Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Upatano Kati ya Ushirikina na Mafundisho ya Biblia?

Je, Kuna Upatano Kati ya Ushirikina na Mafundisho ya Biblia?

Maoni ya Biblia

Je, Kuna Upatano Kati ya Ushirikina na Mafundisho ya Biblia?

MWANDISHI mmoja wa habari alikataa kusafiri kwa ndege kwa mwaka mmoja kwa sababu mbashiri fulani alikuwa ametabiri kwamba atakufa katika aksidenti ya ndege. Watu wa aina zote kutia ndani wanasiasa, wafanyabiashara, waigizaji, wanamichezo, na wanafunzi wa vyuo vikuu, hutumia ushirikina. Wanapokuwa na shaka, mfadhaiko, au mahangaiko, wao huhisi kwamba mazoea hayo yanaweza kuwalinda na hatari au kuwasaidia watimize malengo yao.

Aina nyingi za ushirikina huonekana kuwa utamaduni wenye kupendeza au njia isiyo na madhara ya kujitegemeza kihisia. Margaret Mead, aliyekuwa mtaalamu wa tabia na utamaduni, alisema hivi: “Ushirikina huonyesha tamaa kali tuliyo nayo ya jambo fulani kutendeka tunavyotaka au kuzuia jambo baya lisitupate. Kufuata ushirikina ingawa hatuamini nguvu zake hutusaidia tupate tumaini bila kuwa watumwa wake.” Lakini wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanapaswa kujiuliza, ‘Je, kuna upatano kati ya ushirikina na Ukristo wa kweli?’

Chanzo cha Ushirikina

Kwa ujumla kuna mambo mengi ambayo wanadamu wanahofu, kama vile kifo, mambo yasiyojulikana, maisha baada ya kifo, na kadhalika. Shetani, mpinzani mwasi wa Mungu, ameazimia kuwafanya wanadamu wawe watumwa na amekuwa akieneza uwongo mbaya ili watu waendelee kuhofu. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Shetani hafanyi kazi peke yake kujaribu kuwaondoa watu kutoka kwa Mungu. Katika Biblia Shetani anaitwa “mtawala wa roho waovu.” (Mathayo 12:24-27) Roho waovu ni nani? Katika siku za Noa malaika fulani walijiunga na Shetani katika uasi wake dhidi ya Mungu na kujigeuza kuwa roho waovu. Tangu wakati huo wamekuwa wakijaribu kuathiri akili za watu. Ushirikina ni moja kati ya mbinu wanazotumia.—Mwanzo 6:1, 2; Luka 8:2, 30; Yuda 6.

Uwongo mmoja ambao Shetani ametumia kuweka msingi wa ushirikina ni imani ya kwamba kitu fulani kisichoweza kuonekana huendelea kuishi mwili wa mwanadamu unapokufa na kitu hicho kinaweza kurudi kuwaathiri watu. Lakini Biblia inasema: “Wafu, hawajui lolote kamwe.” Inaendelea kusema kwamba “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima” baada ya mtu kufa.—Mhubiri 9:5, 10.

“Chukizo kwa Yehova”

Watu wengi wameamua kuamini uwongo wa Shetani. Hata hivyo, miaka mingi iliyopita, Mungu aliwapa watu wake Waisraeli mwongozo wa wazi kuhusu jambo hilo. Neno lake linasema hivi: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Kwa kusikitisha, Waisraeli hawakutii onyo hilo nyakati zote. Kwa mfano, katika siku za nabii Isaya, watu fulani waliamini kwamba mavuno mazuri yalitegemea kumfurahisha “mungu wa Bahati Njema,” imani ya ushirikina ambayo iliwaletea matatizo. Walipoteza kibali na baraka za Yehova.—Isaya 65:11, 12.

Mtazamo wa Yehova kuelekea ushirikina haukubadilika Ukristo ulipoanzishwa. Mtume Paulo aliwasihi watu walioamini ushirikina katika jiji la Listra ‘wageuke kutoka kwa mambo hayo ya bure [“ushirikina,” The Emphatic Diaglott] wapate kumjia Mungu aliye hai, aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.’—Matendo 14:15.

Kuvunja Imani Katika Ushirikina

Kuna mazoea mengi ya ushirikina na hakuna yoyote yanayopatana na akili. Ushirikina unaweza kuwafanya watu waseme kwamba mambo mabaya yalitukia kwa sababu ya bahati mbaya badala ya kukubali makosa yao.

Kwa kupendeza, watu wengi wameacha kuamini ushirikina. Yesu alisema: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Clementina, aliyekuwa mbashiri kwa miaka 25 nchini Brazili, alisema: “Nilijipatia riziki kwa kubashiri. Lakini kweli ya Biblia iliniweka huru kutokana na ushirikina.” Kwa kweli, kujifunza Biblia kwa ukawaida na kusali kwa Yehova Mungu kutoka moyoni kunaweza kutusaidia kuwa na nguvu za ndani. Hilo linaweza kutufanya tufikiri kwa usawaziko, na hivyo kutusaidia kufanya maamuzi yanayopatana na akili na yanayoweza kuzuia matatizo na kupunguza mahangaiko.—Wafilipi 4:6, 7, 13.

Biblia inauliza hivi: “Nuru ina ushirika gani na giza? Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali [Shetani]?” Hivyo, Wakristo wa kweli lazima waepuke ushirikina.—2 Wakorintho 6:14-16.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Badala ya kumtegemea Mungu, Waisraeli katika siku za Isaya walimtegemea nani?—Isaya 65:11, 12.

▪ Mtume Paulo aliwahimiza watu huko Listra wafanye nini?—Matendo 14:15.

▪ Je, kuna upatano kati ya ushirikina na Ukristo wa kweli?—2 Wakorintho 6:14-16.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ushirikina unawafanya watu wahisi usalama usio wa kweli