Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ufadhili Ndilo Suluhisho?

Je, Ufadhili Ndilo Suluhisho?

Je, Ufadhili Ndilo Suluhisho?

INGAWA misiba ya asili, umaskini, njaa, magonjwa, na hatari ya kuharibiwa kwa mazingira huzungumziwa sana katika vyombo vya habari, kuna jambo la kupendeza ambalo limeonekana, yaani, ukarimu. Nyakati nyingine kuna habari kuhusu matajiri wanaoyapa mashirika ya kutoa misaada mamia ya mamilioni, au hata mabilioni ya dola. Mara nyingi, watu mashuhuri wanatumia umashuhuri wao kuwahamasisha watu kuhusu matatizo makubwa. Hata watu wengi wasio matajiri wanatoa pesa kwa ajili ya makusudi mbalimbali. Lakini, msaada wa kifedha unaweza kusaidia kwa kadiri gani hasa tunapofikiria wakati ujao?

Enzi Bora ya Ufadhili

Katika nchi fulani, watu wengi zaidi na zaidi wana mwelekeo wa ufadhili. Kitabu kimoja kilisema hivi: “Mwanzoni mwa karne ya 21, kuna mashirika mengi zaidi [ya ufadhili] yaliyo na mali nyingi katika nchi nyingi zaidi kuliko wakati mwingine wowote.” Kadiri watu wengi zaidi wanavyozidi kuwa matajiri, mwelekeo wa ufadhili unatarajiwa kuendelea. Si tu kwamba watu wengi watakuwa na pesa zaidi za kutoa, bali pia matajiri wanapokufa na kuwaachia wengine mali zao, inatazamiwa kwamba mashirika mbalimbali yatakuwa na mali nyingi. Kwa sababu nzuri, jarida la habari la Uingereza The Economist lilisema kwamba huenda huu ukawa mwanzo wa “enzi bora ya ufadhili.”

Sababu moja inayochangia hali hiyo ni kushindwa kwa serikali kutatua matatizo yanayokabili ulimwengu. Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya UKIMWI barani Afrika alisema kwamba “ukosefu wa mwongozo wa kisiasa” ni sababu moja inayowafanya watu wengi mashuhuri wajihusishe na masuala ya afya ulimwenguni. Iwe tatizo linahusu umaskini, afya, mazingira, elimu, au haki katika jamii, matajiri hasa “wanazidi kukosa subira na kushindwa kwa serikali na juhudi za kimataifa kutatua au kupunguza matatizo hayo,” anasema Joel Fleishman katika kitabu chake The Foundation: A Great American Secret—How Private Wealth Is Changing the World. Wakiwa na hamu kubwa ya kubadili mambo, wafadhili fulani matajiri hujaribu kutumia mbinu zilizowafanya wafanikiwe katika biashara.

Nguvu za Ufadhili

Mwanzoni mwa karne ya 20 kulikuwa pia na pindi nyingine iliyoitwa eti enzi bora ya ufadhili. Wafanyabiashara wenye mafanikio kama vile Andrew Carnegie na John D. Rockefeller, Sr., waliamua kutumia mali zao kuwasaidia walio na uhitaji. Wafadhili kama hao waliona kwamba, huku yakiwalisha watu waliokuwa wakifa njaa au kuwatunza watoto wagonjwa, mashirika ya kawaida ya kutoa ufadhili hayakushughulikia kiini cha matatizo. Wakiona uhitaji wa njia mwafaka zaidi za kuandaa msaada, walianzisha taasisi na mashirika ambayo yangechochea mabadiliko ya kijamii na kufadhili miradi ya utafiti iliyokusudiwa kutatua vyanzo vyenyewe vya matatizo. Tangu miaka hiyo ya mapema, makumi ya maelfu ya mashirika hayo yameanzishwa ulimwenguni pote, na zaidi ya mashirika 50 kati ya hayo yana mali yenye thamani inayozidi dola bilioni moja.

Hatuwezi kukanusha kwamba mashirika hayo yamekuwa na matokeo mazuri. Idadi kubwa ya shule, maktaba, hospitali, bustani, na majumba ya ukumbusho ambayo yamejengwa inathibitisha jambo hilo. Hali kadhalika, miradi ya kuongeza mazao na chakula imewezesha kuwaandalia watu wengi chakula katika nchi zilizokumbwa na umaskini. Pesa za kufanya utafiti wa kitiba zimechangia kuboresha huduma za afya na, katika visa fulani, kumaliza magonjwa fulani kama vile homa ya manjano.

Leo, wakati ambapo jitihada za kutatua matatizo zimezidishwa na kukiwa na pesa nyingi kuliko awali, watu wengi wanaona kwamba kutakuwa na mafanikio. Mnamo 2006, rais wa zamani wa Marekani alikiambia hivi kikundi cha wafadhili: “Jitihada za wafadhili zitawanufaisha sana watu kwa ujumla.”

Hata hivyo, wengi wana mashaka. Laurie Garrett, mtaalamu wa huduma za afya ulimwenguni, aliandika hivi: “Mtu anaweza kufikiri kwamba kukiwa na pesa hizo zote, kufikia sasa suluhisho la matatizo ya kitiba ulimwenguni lingekuwa limepatikana. Lakini mtu angekuwa amekosea.” Kwa nini? Anatoa sababu kama vile utaratibu wenye kugharimu sana, ufisadi, ukosefu wa mipango, na mwelekeo wa wafadhili wa kutaja kihususa matatizo ya kiafya—kwa mfano, UKIMWI—ambayo wanataka pesa zao zitumiwe kuyashughulikia.

Kwa sababu hakuna mipango mizuri na pesa “zinatumiwa hasa kwa ajili ya magonjwa makubwa—badala ya huduma za afya kwa ujumla,” Garrett anahisi kwamba “kuna hatari kubwa kwamba enzi hii ya ufadhili haitashindwa tu kutimiza malengo lake, bali pia itafanya mambo yawe mabaya hata zaidi.”

Kwa Nini Pesa Tu Hazitoshi

Haidhuru watu wana nia gani, sikuzote ufadhili hautakuwa na mafanikio kamili. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba pesa au elimu ya kutosha haiwezi kumaliza matatizo kama vile pupa, chuki, ubaguzi, uzalendo, ukabila, na imani za dini za uwongo. Ijapokuwa mambo hayo yanawaongezea wanadamu taabu, hayo siyo kiini cha matatizo. Kama Biblia inavyoonyesha, masuala makubwa zaidi yanahusika.

Sababu moja ni kutokamilika kunakotokana na dhambi. (Waroma 3:23; 5:12) Hali yetu ya kutokamilika inatufanya tuwe na mwelekeo wa kufikiri na kutenda mabaya. Mwanzo 8:21 inasema hivi: “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” Mamilioni ya watu hujihusisha katika ukosefu wa maadili katika ngono na kutumia dawa za kulevya kwa sababu ya mwelekeo huo wa kutenda mabaya. Hivyo, matendo hayo husababisha magonjwa mbalimbali yaenee, kutia ndani UKIMWI.—Waroma 1:26, 27.

Sababu ya pili inayowafanya wanadamu wateseke ni kwamba hatuna uwezo wa kujitawala wenyewe kwa mafanikio. “Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake,” inasema Yeremia 10:23. “Ukosefu wa mwongozo wa kisiasa,” uliotajwa mapema, ni sababu moja kwa nini mashirika mengi ya ufadhili hayahusishi serikali. Biblia inaeleza kwamba wanadamu walipaswa kumtegemea Muumba kuwa Mtawala wao, wala si kutegemea wanadamu wenzao.—Isaya 33:22.

Isitoshe, Biblia inaahidi kwamba Muumba, Yehova Mungu, atashughulikia matatizo yote yanayowasumbua wanadamu. Kwa kweli, tayari amechukua hatua kubwa za kufanya hivyo.

Mfadhili Mkuu Zaidi

Neno “mfadhili” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kuwapenda wanadamu.” Hakuna anayewapenda wanadamu zaidi ya Muumba wetu. Yohana 3:16 inasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Naam, Yehova alitoa kitu chenye thamani zaidi ya pesa ili kuwakomboa wanadamu kutokana na utumwa wa dhambi na kifo. Alimtoa Mwana wake mpendwa kuwa “fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Mtume Petro aliandika hivi kuhusu Yesu: “Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tuachane kabisa na dhambi na kuishi kwa uadilifu. Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’”—1 Petro 2:24.

Pia Yehova amefanya mipango ya kushughulikia tatizo la utawala. Ili kutatua tatizo hilo amesimamisha serikali ya ulimwengu inayoitwa Ufalme wa Mungu. Ukitawala kutoka mbinguni, Ufalme huo utaondoa waovu wote na kuleta amani na umoja kwenye Sayari yetu Dunia.—Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; 7:13, 14.

Kwa kushughulikia kiini cha matatizo yanayowafanya wanadamu wateseke, Mungu atatimiza yale ambayo wanadamu hawawezi kutimiza, wakiwa mtu mmoja-mmoja au kikundi. Kwa sababu hiyo, badala ya kuanzisha mashirika ya ufadhili, Mashahidi wa Yehova wanamwiga Yesu Kristo kwa kutumia wakati na mali zao kutangaza “habari njema ya ufalme [wa Mungu].”—Mathayo 24:14; Luka 4:43.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

“Mungu Humpenda Mtoaji Mchangamfu”

Maneno hayo yanayopatikana katika Biblia kwenye 2 Wakorintho 9:7, ndiyo kanuni inayowaongoza Mashahidi wa Yehova. Wanapotumia wakati, nguvu, na mali zao kuwafaidi wengine, wanajitahidi kufuata himizo hili: “Tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”—1 Yohana 3:18.

Kunapokuwa na uhitaji, kama vile msiba wa asili unapotokea, Mashahidi huona kuwa ni pendeleo kuwasaidia walioathiriwa. Kwa mfano, Vimbunga Katrina, Rita, na Wilma vilipokumba maeneo ya kusini ya Marekani, maelfu ya Mashahidi waliojitolea walifurika katika maeneo yaliyoathiriwa ili kusaidia kazi ya kutoa msaada na kujenga upya. Chini ya usimamizi wa halmashauri za kutoa misaada za maeneo hayo, wajitoleaji hao walirekebisha na kujenga upya zaidi ya nyumba 5,600 za Mashahidi wa Yehova na Majumba ya Ufalme 90. Walisaidia kujenga karibu kila kitu kilichokuwa kimeharibiwa.

Mashahidi wa Yehova hawatoi fungu la kumi wala hawaombi-ombi pesa. Kazi yao inategemezwa kabisa na michango ya hiari.—Mathayo 6:3, 4; 2 Wakorintho 8:12.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Pesa haziwezi kumaliza kiini cha matatizo yanayowafanya wanadamu wawe wagonjwa na kuteseka

[Hisani]

©Chris de Bode/Panos Pictures