Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhubiri Habari Njema Katika Nchi za Mbali

Kuhubiri Habari Njema Katika Nchi za Mbali

Kuhubiri Habari Njema Katika Nchi za Mbali

Limesimuliwa na Helen Jones

Nilikuwa nikitembea kwenye soko lililosongamana watu huko Bangalore, India, mapema katika miaka ya 1970. Ghafula, nyati akaninyanyua juu kwa pembe zake na kunitupa chini. Nyati huyo alipokuwa karibu kunikanyaga, mwanamke mmoja Mhindu alikuja na kuniokoa. Nilikuwa nikifanya nini India?

NILIZALIWA mwaka wa 1931 na kulelewa katika jiji maridadi la Vancouver, Kanada. Wazazi wangu walifuata maadili ingawa hawakwenda kanisani. Hata hivyo, nilitamani sana kumjua Mungu, kwa hiyo nilipokuwa kijana, nilihudhuria mafundisho ya kidini ya watoto yanayofanywa siku ya Jumapili (Siku ya Yenga) na pia madarasa ya kujifunza Biblia wakati wa kiangazi.

Mnamo 1950, nikiwa na umri wa miaka 19, niliolewa na Frank Schiller, ambaye alikuwa na watoto wanne aliowapata wakati wa ndoa yake ya kwanza. Miaka miwili baadaye, tulipata mtoto wa kiume. Tulitaka kuwa wafuasi wa dini fulani; lakini kwa kuwa Frank alikuwa ametalikiana na mke wake wa kwanza, hakuna dini iliyotukubali. Frank alichukizwa sana na jambo hilo hivi kwamba hakutaka kuzungumza kuhusu dini.

Kujifunza Kweli ya Biblia

Mnamo 1954, kaka yangu alinieleza kwa msisimko yale aliyokuwa ameambiwa kuhusu Biblia na mfanyakazi mwenzake ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova. Ingawa nilikuwa na maswali mengi na nilijua mahali ambapo Mashahidi walikutania, sikuhudhuria mikutano yao kwa sababu nilijua Frank alichukizwa na dini. Baada ya muda, Mashahidi wawili walinitembelea. Nilitaka kujua dini yao husema nini kuhusu talaka, nao wakanielekeza kwenye Biblia na kunionyesha msingi wa Kimaandiko wa talaka. (Mathayo 19:3-9) Walinihakikishia kwamba kwa kujifunza Biblia kwa kawaida, maswali yangu kuhusu Biblia yatajibiwa.

Frank alikasirika sana na akakataa kabisa kujihusisha na Mashahidi. Mnamo 1955, nilihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo, na niliporudi nyumbani, kwa msisimko nilimweleza Frank mambo niliyojifunza kutoka katika Biblia. Alinijibu hivi kwa sauti: “Siamini! Ikiwa unaweza kunithibitishia kutoka katika Biblia, basi nitaambatana nawe kwenye mikutano hiyo yenu!”

Nilimpa Biblia, naye akaishika kwa heshima sana. Tulifungua maandiko niliyokuwa nimeandika, na nikaacha Biblia yenyewe ijieleze. Frank hakubishana nami na jioni yote akawa na mawazo mengi.

Baada ya muda, nilimkumbusha kwamba aliahidi atahudhuria mkutano. Akionyesha hataki kwenda, alijibu hivi: “Nitakwenda mara hii moja tu kuona ni nini hufanyika huko.” Hotuba ya Biblia ilikuwa kuhusu wake kujitiisha kwa waume wao. (Waefeso 5:22, 23, 33) Habari hiyo ilimpendeza sana. Wakati huohuo, Frank alihudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi lenye kichwa, “Ridhika na Kazi.” Frank alipendezwa sana na habari hiyo kwa kuwa yeye ni mfanyakazi mwenye bidii. Baada ya funzo hilo, hakukosa mkutano wowote. Baada ya muda mfupi, Frank akawa mwenye bidii katika huduma, nami nikajifunza Biblia na watu waliofanya maendeleo na kubatizwa. Mimi, Frank, pamoja na mama na kaka yangu tulijiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa mwaka huohuo.

Tamaa ya Kufanya Mengi

Katika kusanyiko la wilaya lililofanywa Seattle, Washington, Marekani mnamo 1957, kulikuwa na hotuba kuhusu kutumika katika nchi zilizo na uhitaji mkubwa wa wahudumu wa Ufalme. Nilisali hivi: ‘Ee, Yehova, nataka kwenda pia. Tafadhali tusaidie twende eneo ambapo wahudumu wa Ufalme wanahitajika.’ Lakini Frank alihangaikia daraka lake la kutunza familia na kuitafutia chakula.—1 Timotheo 5:8.

Mwaka uliofuata, familia yetu ilihudhuria kusanyiko la wilaya huko New York City lililofanywa wakati uleule na makusanyiko yaliyofanywa Yankee Stadium na Polo Grounds. Zaidi ya watu 253,000 walisikiliza hotuba ya watu wote! Frank alichochewa sana na aliyoona na aliyosikia. Kwa hiyo, tuliporudi nyumbani, tulichagua kwenda Kenya, kwa kuwa watu huko walizungumza Kiingereza na pia kulikuwa na shule nzuri ambazo tungeweza kuwapeleka watoto wetu.

Mnamo 1959, tuliuza nyumba yetu, tukafunganya virago vyetu na kusafiri kwa gari hadi Montreal, Kanada. Kutoka hapo tulisafiri kwa meli hadi London, Uingereza, kisha tukapanda meli nyingine kutoka Uingereza kupitia Bahari ya Mediterania na Bahari Nyekundu na kuingia Bahari ya Hindi. Hatimaye tuliwasili Mombasa, Kenya, pwani iliyo mashariki ya Afrika. Siku iliyofuata tulisafiri kwa gari-moshi hadi Nairobi, mji mkuu wa Kenya.

Tunapata Baraka Nyingi Afrika

Wakati huo kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Kenya, kwa hiyo tulihubiri kwa uangalifu. Wenzi wa ndoa kadhaa kutoka nchi nyingine walikuwa wakiishi Kenya, nasi tuliruhusiwa kuishi humo. Tuliruhusiwa kukutana katika kikundi cha watu wasiozidi kumi. Kwa hiyo familia yetu, kutia ndani na watoto walishiriki kikamili katika mikutano.

Muda mfupi baada ya kuwasili Kenya, tulipata mahali pa kuishi na Frank akapata kazi. Mwanamke wa kwanza niliyemhubiria nyumba kwa nyumba alikubali kujifunza Biblia na mwishowe akawa painia, yaani, Shahidi wa Yehova anayetumia wakati wake wote kuhubiri. Pia nilijifunza Biblia na msichana Kalasinga tuliyemwita Goody. Alibaki akiwa imara licha ya kupingwa na familia yake na Wakalasinga wenzake. Alipofukuzwa nyumbani, Goody Lull alienda kuishi na familia moja ya Mashahidi, akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, akawa painia, na baadaye akahitimu kutoka shule ya wamishonari ya Gileadi.

Familia yetu ilikumbwa na matatizo. Kijana wetu mkubwa aliugua homa ya baridi-yabisi, naye Frank aliungua vibaya alipokuwa akitengeneza gari na akapoteza kazi yake. Baada ya muda, alipata kazi huko Dar es Salaam, mji mkuu wa Tanganyika (sasa ni Tanzania) uliokuwa kilomita 1,000 hivi kutoka Kenya. Kwa hiyo tulifunganya virago vyetu na kufunga safari ndefu kuelekea huko. Wakati huo kulikuwa na kutaniko ndogo huko Dar es Salaam, nao walitukaribisha.

Ingawa wakati huo kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku nchini Tanzania, marufuku hayo hayakutekelezwa sana. Mnamo 1963, Milton Henschel, mwakilishi kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Marekani alitutembelea. Alipokuwa akitoa hotuba katika Jumba la Karimjee, ambalo ndilo lililokuwa jumba maridadi nchini, mwanamume mmoja mzee aliyevalia kama maskini aliketi kando yangu. Nilimsalimu na nilimruhusu atumie Biblia na kitabu changu cha nyimbo. Programu ilipokwisha, nilimkaribisha aje tena. Alipoondoka, Mashahidi wa eneo hilo walinijia mara moja.

“Unajua huyo ni nani?” wakaniuliza. “Huyo ni meya wa Dar es Salaam!” Hapo awali alikuwa ametisha kusimamisha kusanyiko letu. Alivalia kama maskini ili iwapo ningemtendea vibaya, angetumia hilo kama kisingizio. Alivutiwa sana na jinsi tulivyomjali na kumwonyesha fadhili hivi kwamba aliruhusu kusanyiko hilo liendelee. Watu 274 walihudhuria na 16 wakabatizwa.

Tanzania ilipata uhuru tukiwa huko. Baada ya hayo, waajiri walipendelea kuwapa ajira wenyeji badala ya wageni. Ilibidi wageni wengi kuondoka nchini, lakini Frank alitafuta kazi kwa bidii na mwishowe alifanikiwa alipoambiwa kwamba kulikuwa na uhitaji wa mekanika mwenye ujuzi wa gari-moshi zilizotumia dizeli. Hilo lilituwezesha kuishi nchini humo kwa miaka mingine minne. Mkataba wa kazi wa Frank ulipomalizika, tulirudi Kanada, ambako tulikaa hadi mtoto wetu wa mwisho alipooa. Bado tulijihisi tuna nguvu na tulitaka kufanya mengi zaidi.

Tunahamia India

Mnamo 1970, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Bombay (sasa ni Mumbai), ilipendekeza kwamba tuhamie Bangalore, jiji lililokuwa na wakaaji milioni 1.6 wakati huo. Huko ndiko nyati alininyanyua kwa pembe zake. Wakati huo, kulikuwa na kutaniko la Kiingereza lenye wahubiri 40 na kikundi cha mbali cha Kitamili. Frank alijifunza Biblia na wanaume kadhaa ambao walifanya maendeleo na baadaye wakawa wazee Wakristo. Nilijifunza pia na familia kadhaa ambazo baadaye zilimtumikia Yehova.

Mwanamke mmoja anayeitwa Gloria aliishi katika sehemu maskini ya mji huo. Nilipomtembelea mara ya kwanza, alinikaribisha. Kwa kuwa nyumba yake haikuwa na fanicha, tuliketi sakafuni. Nilimwachia gazeti Mnara wa Mlinzi, naye akakata andiko la Ufunuo 4:11 lililonukuliwa katika gazeti hilo na kulibandika ukutani mahali ambapo angeliona kila siku. Lilitia ndani maneno: “Unastahili, Ee Yehova,” ambayo yalimpendeza sana mwanamke huyo. Mwaka mmoja baadaye alibatizwa.

Frank alialikwa kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Bombay kwa mwaka mmoja na asimamie ujenzi wa Jumba la kwanza la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova nchini India. Jumba hilo lilijengwa kwa kuongezea orofa moja kwa jengo la tawi ambalo lilikuwapo. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi zaidi kidogo tu ya 3,000 nchini India, na idadi isiyozidi 10 walifanya kazi katika ofisi ya tawi. Mnamo 1975, pesa zetu ziliisha na tukawaaga kwa huzuni marafiki wetu tuliowapenda sana.

Tunarudi Afrika

Miaka 10 ilipita na sasa Frank angeweza kulipwa malipo ya uzeeni. Kwa hiyo tulijitolea katika programu ya kimataifa ya ujenzi wa ofisi za tawi. Tulipokea barua iliyotuomba twende Igieduma, Nigeria, ambako ujenzi ulikuwa ukiendelea. Tulipokuwa Igieduma, Frank alijifunza Biblia na mwanamume fulani katika kijiji kilichokuwa karibu. Mwanamume huyo alifanya maendeleo na baadaye akawa mshiriki wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Nigeria.

Kisha tukaenda Zaire kusaidia kujenga ofisi ya tawi. Muda mfupi baada ya hapo, kazi ya kuhubiri ilipigwa marufuku na pasipoti zetu zikachukuliwa. Frank alipatwa na mshtuko wa moyo alipokuwa kazini lakini alipata nafuu wakati wa marufuku hayo. Baadaye, ilibidi wafanyakazi wote wa ujenzi waondoke, nasi tukatumwa nchi jirani ya Liberia. Tulipokuwa katika ofisi ya tawi ya Monrovia, Frank aliombwa arekebishe jenereta. Tulirudi tena Kanada mwaka wa 1986 viza yetu ilipoisha.

Mwishowe Tunaenda Ekuado

Muda mfupi baadaye, tulipata habari kwamba rafiki yetu, Andy Kidd, alikuwa amehamia Ekuado na alikuwa akifurahia sana kuhubiri huko. Andy ndiye aliyekuwa mzee peke yake katika kutaniko lao, na mara nyingi ilibidi ashughulikie sehemu nyingi za mkutano. Alitualika huko na tukatembelea ofisi ya tawi ya Ekuado mnamo 1988 na tukiwa huko, akina ndugu walitufanya tujihisi tukiwa nyumbani.

Tulipata nyumba nzuri; lakini tulilazimika kujifunza Kihispania, na Frank alikuwa na umri wa miaka 71. Katika kipindi cha miaka miwili iliyofuata, tuliweza kuwasaidia watu 12 wafikie ubatizo hata ingawa hatukujua Kihispania vizuri. Frank aliombwa asaidie na ujenzi wa ofisi ya tawi ya Ekuado. Pia alijifunza Biblia na mume wa mmoja wa Mashahidi wa kwanza huko Guayaquil. Mume huyo, ambaye alikuwa amempinga mke wake kwa miaka 46, akawa rafiki na ndugu yetu wa kiroho.

Pigo Kubwa

Tuliishi karibu na mji mdogo wa Ancón, kando ya Bahari ya Pasifiki, ambako tulisaidia kujenga Jumba jipya la Ufalme. Kwa kuhuzunisha, baada ya kutoa hotuba ya mwisho katika Mkutano wa Utumishi, Frank alipatwa na mshtuko wa moyo na akafa usiku wa Novemba 4, 1998 (4/11/1998). Ndugu na dada wa kiroho walinifariji sana! Siku iliyofuata, Frank alizikwa katika makaburi yaliyokuwa kando ya Jumba la Ufalme. Sina maneno ya kueleza uchungu wa kumpoteza mpendwa katika kifo.

Kwa mara nyingine tena, ilibidi nirudi Kanada, wakati huu nikiwa peke yangu ili kushugulikia mambo ya familia na kisheria. Licha ya majonzi, Yehova hakunisahau. Nilipata barua kutoka ofisi ya tawi ya Ekuado iliyosema kwamba bado ninakaribishwa nchini humo. Kwa hiyo nilirudi na kukodi nyumba ndogo karibu na ofisi ya tawi. Kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi na pia kuhubiri kulinisaidia nikabiliane na uchungu wa kumpoteza Frank, lakini bado nilijihisi mpweke sana.

Kuendelea na Kazi

Baada ya muda, nilifahamiana na Junior Jones. Alikuja Ekuado kutoka Marekani mwaka wa 1997 ili kupainia. Tulikuwa na miradi na mapendezi yaleyale. Tulifunga ndoa Oktoba (Mwezi wa 10) 2000. Junior alikuwa na ujuzi wa kujenga kwa hiyo tulialikwa kusaidia kumaliza Jumba la Kusanyiko huko Cuenca, jiji lililokuwa juu kwenye Milima ya Andes. Kisha Aprili 30, 2006 (30/4/2006), Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, huko New York alitoa hotuba ya kuwekwa wakfu, na watu 6,554 walihudhuria.

Ni nani angeweza kuwazia kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme ingeweza kuwa na matokeo sana katika sehemu za mbali kama vile Afrika, India, na Amerika Kusini? Mimi na Junior hatufikirii kustaafu. Miaka zaidi ya 50 ambayo nimemtumikia Yehova imepita haraka hivi kwamba ni kana kwamba nilianza tu kumtumikia jana. Ninajua kwamba ulimwengu mpya utakapokuja, wakati huu tunamoishi utaonekana ni kana kwamba umepita haraka sana.—Ufunuo 21:3-5; 22:20.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 15]

 

Maeneo Tulikotumika

KANADA → UINGEREZA → KENYA → TANZANIA

KANADA → INDIA

KANADA → NIGERIA → JAM. YA KIDEMO. YA KONGO (ZAIRE) → LIBERIA

KANADA → EKUADO

 

MAREKANI

[Picha]

Nikiwa na Frank huko India, tukienda kusanyiko

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na mume wangu Junior Jones