Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniamini?

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniamini?

Vijana Huuliza

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniamini?

“Laiti wazazi wangu wangeniruhusu niende matembezi bila kuchungwa. Si eti ninataka kujihusisha katika mambo mabaya. Ningependa tu kufanya mambo fulani kama vile kwenda kumtembelea shangazi bila mama yangu kuwa na wasiwasi eti nina nia ya kuondoka nyumbani.”—Sarah, 18. *

“Kila mara mimi huwauliza wazazi wangu kwa nini hawaniamini ninapotaka kwenda matembezi na rafiki zangu. Mara nyingi wao huniambia: ‘Tunakuamini. Lakini hatuwaamini rafiki zako.’ Mimi huudhika wanaposema hivyo!”—Christine, 18.

KUAMINIWA kunafanana sana na pesa. Si rahisi kuzipata, kuzipoteza ni rahisi, na haidhuru unapewa kiasi gani, ni kana kwamba hazitoshi kamwe. Iliana mwenye umri wa miaka 16 anasema hivi: “Wakati wowote ninapotaka kwenda kutembea, wazazi wangu huniuliza maswali mengi sana kuhusu ninakoenda, nitakuwa na nani, tutafanya nini, na nitarudi saa ngapi. Ninajua kwamba wao ni wazazi wangu, lakini mimi huudhika wanaponiuliza maswali hayo!”

Je, nyakati nyingine wewe huhisi kwamba wazazi wako wanapaswa kukuamini zaidi? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini? Kwanza, acheni tuchunguze kwa nini mara nyingi suala la wazazi kuwaamini watoto hutokeza matatizo.

Matatizo ya Kukua

Biblia inasema kwamba “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Bila shaka, mwanamke atafanya vivyo hivyo. Iwe wewe ni mvulana au msichana, kusudi kuu la kipindi cha kubalehe ni kukutayarisha kwa ajili ya kuwa mtu mzima, wakati ambapo utakuwa tayari kuondoka nyumbani na hata kuwa na familia yako mwenyewe.

Hata hivyo, kuwa mtu mzima si kama mlango ambao unaingia tu unapofikia umri fulani. Ni kama ngazi unazopanda hatua kwa hatua katika kipindi cha kubalehe. Huenda wewe na wazazi wako mkawa na maoni tofauti kuhusu mahali ambapo umefikia katika kupanda ngazi hizo. “Nina umri wa miaka 20 na bado hilo ni tatizo,” anasema Maria ambaye anahisi kwamba wazazi wake hawaamini kwamba anaweza kuchagua marafiki wazuri. “Wazazi wangu wanafikiri kwamba siwezi kuondoka hali mbaya inapotokea. Nimejaribu kuwaambia kwamba tayari nimejiondoa katika hali nyingi mbaya, lakini bado hawajalegeza msimamo wao!”

Kama maneno ya Maria yanavyoonyesha, kutoaminiwa kunaweza kutokeza matatizo makubwa kati ya vijana na wazazi wao. Je, mambo yako hivyo katika familia yenu? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili wazazi wakuamini zaidi? Ikiwa wameacha kukuamini kwa sababu ya jambo fulani lisilo la hekima ulilofanya, unaweza kufanya nini ili kurekebisha hali?

Thibitisha Unaweza Kuaminika

Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo katika karne ya kwanza: “Endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Ni kweli kwamba hakuwa akizungumza hasa na vijana. Lakini kanuni hiyo inaweza kutumika. Mara nyingi mtu huaminiwa kulingana na jinsi anavyojithibitisha kuwa mwenye kuaminika. Si kwamba lazima uwe mkamilifu. Kila mtu hukosea. (Mhubiri 7:20) Hata hivyo, je, tabia yako kwa ujumla inawafanya wazazi wako wasikuamini?

Kwa mfano, mtume Paulo aliandika: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Jiulize, ‘Nimejiwekea rekodi ya aina gani inapohusu kuwaambia wazazi wangu ukweli kuhusu mahali nilipo na mambo ninayofanya?’ Fikiria maelezo kuhusu jambo hilo kutoka kwa vijana fulani ambao wamejichunguza kwa uangalifu.

Lori: “Kwa siri nilikuwa nikimtumia barua-pepe kijana fulani niliyempenda. Wazazi wangu waligundua na kuniambia niache. Niliahidi nitaacha, lakini sikuacha. Niliendelea kufanya hivyo kwa mwaka mzima. Ningemtumia barua-pepe, kisha wazazi wangu wangegundua nami ningeomba msamaha na kuwaahidi kwamba nitaacha, lakini bado ningeendelea. Ilifikia hatua ambapo wazazi wangu hawangeweza kuniamini tena!”

Unafikiri ni kwa nini wazazi wa Lori waliacha kumwamini, na Lori angetendaje wazazi wake walipozungumza naye mara ya kwanza? Andika jibu lako hapa.

․․․․․

Beverly: “Wazazi wangu hawakuamini kwamba ningetenda kwa njia inayofaa kuelekea wavulana, lakini sasa ninaelewa kwa nini walifanya hivyo. Tulikuwa tukichezeana kimapenzi na wavulana kadhaa waliokuwa na umri wa miaka miwili zaidi yangu. Nilikuwa nikizungumza nao kwa muda mrefu kwenye simu, na katika vikusanyiko mbalimbali ningezungumza nao peke yao. Wazazi wangu walininyang’anya simu kwa mwezi mmoja, na hawakuniruhusu niende mahali vijana hao wangekuwa.”

Unafikiri ni kwa nini wazazi wa Beverly waliacha kumwamini kwa muda fulani, naye angefanya nini ili kurekebisha mambo?

․․․․․

Annette: “Nilipokuwa shuleni, mimi na rafiki yangu tulienda nyumbani tukiwa na pombe kutoka kwenye karamu, ingawa tulijua kwamba wazazi wetu hawangekubali, nasi tukaamua kuinywa baadaye ili kujifurahisha tu. Mama ya rafiki yangu alipata chupa ya pombe yake. Ikafichuliwa kwamba hata mimi nilikuwa na moja. Jambo lililonihuzunisha zaidi ni kuona mama yangu akinitazama akiwa amehuzunika!”

Ikiwa Annette angekuwa dada yako mdogo, ungempa mashauri gani ili aaminiwe tena na mama yako?

․․․․․

Kuaminiwa Tena

Vipi ikiwa, kama vijana waliotajwa, umefanya mambo ambayo yamechangia wazazi wako waache kukuamini? Hata ikiwa mambo yamekuwa hivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kuyabadili. Jinsi gani?

Inaelekea kwamba wazazi wako watakuamini zaidi ukiwa na rekodi ya tabia ya kutegemeka. Kwa mfano: Mfikirie mtu anayedaiwa pesa na benki. Akilipa kwa ukawaida, ataaminiwa na benki na hata anaweza kupewa mkopo baadaye. Mambo yako hivyo pia nyumbani. Ukithibitika kuwa mwaminifu, hata katika mambo madogo, wazazi wako watakuamini zaidi wakati ujao.

Annette alijifunza jambo hilo. Alisema: “Unapokuwa mchanga, hutambui sana umuhimu wa kuaminiwa. Sasa ninahisi kwamba nina daraka na nimechochewa kutenda kwa njia itakayowafanya wazazi wangu waendelee kuniamini.” Tunajifunza nini? Badala ya kulalamika kwamba wazazi wako hawakuamini, kazia fikira kujenga rekodi ya tabia ya kutegemeka.

Kwa mfano, je, unategemeka katika mambo yaliyoorodheshwa hapa chini? Tia alama katika sanduku kando ya mambo unayohitaji kufanyia kazi.

□ Kufika nyumbani wakati niliowekewa na wazazi

□ Kufanya mambo kwa wakati

□ Kumaliza kazi

□ Kudumisha chumba changu kikiwa safi

□ Kutumia simu

□ Kutimiza ahadi zangu

□ Kutumia pesa kwa hekima

□ Kuamka bila kubembelezwa

□ Kusema kweli

□ Kukubali makosa na kuomba msamaha

□ Mambo mengine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Mbona usiazimie kuwa mwaminifu katika mambo uliyotia alama? Fuata mahimizo haya yanayopatikana katika Biblia: ‘Ondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wako wa kwanza.’ (Waefeso 4:22) ‘Acha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo.’ (Yakobo 5:12) “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) “Watiini wazazi wenu katika kila jambo.” (Wakolosai 3:20) Baada ya muda, maendeleo yako yatakuwa wazi kwa watu wengine, kutia ndani wazazi wako.—1 Timotheo 4:15.

Lakini vipi ukihisi kwamba licha ya jitihada zako, wazazi wako hawakuamini kama unavyostahili? Mbona usizungumze nao kuhusu jambo hilo? Badala ya kulalamika kwamba wao wanahitaji kukuamini zaidi, waulize kwa heshima wanataka wewe ufanye nini ili wakuamini. Waeleze waziwazi unakusudia kufanya nini ili wakuamini zaidi.

Usiwatazamie wazazi wako wakuondolee vizuizi mara moja. Bila shaka, wangependa kuhakikisha kwamba utatimiza ahadi zako. Tumia nafasi hii kujithibitisha kuwa unaaminika. Baada ya muda, wazazi wako watakuamini zaidi. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Beverly aliyetajwa awali. “Inachukua muda mrefu kumwamini mtu, lakini ni rahisi kuacha kumwamini,” akasema huku akiongezea hivi, “nimeanza kuaminiwa sasa, na ninahisi vizuri!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini wazazi wako wanaweza kusita kukuamini katika mambo mengi zaidi hata unapojitahidi sana kuwa mwaminifu?

▪ Kwa nini kuwasiliana na wazazi wako ni muhimu ikiwa unataka wakuamini zaidi?

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Kazia fikira kujenga rekodi ya tabia ya kutegemeka

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 28]

Kuwa mtu mzima anayeaminiwa ni kama ngazi unazopanda hatua kwa hatua katika kipindi cha kubalehe

[Mchoro]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

UTU UZIMA

KUBALEHE

UTOTO