Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku za Mwisho—Zitakuwa Lini?

Siku za Mwisho—Zitakuwa Lini?

Siku za Mwisho—Zitakuwa Lini?

“TUNATAZAMIA kwamba baada ya miaka bilioni moja hivi, dunia itakuwa jangwa kavu, lililonyauka, na lisiloweza kuzaa. Ni vigumu kuwazia jinsi viumbe wenye chembe nyingi watakavyoendelea kuishi,” lasema toleo la karibuni la gazeti Sky & Telescope. Kwa nini? “Jua linalozidi kuwa jangavu litachemsha bahari na kuunguza mabara,” lasema gazeti Astronomy, na kuongeza hivi: “Uharibifu huo mkubwa si jambo linalohangaisha tu, ni jambo tusiloweza kuepuka.”

Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Bila shaka, Muumba wa dunia anaweza pia kuidumisha. Kwa kweli, “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Lakini hakutaka ikaliwe na watu waovu, wanadamu wanaokufa. Mungu aliweka wakati ambapo angerudisha utawala wake kupitia Ufalme unaotajwa katika Danieli 2:44.

Yesu alihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Alizungumza kuhusu wakati wa kuyahukumu mataifa na watu. Alionya kuhusu dhiki ambayo ingekuwa kubwa kuliko dhiki nyingine yoyote iliyowahi kutukia. Naye alitoa ishara yenye mambo mengi ili kuonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu wetu ulikuwa umekaribia.—Mathayo 9:35; Marko 13:19; Luka 21:7-11; Yohana 12:31.

Uhakika wa kwamba mtu muhimu sana kama Yesu alizungumzia matukio hayo umechochea fikira za watu wengi. Mambo hayo yangetukia lini? Watu fulani wamejaribu kujua wakati hususa wa mwisho huo kwa kuchunguza unabii na tarehe za matukio. Mmoja wao ni Sir Isaac Newton, mtaalamu wa hesabu wa karne ya 17, ambaye aligundua nguvu za uvutano na pia mbuni wa mashine ya hesabu inayoitwa kalkulasi.

Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Si juu yenu kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Matendo 1:7) Na alipokuwa akitoa “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:3, 36) Kisha baada ya kulinganisha uharibifu wa ulimwengu wa wanadamu waovu wakati wa Noa na uharibifu ambao utatukia wakati wa “kuwapo kwa Mwana wa binadamu,” Yesu alisema: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—Mathayo 24:39, 42.

Hivyo, ingawa hatujafunuliwa wakati hususa wa mwisho wa ‘mfumo huu wa mambo,’ ile “ishara” ambayo Yesu alitoa ingetusaidia kujua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Huo ungekuwa wakati wa ‘kuendelea kukesha ili tupate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.’—Luka 21:36.

Kabla ya kuwapa ishara yenyewe, Yesu alionya hivi: “Jihadharini msipotoshwe; kwa maana wengi watakuja kwa msingi wa jina langu, wakisema, ‘Mimi ndiye,’ na, ‘Wakati unaofaa umekaribia.’ Msiwafuate. Zaidi ya hayo, wakati mnaposikia juu ya vita na machafuko, msiogope. Kwa maana mambo hayo lazima yatukie kwanza, lakini ule mwisho hautatokea mara moja.”—Luka 21:8, 9.

Ni Nini Ile Ishara?

Akitueleza kile ambacho kingeonyesha kwamba siku za mwisho zimefika, Yesu aliongezea hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi, na katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni na upungufu wa chakula; kutakuwa na mambo yenye kuogopesha na ishara kubwa kutoka mbinguni.” (Luka 21:10, 11) Yesu alisema hivi pia: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Matukio ambayo Yesu alitaja, yaani, vita, matetemeko ya nchi, tauni, upungufu wa chakula, hayangekuwa mambo mapya. Yamekuwa yakitukia tangu mapema katika historia ya wanadamu. Tofauti ingekuwa kwamba yangetukia katika kipindi kimoja cha wakati.

Jiulize, ‘Ni wakati gani ambapo matukio yote yanayotajwa katika Injili yametukia katika kipindi kimoja cha wakati?’ Tangu 1914, wanadamu wameshuhudia vita vibaya vya ulimwengu; matetemeko makubwa ya nchi ambayo yamekuwa na matokeo mabaya sana, kama vile tsunami; magonjwa yanayoenea sana kama malaria, mafua, na UKIMWI; mamilioni wakifa kwa sababu ya upungufu wa chakula; watu ulimwenguni pote kuogopa kwa sababu ya mashambulizi ya kigaidi na matumizi ya silaha za maangamizi makubwa; na kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa kimbingu wa Mungu. Mambo hayo yametukia tu kama vile Yesu alivyotabiri.

Pia kumbuka yale ambayo mtume Paulo aliandika: “Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.” (2 Timotheo 3:1-5) Naam, “nyakati za hatari” ambazo zingetiwa alama na kuenea kwa uasi-sheria, ukosefu wa ujitoaji-kimungu, ukatili, na ubinafsi ulimwenguni pote. *

Lakini je, inawezekana kwamba “siku za mwisho” ambazo zingeutangulia ule mwisho wenyewe bado hazijafika? Je, kuna uthibitisho mwingine unaoonyesha siku hizo zingeanza lini?

“Wakati wa Mwisho” Ungeanza Lini?

Baada ya kupokea habari kuhusu mambo ambayo yangetendeka muda mrefu baadaye, nabii Danieli aliambiwa hivi: “Mikaeli [Yesu Kristo] atasimama wakati huo, [“wakati wa mwisho” unaotajwa katika Danieli 11:40] yule mkuu anayesimama kwa ajili ya wana wa watu wako.” (Danieli 12:1) Mikaeli atakaposimama atafanya nini?

Kitabu cha Ufunuo kinazungumzia wakati ambapo Mikaeli angetenda akiwa Mfalme. Kinasema hivi: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye. Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:7-9, 12.

Kronolojia ya Biblia inaonyesha kwamba vita hivyo vya kumwondoa Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni vingeleta ole mkubwa duniani kwa sababu Ibilisi ana hasira akijua kwamba wakati wake uliobaki wa kuitawala dunia ni mfupi. Hasira yake ingeongezeka katika siku za mwisho mpaka atakaposhindwa kabisa katika vita vya Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16; 19:11, 15; 20:1-3.

Baada ya kutaja matokeo ya vita hivyo vya kimbingu, mtume Yohana alitangaza: “Nami nikaisikia sauti kubwa mbinguni ikisema: ‘Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake, kwa sababu mshtaki wa ndugu zetu ametupwa chini, anayewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu!’” (Ufunuo 12:10) Je, umeona kwamba mstari huo unatangaza kusimamishwa kwa Ufalme chini ya Kristo? Kwa kweli, Ufalme huo wa kimbingu ulisimamishwa mwaka wa 1914. * Hata hivyo, kama Zaburi 110:2 inavyoonyesha, Yesu angetawala “katikati ya adui [zake]” mpaka wakati ambapo Ufalme ungetawala dunia yote kama unavyotawala mbinguni.—Mathayo 6:10.

Kwa kupendeza, malaika ambaye alimweleza nabii Danieli kuhusu mambo ambayo yangetukia, alisema hivi: “Wewe, Ee Danieli, yafanye siri maneno hayo na kukifunga kitabu kwa muhuri, mpaka wakati wa mwisho. Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” (Danieli 12:4) Hilo linatoa uthibitisho zaidi kwamba sasa tunaishi katika “wakati wa mwisho.” Ujuzi kuhusu maana ya unabii huo mbalimbali umefunuliwa wazi na sasa unatangazwa ulimwenguni pote. *

“Siku za Mwisho” Zitakwisha Lini?

Biblia haisemi siku za mwisho zitakuwa na urefu gani. Lakini katika siku za mwisho, hali duniani zitazidi kuwa mbaya kadiri wakati wa Shetani unavyozidi kupungua. Mtume Paulo alionya kwamba “watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:13) Akizungumzia mambo ambayo yangetukia, Yesu alisema hivi: “Siku hizo zitakuwa siku za dhiki ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa uumbaji ambao Mungu aliumba mpaka wakati huo, na haitatukia tena. Kwa kweli, kama Yehova hangezifupisha siku hizo, hakuna chochote chenye mwili ambacho kingeokolewa. Lakini amezifupisha siku hizo kwa sababu ya waliochaguliwa ambao amewachagua.”—Marko 13:19, 20.

Baadhi ya mambo ambayo yatatukia ni “dhiki kuu,” inayotia ndani vita vya Har–Magedoni, na kuzuiliwa kwa Shetani na roho wake waovu ili wasiwe na uvutano juu ya dunia. (Mathayo 24:21) “Mungu, asiyeweza kusema uwongo,” ametuhakikishia kwamba mambo hayo yatatukia. (Tito 1:2) Mungu ndiye atakayeleta Har–Magedoni na kumfanya Shetani atupwe ndani ya abiso.

Mtume Paulo aliongozwa na roho kutujulisha yale ambayo yangetangulia uharibifu utakaoletwa na Mungu. Kwa habari ya “nyakati na majira,” aliandika hivi: “Siku ya Yehova inakuja sawasawa kabisa kama mwizi usiku. Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja kama vile maumivu ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataponyoka hata kidogo.” (1 Wathesalonike 5:1-3) Biblia haitaji ni nini hasa kitakachosababisha tangazo la uwongo la “amani na usalama,” hilo litajulikana baadaye; lakini tangazo hilo halitazuia kuja kwa siku ya Yehova ya hukumu. *

Ikiwa tunasadiki uhakika wa unabii huo mbalimbali, ujuzi kuhusu matukio hayo unapaswa kutuchochea kutenda. Kwa njia gani? Petro anajibu: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Petro 3:11, 12) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Hilo linaninufaishaje?’ Makala inayofuata itajibu swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kwa habari zaidi kuhusu “siku za mwisho,” tafadhali soma Amkeni! la Aprili (Mwezi wa 4) 2007, ukurasa 8-10, na Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2006 (15/9/2006), ukurasa 4-7, na Oktoba 1, 2005, (1/10/2005) ukurasa 4-7, yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Kwa habari zaidi kuhusu kronolojia ya Biblia, ona ukurasa wa 215-218 katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 19 Ona kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! na Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2008, ukurasa wa 31-39, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 23 Ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! (chapa ya 2006), ukurasa wa 250-251, fungu la 13 na 14.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Yesu alisema kwanba Mungu tu ndiye anayejua “siku ile na saa ile”

[Picha katika ukurasa wa 4]

Sir Isaac Newton

[Hisani]

© A. H. C./age fotostock

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ishara ambayo Yesu alitoa imekuwa ikionekana tangu 1914

[Hisani]

© Heidi Bradner/Panos Pictures

© Paul Smith/Panos Pictures