Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuipata Dini ya Kweli

Jinsi ya Kuipata Dini ya Kweli

Jinsi ya Kuipata Dini ya Kweli

Watu fulani wanauliza: ‘Ikiwa kuna kweli kutoka kwa Mungu, kwa nini siwezi kuipata kwa urahisi? Ikiwa Mungu ana ujumbe muhimu kwa wanadamu wote, je, hangeuwasilisha kwa njia iliyo wazi ili watu wautambue mara moja pasipo kuhitaji kufanya uchunguzi?’

KWA kweli, Mungu ana uwezo wa kufanya jambo kama hilo. Lakini je, hiyo ndiyo njia aliyochagua ya kuwasilisha kweli?

Jinsi Mungu Anavyowasilisha Kweli

Mungu anapitisha ujumbe wake kwa njia inayowaruhusu watu wanyoofu wanaoitafuta kweli waipate. (Zaburi 14:2) Fikiria ujumbe ambao Mungu alimpa nabii wake Yeremia karne nyingi zilizopita. Ujumbe huo ulitolewa kwa watu wa Mungu walioasi kuhusu Wababiloni kuharibu Yerusalemu.—Yeremia 25:8-11; 52:12-14.

Hata hivyo, wakati huohuo manabii wengine walidai kwamba wana ujumbe kutoka kwa Mungu. Hanania alitabiri kwamba Yerusalemu lingekuwa na amani. Huo ulikuwa ujumbe tofauti sana na ule wa Yeremia. Kwa hiyo, watu wakati huo wangemwamini nani—Yeremia au wale waliompinga?—Yeremia 23:16, 17; 28:1, 2, 10-17.

Ili wajue ni nani aliyekuwa akisema kweli, Wayahudi wanyoofu walihitaji kumjua Yehova kibinafsi. Walihitaji kuelewa sheria na kanuni zake na pia jinsi anavyoona makosa. Kwa kufanya hivyo, wangekubaliana na maneno ya Mungu aliyosema kupitia Yeremia kwamba “hakuna mtu yeyote aliyekuwa akitubu ubaya wake.” (Yeremia 8:5-7) Isitoshe, wangetambua kwamba hali hiyo ya kusikitisha haingekuwa na matokeo mazuri kwa Yerusalemu na wakaaji wake.—Kumbukumbu la Torati 28:15-68; Yeremia 52:4-14.

Unabii wa Yeremia kuhusu Yerusalemu ulitimia. Jiji hilo liliteketezwa kabisa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K.

Ingawa matokeo ya kutotii yalitabiriwa zamani sana, jitihada ilihitajiwa ili kutambua wakati ulikuwa umewadia wa Mungu kuchukua hatua.

Kweli ya Kikristo

Namna gani kweli iliyotangazwa na Yesu Kristo? Je, kila mtu aliitambua kuwa ujumbe kutoka kwa Mungu? Hapana. Hata ingawa Yesu alikuwa miongoni mwa Waisraeli akiwafundisha na kufanya miujiza, wasikilizaji wengi hawakutambua kwamba yeye ni Masihi aliyeahidiwa, yaani, Kristo au Mtiwa-mafuta.

Yesu aliwaambia hivi Mafarisayo waliouliza Ufalme wa Mungu ungekuja lini: “Ufalme wa Mungu hautakuja kwa wonyesho wenye kutokeza sana.” Kisha akasema: “Ufalme wa Mungu umo katikati yenu.” (Luka 17:20, 21) Yesu, Mtawala aliyewekwa rasmi na Mungu alikuwa katikati yao! Lakini Mafarisayo hao walikataa kuona uthibitisho wa kwamba alikuwa akitimiza unabii kuhusu Masihi na kumkubali kuwa “Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mathayo 16:16.

Wanafunzi wa Kristo wa karne ya kwanza walipata itikio hilohilo. Ingawa miujiza ilionyesha kwamba Mungu alikuwa akiwategemeza wanafunzi hao, kweli haikuwa wazi kwa watu wote. (Matendo 8:1-8; 9:32-41) Yesu aliwaagiza wanafunzi wake ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu’ kwa kuwafundisha. Waliposikiliza na kujifunza kweli za Maandiko, watu wanyoofu waliotafuta kweli wakawa waamini.—Mathayo 28:19; Matendo 5:42; 17:2-4, 32-34.

Ndivyo ilivyo leo. ‘Habari njema ya ufalme inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14) Hilo halifanywi kwa “wonyesho wa kutokeza sana,” yaani, kwa njia iliyo wazi sana hivi kwamba kila mtu duniani ataitambua kuwa ujumbe kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, kweli ya Mungu inatambuliwa na inawavutia watu wenye mioyo minyoofu ambao wanataka kumwabudu Mungu kwa njia anayotaka.—Yohana 10:4, 27.

Kusoma gazeti linalozungumzia Biblia kunaonyesha kwamba huenda ukawa unatafuta kweli. Utajuaje ni dini gani inayofundisha kweli?

Njia Bora ya Kupata Kweli

Katika karne ya kwanza, wakaaji wa Beroya walipongezwa na mtume Paulo kwa sababu ya jinsi walivyoitikia mafundisho yake. Hata ingawa hawakukubali mara moja kile ambacho Paulo alisema kuwa kweli, walimsikiliza kwa heshima. Tunaweza kujifunza jambo fulani tukichunguza kile ambacho Waberoya walifanya baada ya kusikia ujumbe huo.

Biblia inaeleza hivi: “Sasa [Waberoya] walikuwa wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo. Kwa hiyo wengi kati yao wakawa waamini.” (Matendo 17:10-12) Kwa hiyo, hawakutafuta kijuujuu tu. Hawakutarajia kupata kweli kwa kujadiliana kwa muda mfupi mara moja au mbili na Paulo.

Ona kwamba Waberoya “walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili.” Hilo linatuonyesha mtazamo waliokuwa nao walipojifunza Maandiko. Hawakukubali kila kitu bila kuuliza wala hawakukataa kila kitu bila kufikiri. Hawakuchambua yale ambayo waliambiwa na Paulo, ambaye alikuwa mwakilishi wa Mungu.

Fikiria hili pia: Ilikuwa mara ya kwanza kwa Waberoya kusikia kuhusu Ukristo. Mambo waliyoambiwa yalisikika kuwa mazuri, lakini huenda haikuwa rahisi kuamini kwamba ni ya kweli. Badala ya kuyapuuza, walichunguza Maandiko kwa uangalifu ‘ili kuona kama mambo waliyoambiwa na Paulo ndivyo yalivyo.’ Ona pia kwamba watu katika Beroya na Thesalonike waliotafuta kweli kwa bidii walikuwa waamini. (Matendo 17:4, 12) Hawakukata tamaa na kusema kwamba kweli haiwezi kupatikana. Waliitambua dini ya kweli.

Jinsi Kweli Inavyowachochea Watu

Kama Waberoya, mtu anapopata kweli anakuwa na hamu ya kuwaambia wengine. Huenda watu wengine wakapinga wakisema ni unyenyekevu kufikiri kwamba dini nyingine pia zinaweza kuwa na kweli. Hata hivyo, mtu akipata kweli ya Biblia hana shaka yoyote. Hajiulizi ikiwa kweli inaweza kupatikana au ikiwa dini zote zinaongoza kwenye wokovu. Hata hivyo, ili mtu apate kweli anahitaji kufanya uchunguzi kwa uangalifu, na hilo linahitaji unyenyekevu.

Mashahidi wa Yehova wamefanya uchunguzi huo na hiyo ndiyo sababu wanaamini kwamba wamepata dini ya kweli. Wanakualika uchunguze Maandiko ili utambue ni nani wanaofuata dini ya kweli leo. Ingawa orodha ya mambo yanayotambulisha dini ya kweli haitoshi, sanduku kwenye ukurasa huu linalozungumza kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza linaweza kukusaidia.

Ukikubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova bila malipo unaweza kuchunguza kwa kina yale ambayo Biblia inafundisha hasa. Kujifunza mambo hayo kutakusaidia kuitambua dini ya kweli.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Mambo Yanayoitambulisha Dini ya Kweli

Chunguza mazoea na mafundisho ya Wakristo wa karne ya kwanza:

Walitegemea mwongozo wa Neno la Mungu.—2 Timotheo 3:16; 2 Petro 1:21.

Walifundisha kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu na alikuwa tofauti kabisa na Mungu na alijitiisha Kwake.—1 Wakorintho 11:3; 1 Petro 1:3.

Walifundisha kwamba wafu watafufuliwa na kuishi tena.—Matendo 24:15.

Walijulikana kwa kuwa na upendo kati yao.—Yohana 13:34, 35.

Hawakuabudu wakiwa mtu mmojammoja bali walipangwa katika makutaniko na walikuwa na umoja chini ya waangalizi na baraza kuu la wazee waliojitiisha chini ya Yesu akiwa Kichwa.—Matendo 14:21-23; 15:1-31; Waefeso 1:22; 1 Timotheo 3:1-13.

Walihubiri kwa bidii kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee kwa wanadamu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 1:8.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wangejuaje kwamba Yeremia alikuwa nabii wa kweli, ilhali watu wengine walimpinga?

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Waberoya wa karne ya kwanza walimsikiliza Paulo kisha wakayachunguza Maandiko ili kuhakikisha kwamba mambo aliyosema yalikuwa kweli

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kujifunza Biblia kwa uangalifu kutakusaidia kutambua dini ya kweli