Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini ya Kweli Je, Ni Moja Tu?

Dini ya Kweli Je, Ni Moja Tu?

Dini ya Kweli Je, Ni Moja Tu?

Watu fulani huchukizwa na swali hilo. Kwa kuwa kuna dini nyingi ulimwenguni, wao hufikiri kwamba yeyote anayedai kwamba yeye tu ndiye aliye na ukweli lazima awe na akili finyu au hata kiburi. Wao huona kwamba inapatana na akili kufikiri kuna jambo fulani zuri katika dini zote au nyingi kati ya hizo. Je, una maoni kama hayo?

BILA shaka, kuna pindi ambapo lingekuwa jambo la busara kuwa na maoni mbalimbali. Kwa mfano, mtu anaweza kuamini vyakula fulani vinaweza kumfanya awe na afya bora. Lakini je, anapaswa kuwalazimisha watu wale vyakula hivyo kana kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na afya nzuri? Kwa kweli, ungekuwa ni unyenyekevu na hekima kuona kwamba huenda vyakula ambavyo mtu mwingine anachagua ni vyenye afya zaidi angalau kwa mtu huyo.

Je, tunaweza kusema hivyo kuhusu dini? Je, kuna njia mbalimbali zinazokubalika ambazo mtu anaweza kuchagua ikitegemea malezi au jinsi mtu anavyoelewa mambo? Au je, kuna imani moja tu ya kweli ya kidini inayopaswa kufuatwa na wanadamu wote? Acheni tuchunguze maoni ya Biblia. Kwanza tutachunguza ikiwa watu wanaweza kupata kweli. Ikiwa haiwezi kupatikana, basi hakuna haja ya kutafuta dini moja ya kweli.

Je, Kweli ya Kidini Inaweza Kupatikana?

Muda mfupi kabla ya kuuawa, Yesu Kristo alimwambia hivi Gavana Mroma Pontio Pilato aliyekuwa akimhoji: “Kila mtu aliye upande wa ile kweli huisikiliza sauti yangu.” Huenda Pilato alikuwa na shaka alipomwuliza: “Kweli ni nini?” (Yohana 18:37, 38) Kwa upande mwingine, Yesu alisema kwa ujasiri kuhusu kweli. Hakuwa na shaka kwamba kuna kweli. Kwa mfano, fikiria mambo manne ambayo Yesu aliwaambia watu tofauti.

“Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.”Yohana 18:37.

“Mimi ndiye njia na kweli na uzima.”—Yohana 14:6.

“Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.”Yohana 4:23, 24.

“Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:31, 32.

Kwa kuwa Yesu alizungumza kwa uhakika kuhusu kweli na kwamba tunaweza kujifunza kweli, je, hatupaswi kuchunguza uwezekano wa kwamba kuna kweli ya kidini na kwamba inaweza kupatikana?

Je, Kuna Kweli?

Bila shaka utakubali kwamba kuna mambo fulani ambayo tunaweza kuwa na uhakika kwamba yapo. Una hakika kwamba wewe upo na kwamba vitu vinavyokuzunguka ni halisi. Miti, milima, mawingu, jua, na mwezi, yaani, ulimwengu halisi, si vitu vya kuwaziwa tu. Kwa kweli kuna watu wachache ambao wanaweza kujaribu kukusadikisha kwamba uhalisi wa vitu hivyo unatiliwa shaka. Lakini wewe hukubaliani na wazo hilo la ajabu, sivyo?

Pia kuna sheria za asili. Tuna hakika vilevile kwamba sheria hizo zipo. Kwa mfano, ukiruka kutoka kwenye jabali kubwa utaanguka; ukikataa kula utasikia njaa; na ukikosa kula kwa muda mrefu utakufa. Una hakika kwamba sheria hizo za asili haziwaathiri watu wachache tu na kutowaathiri wengine. Zinawaathiri wanadamu wote na hivyo zinatumika ulimwenguni pote.

Biblia inataja sheria moja inayotumika ulimwenguni pote inapouliza hivi: “Je, mtu anaweza kukusanya moto kifuani pake na mavazi yake yasiungue?” Kwa kweli maneno hayo yalipoandikwa, ilijulikana ulimwenguni pote kwamba nguo zinaweza kuteketea zikiguswa na moto. Hata hivyo, methali hiyo ya Biblia ilikuwa ikitaja jambo muhimu zaidi, yaani, “yule anayelala na mke wa mwenzake” atapata madhara makubwa.—Methali 6:27, 29.

Je, tunaweza kuwa na hakika kwamba maneno hayo ni kweli kabisa? Huenda watu fulani wakakataa. Wanaweza kudai kwamba viwango vya maadili hutofautiana kati ya watu, na kwamba vinategemea malezi, imani, na hali za mtu. Lakini fikiria sheria chache za Mungu kuhusu maadili zinazopatikana katika Biblia. Je, sheria hizo hazikubaliwi kuwa kweli ulimwenguni pote?

Biblia hushutumu uzinzi. (1 Wakorintho 6:9, 10) Watu fulani hawaoni fundisho hilo la Biblia kuwa kweli, na hivyo wao hufanya uzinzi. Hata hivyo, hata wao hupatwa na madhara machungu yanayotia ndani dhamiri mbaya, talaka, na majeraha ya kihisia yanayowaathiri wote wanaohusika.

Mungu pia anashutumu ulevi. (Methali 23:20; Waefeso 5:18) Ni nini hutukia watu wanapolewa? Katika visa vingi wao hupoteza kazi, afya yao huzorota, na familia zao huvunjika na kuumia kihisia. (Methali 23:29-35) Madhara hayo huwapata hata wale ambao hawaamini kwamba ulevi ni mbaya. Je, ukweli kuhusu viwango hivyo vya maadili vinategemea imani au jinsi mtu anavyoona mambo?

Pia kuna amri za Biblia ambazo zinatuchochea kufanya mema kama vile amri ya mume kumpenda mke wake, mke kumheshimu mume wake, na kuwafanyia wengine mema. (Mathayo 7:12; Waefeso 5:33) Kutii amri hizo huleta faida. Je, ungesema kwamba amri hizo zinawanufaisha watu fulani tu na haziwanufaishi wengine?

Iwe sheria za Biblia zinafuatwa au hazifuatwi matokeo huonekana. Jambo hilo linaonyesha kwamba sheria hizo si maoni mbalimbali ambayo mtu anachagua kufuata. Badala yake, sheria hizo ni kweli. Uthibitisho umeonyesha kwamba sheria za Biblia zinapofuatwa kunakuwa na matokeo mazuri, lakini zisipofuatwa kunakuwa na matokeo mabaya.

Hebu fikiria: Ikiwa viwango vya maadili vya Biblia ni vya kweli kwa wanadamu wote, vipi kuhusu viwango vya Neno la Mungu kuhusu ibada? Vipi kuhusu kile ambacho Biblia inasema juu ya hali ya wafu na tumaini letu la kuishi milele? Ni jambo linalopatana na akili kwamba mafundisho hayo ya Biblia ni kweli ambazo zimetolewa kwa ajili ya wanadamu wote. Faida na madhara hayawapati tu wale wanaoamini kweli hizo.

Inawezekana kupata kweli. Yesu alisema kwamba Neno la Mungu, Biblia ni kweli. (Yohana 17:17) Hata hivyo, huenda ikaonekana kwamba kweli haiwezi kupatikana. Kwa nini? Kwa sababu dini nyingi zinadai kufundisha yale ambayo Biblia inasema. Ni dini gani inayofundisha kweli ya Neno la Mungu? Je, ni dini moja tu? Je, kweli yote au sehemu yake inaweza kupatikana katika dini mbalimbali?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Madhara ya kukumbatia moto yanahusianaje na kutotii amri za Mungu?