Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukichwa Katika Ndoa Unamaanisha Nini?

Ukichwa Katika Ndoa Unamaanisha Nini?

Maoni ya Biblia

Ukichwa Katika Ndoa Unamaanisha Nini?

KATIKA nchi nyingi sherehe za ndoa zinatia ndani viapo vya ndoa na wakati huo mke anaahidi kumtii mume wake. Hata hivyo, wanawake wengi hawapendi wazo la ukichwa wa wanaume katika ndoa. Fikiria kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu jambo hili. Utagundua kwamba msimamo wa Biblia umesawazika na una matokeo mazuri.

Mungu Anaufafanuaje Ukichwa?

Biblia inafafanua ukichwa katika andiko la Waefeso 5:22-24: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko . . . Kwa kweli, kama kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote.” Akiwa “kichwa cha mke wake,” mume anapaswa kuongoza mambo katika familia, naye mke afuate mwongozo wa mume na kuheshimu ukichwa wake.—Waefeso 5:33.

Mume ana mamlaka ya kadiri kwani anapaswa kujitiisha kwa Mungu na Kristo. Hajapewa mamlaka ya kumwongoza mke wake avunje sheria za Mungu au atende kinyume na dhamiri yake iliyoongozwa na Biblia. Hata hivyo, katika mipaka hiyo, Mungu amempa wajibu wa kufanya maamuzi muhimu kwa ajili ya familia.—Waroma 7:2; 1 Wakorintho 11:3.

Biblia inamwamuru mume atumie ukichwa wake bila ubinafsi kwa kutanguliza masilahi ya mke wake kabla ya masilahi yake. Waefeso 5:25 inasema hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” Mume anayefuata mfano bora wa Kristo wa upendo anakataa kutumia ukichwa kwa ubinafsi.

Isitoshe, Biblia inamwagiza mwanamume aishi na mke wake “kulingana na ujuzi.” (1 Petro 3:7) Hilo halimaanishi tu kutambua tofauti za kimwili na kihisia kati ya wanaume na wanawake. Anapaswa kuelewa mahitaji ya mke wake.

“Yeye Ni Mwenzako”

Je, ujitiisho wa mke unamaanisha hapaswi kufanya chochote? Mfikirie Sara, anayetajwa katika Biblia kuwa mfano kwa sababu alimtii mume wake, Abrahamu. (1 Petro 3:5, 6) Alijitiisha kwake katika mambo makubwa na madogo. Kwa mfano aliacha nyumba yenye starehe na kuanza maisha ya kuhama-hama na kulala katika mahema, naye alitii katika mambo madogo kama vile kutayarisha chakula wakati ambao hakutarajia. (Mwanzo 12:5-9; 18:6) Hata hivyo, katika jambo fulani zito mara kadhaa alitoa maoni yaliyopingana na ya Abrahamu. Hayo yalitukia alipotaka Abrahamu amfukuze kijakazi wake, Hagari pamoja na mwana wake wa kwanza, Ishmaeli. Badala ya kumshutumu Sara, Mungu alimwambia Abrahamu ‘aisikilize sauti yake.’ Lakini katika pindi hiyo, Sara aliendelea kujitiisha kwa Abrahamu kwa kumngoja ashughulikie mambo badala ya kujaribu kuwafukuza Hagari na Ishmaeli yeye mwenyewe.—Mwanzo 21:8-14.

Mfano wa Sara unaonyesha kwamba mke hapaswi kumfuata mume wake kama kipofu, badala yake anapaswa kuwa ‘mwenzake’ anayeheshimika. (Malaki 2:14) Akiwa mwenzake, ana jukumu muhimu kuhusu maamuzi ya familia na ana kiasi fulani cha mamlaka katika familia, mara nyingi anatimiza mambo fulani katika nyumba hata mambo yanayohusu pesa. Bila shaka, mume akiwa kichwa ana jukumu la kufanya uamuzi wa mwisho.—Methali 31:10-31; 1 Timotheo 5:14.

Kumheshimu Mwanzilishi

Yehova Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke, naye alianzisha ndoa ili iwe muungano wenye heshima kati yao. (Mwanzo 2:18-24) Pia alimpa mume na mke majukumu ambayo yanaweza kuwaletea shangwe nyingi zaidi.—Kumbukumbu la Torati 24:5; Methali 5:18.

Akiwa Mwanzilishi wa ndoa, Yehova ana haki na uwezo wa kuweka viwango vya kufuatwa katika mpango wa ndoa. Wenzi wa ndoa wanaotimiza majukumu yao na kufuata mpango wa Mungu wa ukichwa, si tu kwa sababu mpango huo unafaa bali pia kwa sababu ya kuheshimu mamlaka ya kimungu, wanapata kibali na utegemezo wake.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni nani aliyeweka mfano bora wa ukichwa?—Waefeso 5:25.

▪ Je, Mungu ameweka mipaka kwa mamlaka ya mume?—1 Wakorintho 11:3.

▪ Kusudi la mpango wa ndoa na ukichwa ni nini?—Methali 5:18.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ukichwa unaofuata mfano wa Kristo unaleta furaha na unawaridhisha wenzi wote wawili