudi wengi hawakuwa na shughuli na Wasamaria. Kulingana na The International Standard Bible Encyclopedia, kwa Wayahudi, “mazungumzo pamoja na mwanamke katika mahali pa hadharani lilikuwa jambo la kuchukiza hasa.” Hata hivyo, Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima na ufikirio, naye hakuwabagua watu kwa sababu ya jamii au jinsia yao. Tofauti na hilo, Yesu alijitambulisha waziwazi kwa mara ya kwanza kuwa yeye ndiye Masihi alipoongea na mwanamke huyo Msamaria.—Yohana 4:7-9, 25, 26.

Pindi nyingine Yesu alifikiwa na mwanamke ambaye kwa miaka 12 alikuwa ameteseka kutokana na mtiririko wa damu wenye kuaibisha na kudhoofisha. Alipomgusa, alipona mara moja. “Yesu akageuka, akamwona, na kusema: ‘Jipe moyo, binti yangu; imani yako imekuponya.’” (Mathayo 9:22) Kulingana na Sheria ya Musa, mwanamke aliyekuwa na ugonjwa huo hakupaswa kuchangamana na umati, sembuse kumgusa mtu yeyote. Hata hivyo, Yesu hakumkemea. Badala yake, alimfariji kwa huruma na kumwita “binti.” Neno hilo lilimtuliza kama nini! Na lazima Yesu awe alifurahi kama nini kumponya!

Baada ya Yesu kufufuliwa, alimtokea kwanza Maria Magdalene na mwanafunzi mwingine ambaye Biblia inamtaja kuwa “yule Maria mwingine.” Yesu angeweza kumtokea kwanza Petro, Yohana, au mwanafunzi mwingine wa kiume. Badala yake, aliwastahi wanawake hao kwa kuwaruhusu kuwa watu wa kwanza kuona ufufuo wake. Malaika aliwaagiza wawaambie wanafunzi wa kiume wa Yesu kuhusu tukio hilo lenye kustaajabisha. Yesu aliwaambia hivi wanawake hao: “Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu.” (Mathayo 28:1, 5-10) Ni wazi kwamba Yesu hakuwa ameathiriwa na maoni ya ubaguzi yaliyokuwa yameenea sana kati ya Wayahudi siku hizo, ambayo yalisema kwamba wanawake hawakupaswa kutoa ushahidi mahakamani.

Hivyo, badala ya kuwabagua wanawake au kuunga mkono mtazamo wa kwamba wanaume ni bora kuliko wanawake, Yesu alionyesha kwamba anawaheshimu na kuwathamini wanawake. Kuwatendea kwa jeuri kulikuwa kinyume cha mafundisho ya Yesu na mtazamo wake, na tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu alionyesha kikamili maoni ya Baba yake, Yehova.

Wanawake Wanaolindwa na Mungu

“Hakuna mahali katika eneo la Mediterania la kale au katika Mashariki ya Karibu ambapo wanawake walipewa uhuru wanaofurahia katika jamii ya Magharibi ya kisasa. Maoni ya kawaida yalikuwa kwamba wanawake walikuwa wa hali ya chini kuliko wanaume, kama vile watumwa walivyokuwa wa hali ya chini kuliko watu walio huru, na wachanga kuliko wazee. . . . Watoto wa kiume walistahiwa zaidi kuliko wa kike, na nyakati nyingine watoto wachanga wasichana waliachwa nje bila ulinzi ili wafe.” Hivyo ndivyo kamusi moja ya Biblia hufafanua mtazamo uliokuwa umeenea kuelekea wanawake zamani. Mara nyingi walionwa kama watumwa.

Biblia iliandikwa wakati ambapo jamii zilionyesha mtazamo huo. Hata hivyo, sheria ya Mungu katika Biblia iliwapa wanawake heshima kubwa, tofauti na mtazamo uliokuwa katika utamaduni mbalimbali wa kale.

Masimulizi mbalimbali yanayoonyesha jinsi Yehova alivyotenda kwa niaba ya wanawake yanathibitisha kwamba anawajali waabudu wake wanawake. Mara mbili aliingilia kati ili kumlinda Sara asilalwe kinguvu. (Mwanzo 12:14-20; 20:1-7) Mungu alimpendelea Lea, mke wa Yakobo ambaye hakupendwa sana, kwa ‘kufungua tumbo lake la uzazi,’ naye akazaa mwana. (Mwanzo 29:31, 32) Wazalishaji wawili Waisraeli ambao walimwogopa Mungu walipohatarisha uhai wao ili kuwalinda watoto wa kiume Waebrania wasiuawe huko Misri, Yehova alionyesha uthamini wake kwa ‘kuwapa familia.’ (Kutoka 1:17, 20, 21) Pia alijibu sala ya Hana ambayo alitoa kwa bidii. (1 Samweli 1:10, 20) Na mjane wa nabii fulani alipokabiliwa na mkopeshaji ambaye alitaka kuchukua watoto wake kuwa watumwa ili kulipia deni lake, Yehova hakumwacha. Kwa upendo, Mungu alimwezesha nabii Elisha aongeze mafuta yake ili alipe deni, na bado abaki na mafuta ya kutosha kwa ajili ya familia yake. Hivyo akahifadhi familia yake na heshima yake.—Kutoka 22:22, 23; 2 Wafalme 4:1-7.

Mara nyingi manabii walishutumu zoea la kuwatumia vibaya wanawake au kuwatendea jeuri. Nabii Yeremia aliwaambia hivi Waisraeli katika jina la Yehova: “Toeni haki na uadilifu, nanyi mumkomboe yeye anayenyang’anywa kutoka mkononi mwa mpunjaji; wala msimtendee vibaya mkaaji mgeni yeyote, mvulana asiye na baba au mjane. Msiwatendee jeuri yoyote. Wala msimwage damu yoyote isiyo na hatia mahali hapa.” (Yeremia 22:2, 3) Baadaye, matajiri na wenye mamlaka katika Israeli walishutumiwa kwa sababu ya kuwafukuza wanawake kutoka nyumbani mwao na kuwatendea watoto wao kwa ukatili. (Mika 2:9) Mungu wa haki huona na kushutumu uovu huo ambao wanawake na watoto wao hutendewa.

“Mke Mwema”

Maoni yanayofaa kuhusu mke mwema yanatolewa na mwandikaji wa kale wa Methali. Kwa kuwa maelezo hayo maridadi kuhusu wajibu na heshima ya mke yameandikwa katika Neno la Yehova, tunaweza kuwa na hakika kwamba anayakubali. Badala ya kumkandamiza au kumwona kuwa wa hali ya chini, mwanamke kama huyo huthaminiwa, huheshimiwa, na kuaminiwa.

“Mke mwema” anayetajwa katika Methali sura ya 31 ni mfanyakazi mwenye bidii. Anafanya kwa bidii kazi “inayopendeza mikono yake,” naye hufanya biashara na hata kuuza na kununua mashamba. Yeye huona shamba na kulinunua. Yeye hutengeneza mavazi ya ndani na kuyauza. Naye huwapa wafanya-biashara mishipi. Yeye ni mwenye nguvu na bidii katika utendaji wake. Isitoshe, maneno yake ya hekima na fadhili zake zenye upendo zinathaminiwa sana. Kwa sababu hiyo, yeye huheshimiwa sana na mume wake, wana wake, na muhimu zaidi, Yehova pia humheshimu.

Wanawake hawapaswi kukandamizwa na wanaume ambao huwatumia vibaya, huwatesa, au huwatendea ukatili wa aina yoyote ile. Badala yake, mwanamke aliyeolewa anapaswa kuwa “msaidizi” mwenye furaha na mwenye ustadi wa mume wake.—Mwanzo 2:18.

Wapeni Heshima

Akiwaandikia waume Wakristo kuhusu jinsi wanavyopaswa kuwatendea wake zao, Petro, mwandikaji aliyeongozwa na roho, aliwahimiza waige mtazamo wa Yehova na Yesu Kristo. ‘Enyi waume, endeleeni kuwapa heshima,’ akaandika. (1 Petro 3:7) Kumpa mtu heshima hutoa wazo la kwamba unamthamini na kumheshimu sana. Hivyo, mtu anayemheshimu mke wake hamwaibishi, hamshushii heshima, au kumtendea kwa jeuri. Badala yake, yeye huonyesha kwa maneno na matendo, hadharani na faraghani, kwamba anamthamini na kumpenda.

Kwa kweli kumheshimu mke huchangia furaha katika ndoa. Fikiria mfano wa Carlos na Cecilia. Wakati fulani katika ndoa yao, walijikuta wakibishana bila kusuluhisha jambo lolote. Nyakati nyingine, waliacha kuzungumziana. Hawakujua jinsi ya kutatua matatizo yao. Carlos alikuwa mjeuri; naye Cecilia alikuwa mwenye kudai mengi na mwenye kiburi. Hata hivyo, walipoanza kujifunza Biblia na kufuata waliyojifunza, hali yao ilianza kuwa bora. Cecilia anasema: “Ninatambua kwamba mafundisho ya Yesu na mfano wake umebadili utu wangu na wa mume wangu. Kwa sababu ya mfano wa Yesu, nimekuwa mnyenyekevu zaidi na sidai mengi. Nimejifunza kutafuta msaada wa Yehova kupitia sala, kama Yesu alivyofanya. Carlos amejifunza kuwa mvumilivu na kujizuia, na kumheshimu mke wake kama Yehova anavyotaka.”

Ndoa yao si kamilifu, lakini imedumu kwa miaka mingi. Katika miaka ya karibuni wamekabili hali ngumu sana. Carlos alipoteza kazi yake na akafanyiwa upasuaji kwa sababu ya kansa. Hata hivyo, matatizo hayo hayakutikisa ndoa yao, ambayo imekuwa imara zaidi.

Tangu wanadamu wafanye dhambi na kupoteza ukamilifu, wanawake katika utamaduni mbalimbali wamevunjiwa heshima. Wametendewa vibaya kimwili, kiakili, na kingono. Lakini Yehova hakukusudia watendewe kwa njia hiyo. Biblia inaonyesha wazi kwamba haidhuru maoni ya kidesturi ambayo yanashikiliwa na watu wengi, wanawake wote wanapaswa kutendewa kwa staha na heshima. Ni haki yao kutoka kwa Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Mwanamke Msamaria

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Mwanamke mgonjwa

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Maria Magdalene

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yehova alimlinda Sara mara mbili

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ndoa ya Carlos na Cecilia ilikuwa karibu kuvunjika

[Picha katika ukurasa wa 7]

Picha ya karibuni ya Carlos na Cecilia