Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Safina ya Noa na Uundaji wa Meli (Januari 2007) Nilijua kwamba safina ilitengenezwa kwa njia ya ajabu, lakini sikuelewa kabisa uzuri wake. Makala hiyo ilieleza kwa njia rahisi na yenye kueleweka jinsi urefu, upana, na kimo chake kilivyoifanya ifae kwa usafiri. Niliamua kutengeneza muundo wa safina hiyo pamoja na vijana katika kutaniko letu, tukitumia picha iliyoonyeshwa. Tulitengeneza wanyama kwa karatasi na kuwatia ndani ya safina hiyo na tukachora picha ya Noa na familia yake. Tulijifunza mengi zaidi kuhusu tukio hilo la Biblia kwa kujihusisha katika masimulizi hayo. Asanteni sana.

T. A., Japani

Mwana wangu mwenye umri wa miaka sita hupenda kutengeneza vitu. Mimi na yeye tulifurahi sana kupata maagizo ya jinsi ya kujenga safina ndogo ya Noa. Makala yenu nzuri ilifanya tuwe na alasiri moja yenye kupendeza sana. Tukiwa tunaishi katika ulimwengu wenye shughuli nyingi na mikazo ambayo vijana wetu wanakabili kila juma shuleni, ni baraka kama nini kuwa na kifaa kama Amkeni! kinachowasaidia wazazi kuwalea watoto wao katika njia za Yehova.

M. F., Marekani

Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kushindaje Tatizo Hili? (Novemba 2006) Moyo wangu uliguswa niliposoma makala hiyo na kutambua jinsi Yehova anavyotujali na kutusaidia kutatua matatizo yetu. Hata ingawa tunaweza kurudia matendo mabaya, Yehova yuko “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Kutambua jambo hilo husaidia vijana ‘wakimbie tamaa zinazotukia ujanani.’—2 Timotheo 2:22.

V.F.F., Brazili

Vijana Huuliza . . . kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana? (Desemba 2006) Nimekuwa nikijifunza Biblia kwa miaka sita sasa. Ingawa wazazi wangu ni wakali kutuelekea sisi watoto, ninajua kwamba wananijali sana. Niliposoma makala hiyo, ilinisaidia kuelewa mahangaiko ya wazazi wangu na ikanisaidia kuthamini utunzaji wa kibinafsi ambao Yehova ananionyesha.

K. T., Thailand

Nilikuwa Mwana Mpotevu (Desemba 2006) Nilianza kujifunza kumhusu Yehova mwaka wa 1992. Lakini kuna wakati maishani nilipotaka kuishi kwa njia tofauti na ile ya Yehova. Kama tu Meros Sunday, nilipata matatizo mengi, na baada ya miaka mitatu ya kumwacha Yehova, nilianza kumwomba msaada. Sasa nimemrudia tena! Asanteni sana kwa kazi yenu.

D. K., Ukrainia

Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kuanza Urafiki wa Karibu na Mtu wa Jinsia Tofauti Lini? (Januari 2007) Nina umri wa miaka 15. Nilipomtembelea shangazi na mjomba, nilikutana na mvulana Shahidi mwenye umri wa miaka 17. Tulianza kuwasiliana kwenye Intaneti. Mwanzoni, tulifanya hivyo mara chache tu. Lakini baada ya muda, tukawa tukiwasiliana kila siku, na tukaanzisha uhusiano wa karibu. Kisha nikasoma makala hiyo na kutambua kwamba tulikuwa tumeanzisha urafiki wa karibu sana. Kwa msaada wa wazazi wangu na makala hiyo katika Amkeni!, nilifanya uamuzi unaofaa zaidi, yaani, kuvunja uhusiano wangu na mvulana huyo. Bado sisi ni marafiki, lakini nimeweka uhusiano wangu na Yehova kwanza. Ninashukuru sana kwamba makala hiyo ilinisaidia kurudiwa na fahamu.

D. D., Kanada