Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku za Mwisho—Ni Nini Kitakachofuata?

Siku za Mwisho—Ni Nini Kitakachofuata?

Siku za Mwisho—Ni Nini Kitakachofuata?

WATU fulani wanaogopeshwa sana na “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Wao hufikiria tu kwamba zitakuwa nyakati za hatari. Hivyo, kwa nini kwa miaka mingi watu wengi wametazamia siku hizo kwa hamu? Kwa sababu siku za mwisho pia huonyesha kwamba nyakati nzuri zitafuata.

Kwa mfano, Sir Isaac Newton alisadiki kwamba wakati wa mwisho ungetokeza amani na ufanisi ulimwenguni pote chini ya Utawala wa Miaka Elfu wa Ufalme wa Mungu. Alisema kwamba unabii wa Mika 4:3 na Isaya 2:4 ungetimizwa wakati huo: “Watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”

Yesu alipozungumza kuhusu wakati wa mwisho, aliwahimiza wanafunzi wake wawe na mtazamo unaofaa. Baada ya kuwaambia kuhusu hali ngumu, mahangaiko, na woga ambao ungekuwapo wakati wa ile dhiki kuu, alisema: “Mambo haya yanapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” (Luka 21:28) Kukombolewa kutokana na nini?

Ahadi za Mungu

Vita, mizozo ya kijamii, uhalifu, jeuri, na njaa ni baadhi tu ya mambo yanayokumba wanadamu leo na kuwafanya waishi kwa woga. Je, umeathiriwa na mojawapo ya mambo hayo? Basi ona yale ambayo Mungu anaahidi:

“Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

“Watu wangu watakaa katika makao yenye amani na katika makao ya uhakika kamili na katika mahali pa kupumzika pasipo na usumbufu.”—Isaya 32:18.

“[Yehova] anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—Zaburi 46:9.

“Nao wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.”—Mika 4:4.

“Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”—Zaburi 72:16.

“Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.

Hata ikiwa tunaishi katika eneo ambako hali za maisha si mbaya sana, sote tunajua kwamba tutakuwa wagonjwa na tutakufa. Hayo pia hayatakuwapo katika ulimwengu mpya wa Mungu. Pia tunaweza kutazamia kwa hamu kuwaona tena wapendwa wetu waliokufa. Ona mambo yafuatayo:

“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.

“[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

“Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.

“Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

Mtume Petro alijumlisha mambo hayo yote alipoandika hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Ili kuwe na uadilifu duniani pote, mtu yeyote anayeweza kuharibu hali hiyo anapaswa kuondolewa. Pia ingekuwa lazima kuyaondoa mataifa yaliyopo leo ambayo husababisha mizozo na umwagaji wa damu kwa kutafuta mapendezi yao wenyewe kwa ubinafsi. Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utachukua mahali pa serikali zote za kidunia. Kuhusu utawala huo, tunahakikishiwa hivi: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo. Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.”—Isaya 9:7.

Unaweza kuishi chini ya hali hizo kwani Biblia inatuhakikishia hivi: “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Usikawie. Jipatie ujuzi utakaokuletea uzima wa milele. (Yohana 17:3) Anza kwa kuwasiliana na wachapishaji wa gazeti hili na kuomba funzo la Biblia la nyumbani bila malipo.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Unaweza kutazamia kuishi milele kwa amani ukiwa na afya kamilifu katika Paradiso itakayokuwa hapa duniani