Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Anayepaswa Kuamua Dini ya Kweli?

Ni Nani Anayepaswa Kuamua Dini ya Kweli?

Ni Nani Anayepaswa Kuamua Dini ya Kweli?

YESU alionyesha wazi kwamba si dini zote zinazokubaliwa na Mungu. Alizungumza kuhusu “manabii wa uwongo,” akiwalinganisha na mti unaozaa matunda yasiyofaa ambao “hukatwa na kutupwa ndani ya moto.” Pia alisema: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 7:15-22.

Kwa kweli, Yesu alisema hivi kuhusu watu fulani ambao wangedai kumfuata: “Nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mathayo 7:23) Isitoshe, akizungumza na viongozi wa kidini wa siku zake, Yesu alitumia maneno yaleyale ambayo Mungu aliwaambia Waisraeli waasi-imani. Alisema hivi kuwahusu: “Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.”—Marko 7:6, 7.

Ni wazi kwamba Mungu au Mwana wake hawakubali ibada ya aina zote. Hivyo, si dini zote za kweli. Je, hilo linamaanisha kwamba ni dini moja tu inayofundisha kweli? Je, haiwezekani kwamba Mungu anatumia dini kadhaa na kukataa nyingine? Au je, inawezekana kwamba Mungu anakubali au kukataa ibada ya mtu mmoja-mmoja walio katika dini mbalimbali licha ya yale ambayo dini zao hufundisha?

Mtume Paulo aliandika hivi akiongozwa na roho ya Mungu: “Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.” (1 Wakorintho 1:10) Biblia pia inawahimiza Wakristo wawe na ‘akili ileile na wawe na upendo uleule, waunganishwe pamoja katika nafsi, wakishika wazo moja akilini.’—Wafilipi 2:2.

Bila shaka, kunapokuwa na umoja kama huo, kunakuwa na dini moja. Kupatana na hilo, Biblia inasema kwamba kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.”—Waefeso 4:4, 5.

Biblia Inafunua Nini?

Biblia inaunga mkono wazo hilo. Kwa kuichunguza Biblia utaona kwamba Mungu alishughulika na watu wake kupitia mfumo mmoja wa ibada. Mapema katika historia ya wanadamu, Mungu alitumia wazee wa ukoo kuwa wawakilishi wake. Wazee fulani maarufu kati yao ni Noa, Abramu (Abrahamu), Isaka, na Yakobo.—Mwanzo 8:18-20; 12:1-3; 26:1-4; 28:10-15.

Wazao wa Yakobo walikuwa watumwa nchini Misri. Wakiwa huko, ingawa walikandamizwa waliongezeka na kuwa mamilioni. Mungu aliwakomboa kutoka utumwani na kuwapitisha kimuujiza katika Bahari Nyekundu. Kisha akawafanya wawe watu wake, na akawapa sheria kupitia mpatanishi ambaye ni Musa. Hivyo wakawa taifa la kale la Israeli, taifa la Mungu.—Kutoka 14:21-28; 19:1-6; 20:1-17.

Mungu hakukubali ibada ya mataifa yaliyozunguka Israeli. Kwa kweli, aliwaadhibu watu wake walipoacha sheria zake na kufuata ibada ya mataifa hayo.—Mambo ya Walawi 18:21-30; Kumbukumbu la Torati 18:9-12.

Namna gani watu mmojammoja kutoka mataifa mengine waliotaka kumwabudu Mungu wa kweli? Walihitaji kwanza kuacha ibada yao ya uwongo na kisha kujiunga na Waisraeli katika kumwabudu Yehova Mungu. Wengi wao walipata kibali cha Mungu na kuwa watumishi wake washikamanifu. Watu hao walitia ndani wanawake kama Rahabu Mkanaani na Ruthu Mmoabu; na wanaume kama vile Uria Mhiti na Ebed-meleki Mwethiopia; na vikundi vya watu kama vile Wagibeoni. Mfalme Sulemani wa Israeli alisali kutoka moyoni kwa niaba ya watu wote waliojiunga katika ibada ya kweli pamoja na watu wa Mungu. *2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33.

Baada ya Yesu Kuja Duniani

Baadaye Yesu alipokuja duniani, ibada ya kweli ilianzishwa kwa kutegemea mafundisho yake, na kusudi la Mungu lilifafanuliwa kwa njia kubwa. Baada ya muda, waabudu wa kweli waliitwa “Wakristo.” (Matendo 11:26) Hivyo, Wayahudi waliotaka kibali cha Mungu walihitaji kuacha ibada yao ya zamani. Hawakupaswa kuchagua mifumo miwili ya ibada au kuabudu wakiwa mtu mmojammoja. Kama vile tumeona katika Neno la Mungu, waabudu wa kweli waliunganishwa katika “imani moja.”—Waefeso 4:4, 5.

Leo huenda wazo la kwamba Mungu anashughulika na wanadamu kupitia dini moja tu halivutii watu fulani. Hata hivyo, hivyo ndivyo Biblia inakata maneno. Nyakati za zamani, watu wengi walioabudu kwa njia zao wenyewe walitambua ukweli huo. Walijiunga na waabudu wa kweli wa Yehova, na ingawa mwanzoni walikuwa na mashaka, yote yaligeuzwa yakawa baraka nyingi na furaha. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba baada ya mwanamume Mwethiopia kukubali Ukristo na kubatizwa “aliendelea kwenda zake akishangilia.”—Matendo 8:39.

Mtu yeyote leo anayekubali na kufuata dini ya kweli atapata baraka kama hizo. Lakini kwa sababu kuna dini nyingi sana, unaweza kuitambuaje dini ya kweli?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Unaweza kusoma kuhusu watu hao katika masimulizi ya Biblia yafuatayo: Yoshua 2:1-7; 6:22-25; Ruthu 1:4, 14-17; 2 Samweli 11:3-11; Yeremia 38:7-13; na Yoshua 9:3-9, 16-21.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ni nini kitakachoipata dini inayozaa matunda yasiyofaa?