Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tatizo la Uhalifu Linaweza Kutatuliwa?

Je, Tatizo la Uhalifu Linaweza Kutatuliwa?

Je, Tatizo la Uhalifu Linaweza Kutatuliwa?

“Uchunguzi unaonyesha kwamba wahalifu wanaofanya uhalifu kwa kurudia wataendelea kusumbua jamii hata baada ya kutoka gerezani, na gahrama za uhalifu wao ambazo si za kifedha tu zitaendelea kuongezeka.”—Kitabu Inside The Criminal Mind, cha Dakt. Stanton E. Samenow.

HATA iwe unaishi wapi, kila siku inaonekana ni kana kwamba inakuja na aina nyingine za uhalifu wenye kutisha hata zaidi. Kwa hiyo inafaa kuuliza: Je, vizuizi kama vile adhabu kali, vifungo vya gereza, na kadhalika vinafanya kazi? Je, magereza yanawafanya wahalifu waache uhalifu? Na jambo muhimu hata zaidi, Je, jamii inakabiliana na kiini cha uhalifu?

Dakt. Stanton E. Samenow anaandika hivi kuhusu njia za sasa za kukabiliana na uhalifu: “Baada ya kufungwa gerezani, [mhalifu] anaweza kujifunza mbinu za kuwa mjanja na mwangalifu zaidi, lakini anaendelea na njia yake ya maisha na kuzidi kufanya uhalifu. Takwimu zinazoonyesha ikiwa mtu amerudia kufanya uhalifu huonekana tu mtu anapokamatwa tena.” Kwa hiyo, magereza yamekuwa kama vyuo vya wahalifu, yakiwasaidia bila kukusudia kuboresha ustadi wao.—Ona sanduku “Je, Magereza Ni Vyuo vya Uhalifu?” kwenye ukurasa wa 7.

Isitoshe, mara nyingi wahalifu hawaadhibiwi, na hivyo kuwafanya wafikiri kwamba uhalifu una faida. Maoni hayo yanawafanya wawe jasiri na sugu zaidi. Mtawala mmoja mwenye hekima alisema hivi: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.”—Mhubiri 8:11.

Je, Wanachagua Kuwa Wahalifu au Wanasukumwa na Hali?

Je, watu fulani hufanya uhalifu kwa sababu hawana njia nyingine yoyote ya kujikimu? Samenow anasema hivi: “Niliona uhalifu kuwa hali ya kawaida au isiyoweza kuepukika hasa ikiwa mtu ni maskini sana, hana uwezo, na amekosa tumaini.” Hata hivyo, baada ya uchunguzi mwingi alibadili maoni yake. Alikata kauli hivi: “Wahalifu huchagua kufanya uhalifu. Uhalifu . . . ‘unasababishwa’ na jinsi ambavyo [mtu] anafikiri, na si kwa sababu ya mazingira yake.” Samenow anaendelea kusema hivi: “Tabia inasababishwa hasa na kufikiri kwa mtu. Kila kitu tunachofanya kinatanguliwa, kinaambatana, na kinafuatwa na kufikiri kwa mtu.” Kwa hiyo, badala ya kuwaona wahalifu kuwa wanafanya uhalifu bila kukusudia, Samenow alikata maneno kwamba “wao ndio wanaowaonea wengine kwa kuwa wamechagua njia hiyo ya maisha.” *

Jambo kuu ni kwamba “wamechagua.” Kwa kweli, kichwa kimoja katika gazeti moja la Uingereza hivi karibuni kilikuwa: “Uhalifu Ni Kazi Inayochaguliwa na Vijana wa Mjini Wanaotaka Hali Bora.” Hata hali zikiwa ngumu, wanadamu wana uhuru wa kuchagua na hivyo wanaweza kuchagua ni maisha ya aina gani watakayoishi. Kwa kweli, mamilioni ya watu kila siku hukabiliana na ukosefu wa haki na umaskini, au wanaishi katika familia zilizovunjika; lakini hawawi wahalifu. Samenow anasema hivi: “Wahalifu ndio husababisha uhalifu, wala si mazingira mabaya, malezi mabaya, . . . au ukosefu wa kazi. Uhalifu uko katika akili za wanadamu na hausababishwi na hali za kijamii.”

Uhalifu Huanzia Moyoni

Biblia inakazia mtu wa ndani na si hali zake. Yakobo 1:14, 15 inasema: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.” Mtu anapofikiria mawazo mabaya, anakuza tamaa mbaya. Hilo linaweza kumwongoza atende mabaya. Kwa mfano, kupendezwa kijuu-juu tu na picha au habari za ngono kunaweza kumwongoza mtu apendezwe kupita kiasi na ngono, na hilo linaweza kumsukuma atende kulingana na tamaa zake, labda hata kwa kuvunja sheria.

Jambo lingine tunalopaswa kutilia maanani ni kwamba ulimwengu hukazia ubinafsi, pesa, raha, na kutosheleza tamaa mara moja. Biblia ilitabiri hivi kuhusu nyakati zetu: “Katika siku za mwisho . . . , watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wakali, wasiopenda wema, [na] wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-5) Inasikitisha kwamba kupitia sinema, michezo ya video, vitabu na watu mashuhuri ambao hawaweki mfano mzuri, ulimwengu huendeleza tabia ambazo huchochea uhalifu zaidi. * Hata hivyo, si lazima watu mmoja-mmoja waathiriwe na mambo hayo. Kwa kweli, watu fulani ambao waliathiriwa na mambo hayo wakati mmoja wamebadilisha kabisa mtazamo na maisha yao.

Watu Wanaweza Kubadilika!

Mtu akifanya uhalifu haimaanishi atakuwa mhalifu daima. Kitabu Inside the Criminal Mind kinasema kwamba kama vile tu huenda mtu akachagua kuishi maisha ya uhalifu, mtu huyo pia “anaweza kuchagua mwelekeo mpya na kujifunza kuishi maisha manyofu.”

Kuna mifano mingi inayoonyesha kwamba watu wa malezi mbalimbali wanaweza kubadilika. * Wanachohitaji ni kuwa tayari kubadili mtazamo, nia, na kufikiri kwao ili kupatane na viwango imara vya Muumba wetu wala si viwango vinavyobadilika-badilika vya wanadamu. Kwa kweli hakuna mtu anayetujua vizuri zaidi kuliko Muumba wetu. Zaidi ya hayo, Mungu ana haki ya kuamulia wanadamu lililo sawa na lililo kosa. Ili kutimiza hilo, Mungu alitumia roho yake kuwaongoza wanaume 40 hivi waandike kile ambacho tunajua kuwa Biblia Takatifu—kitabu chenye kustaajabisha ambacho kinaweza kuitwa kwa kufaa mwongozo wa wanadamu wa kupata maisha yenye furaha na yenye kusudi.—2 Timotheo 3:16, 17.

Huenda isiwe rahisi kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kumpendeza Mungu, kwa kuwa tunahitaji kushindana na mwelekeo wetu wa kufanya dhambi. Kwa kweli, mwandikaji mmoja wa Biblia alielezea kushindana kwake na mwelekeo huo kuwa kama ‘pigano’! (Waroma 7:21-25) Alishinda pigano hilo kwa sababu hakutegemea nguvu zake bali zile za Mungu, ambaye Neno lake lililoongozwa na roho “liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

Faida za “Lishe” Bora

Ili mtu awe na afya bora, anahitaji chakula kizuri. Pia ni lazima chakula hicho kitafunwe vizuri na kumeng’enywa, jambo ambalo linahitaji wakati na jitihada. Vivyo hivyo, ili tuwe na afya kiroho tunahitaji “kutafuna” maneno ya Mungu ili yaingie katika akili na moyo wetu. (Mathayo 4:4) Biblia inasema hivi: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo . . . , na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—Wafilipi 4:8, 9.

Ona kwamba ni lazima ‘tuendelee kuyafikiria’ mawazo ya Mungu ikiwa tunataka kuvua utu wa zamani na kuvaa utu mpya. Subira inahitajiwa, kwa kuwa ukuzi wa kiroho hautokei mara moja.—Wakolosai 1:9, 10; 3:8-10.

Fikiria mfano wa mwanamke mmoja ambaye alitendewa vibaya kingono alipokuwa mtoto; alianza kutumia dawa za kulevya, vileo, na sigara; na sasa anatumikia kifungo cha maisha kwa sababu ya uhalifu mbalimbali. Akiwa gerezani, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na kuthamini kweli alizojifunza. Matokeo yalikuwa nini? Polepole, utu wake wa zamani ulianza kupotea na akavaa utu mpya ulio kama wa Kristo. Sasa yeye si mtumwa wa fikira na matendo yenye kuangamiza. Andiko analopenda ni 2 Wakorintho 3:17 linalosema: “Basi Yehova ndiye Roho; na mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” Ndiyo, hata ingawa bado yuko gerezani, anafurahia uhuru ambao hajawahi kuwa nao.

Mungu Ni Mwenye Rehema

Machoni pa Mungu, kila mtu anaweza kubadilika. * Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, anasema hivi: “Nimekuja kuwaita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi watubu.” (Luka 5:32) Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kubadilika na kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Lakini watu walio na subira na wanaokubali msaada wa Mungu, kutia ndani msaada wenye upendo kutoka kwa Wakristo wakomavu kiroho hufaulu. (Luka 11:9-13; Wagalatia 5:22, 23) Ili kutoa msaada huo, Mashahidi wa Yehova hutembelea magereza ulimwenguni pote ili kujifunza Biblia na wanaume na wanawake ambao wamefanya uhalifu wa kila aina. * Mashahidi pia hufanya mikutano ya Kikristo kila juma katika magereza mengi.—Waebrania 10:24, 25.

Hata ingawa wahalifu fulani wameacha njia zao na kuwa Wakristo wa kweli, Biblia inasema waziwazi kuhusu “kuongezeka kwa uasi-sheria.” (Mathayo 24:12) Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, utabiri huo ni sehemu ya unabii mkubwa ambao una habari njema.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ugonjwa wa akili unaweza kuchangia uhalifu, hasa kwenye nchi ambazo wagonjwa hao wanaachwa waranderande mitaani ambako wanaweza kupata silaha. Hata hivyo, makala hii haizungumzii suala hilo.

^ fu. 11 Kwa habari zaidi kuhusu uhalifu, ona Amkeni! la Februari 22, 1998 (22/2/1998), ukurasa wa 3-9, chini ya kichwa, “Ulimwengu Usio na Uhalifu—Lini?” na Septemba (Mwezi na 9) 1986, ukurasa wa 3-12, chini ya kichwa, “Uhalifu Utaisha Katika Barabara Zetu?”

^ fu. 14 Gazeti hili na gazeti Mnara wa Mlinzi, mara nyingi yamesimulia kuhusu watu waliochochewa na kweli za Biblia kuacha maisha ya uhalifu. Ona Amkeni! la Julai (Mwezi wa 7) 2006, ukurasa wa 11-13, na Oktoba 8, 2005 (8/10/2005), ukurasa wa 20-21, kutia ndani Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2000 (1/1/2000), ukurasa wa 4-5; Oktoba 15, 1998, ukurasa wa 27-29; na Februari 15, 1997, ukurasa wa 21-24.

^ fu. 21 Ona makala “Maoni ya Biblia: Je, Mungu Husamehe Dhambi Nzito?” kwenye ukurasa wa 10.

^ fu. 21 Ona sanduku “Msaada wa Kiroho kwa Wafungwa,” kwenye ukurasa wa 9.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Mamilioni ya watu maskini si wahalifu

[Sanduku/ Picha katika ukurasa wa 6, 7]

“WANAKAMATWA TENA KABLA YA MIAKA MIWILI KWISHA”

Chini ya kichwa hicho, gazeti The Times la London huko Uingereza, liliripoti kwamba zaidi ya asilimia 70 ya watu nchini Uingereza waliohukumiwa kwa sababu ya kuvunja nyumba na kuiba wanakamatwa tena kabla ya miaka miwili kwisha. Uhalifu mwingi unafanywa na waraibu wa dawa za kulevya ambao wanatafuta pesa za kununua dawa hizo ghali, zinazowadhuru.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

“JE, MAGEREZA NI VYUO VYA UHALIFU?”

“Magereza yamekuwa vyuo vya uhalifu,” aliandika Profesa John Braithwaite katika kichapo chake UCLA Law Review. Dakt. Stanton E. Samenow anasema hivi katika kitabu chake Inside the Criminal Mind: “Wahalifu wengi hujifunza kutokana na mambo yanayowapata,” lakini hawajifunzi kile ambacho jamii inajaribu kuwafundisha. “Huko gerezani,” anaandika, “mtu ana wakati mwingi sana wa kujifunza jinsi ya kuwa mhalifu bora. . . . Kwa kweli wengine wamekuwa wahalifu wenye mafanikio zaidi, wakijitumbukiza kwenye uhalifu lakini wakiwa wajanja ili wasikamatwe.”

Katika sura nyingine ya kitabu chake, Samenow anasema: “Kifungo hakibadili utu wa mhalifu. Iwe yuko barabarani au gerezani, yeye huwasiliana na wengine, hujifunza mbinu mpya za uhalifu, na kupitisha madokezo fulani kwa wahalifu wengine.” Kijana mmoja mhalifu alisema hivi: “Kufungwa kumenistahilisha kuwa mwalimu wa uhalifu.”