Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wengi Hawana Tumaini

Kwa Nini Wengi Hawana Tumaini

Kwa Nini Wengi Hawana Tumaini

Mambo yanayotendeka ulimwenguni pote yanafanya watu waogope wakati ujao. Majiji mengi sasa yana kamera za kuwachunguza raia. Kwa sababu ya kuogopa ugaidi, viwanja vingi vya ndege vyenye shughuli nyingi vimekaribia kufanana na kambi za kijeshi. Idadi inayozidi kuongezeka ya wezi na watu wanaowatendea watoto vibaya kingono hutumia Intaneti kuvizia watu wasiojua makusudio yao mabaya. Matatizo ya kimazingira kama vile uchafuzi, ukataji miti, kutoweka kwa viumbe, na kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni kunatishia uhai katika sayari yetu.

INGAWA matatizo hayo hayangewaziwa makumi ya miaka iliyopita, leo yanawahangaisha watu ulimwenguni pote. Kwa sababu nzuri, watu wengi hujiuliza ulimwengu huu unapatwa na nini na maisha yao na ya watoto wao yatakuwaje wakati ujao. Je, utafika wakati ambapo watu wataogopa kupanda basi, gari-moshi, au ndege? Bei ya vitu ikizidi kupanda na mali-asili zikizidi kutumiwa vibaya, je, vizazi vijavyo vitapata matibabu bora, chakula kizuri, na vyanzo vya nishati vya kutosha?

“Wakati ujao unatisha kwelikweli,” alisema waziri wa afya wa Kanada alipozungumza kuhusu gharama za matibabu zinazozidi kuongezeka. Pia, watu wana wasiwasi mwingi kuhusu vyakula na vyanzo vya nishati. Kwa nini? Ili kupunguza matumizi ya mafuta yanayochimbuliwa ardhini, nchi fulani zinatumia pesa nyingi ili kutokeza mafuta kutokana na vyanzo vingine, kama vile ethanoli, inayotokana na mimea. Hivyo, kwa mara ya kwanza katika historia, ardhi haipaswi tu kuwaandalia wanadamu chakula bali pia kutokeza mafuta kwa ajili ya magari. Tayari watu wanakabili tatizo la kuongezeka kwa bei ya chakula.

Wakati huohuo, pengo kati ya matajiri na maskini linazidi kuongezeka na kuzidisha mizozo ya kijamii. “Katika miaka kumi ya kwanza katika karne hii ya 21, maendeleo makubwa katika hali njema ya binadamu na vilevile hali mbaya sana ya umaskini,” inasema ripoti ya Shirika la Afya Ulimwenguni. “Katika baadhi ya nchi maskini sana, watu wanaishi umepungua nusu ya miaka ambayo watu katika nchi tajiri sana wanaishi.” Hali hiyo inasababishwa hasa na magonjwa na msukosuko wa kijamii na kiuchumi katika nchi zenye serikali zisizo imara.

Zaidi ya hayo, unapofikiria tisho la kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni kunakoweza kusababisha kuenea kwa majangwa na hali mbaya sana ya hewa, si ajabu kwamba watu wengi wanaochunguza hali ya ulimwengu wana wasiwasi kuhusu wakati ujao. Gazeti Bulletin of the Atomic Scientists, ambalo linarekebisha Saa ya Maangamizi, lilizungumzia hofu ya wakati ujao mbaya “huku wanasayansi wakiendelea kuchunguza jinsi [kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni] kunavyoathiri mifumo ya ikolojia ya Dunia.”

Je, wakati wetu ujao ni mbaya kadiri hiyo? Je, tumaini letu pekee la wakati ujao mzuri linategemea viongozi wa kibiashara, kisiasa, kidini, na kisayansi? Watu fulani wanauliza, ‘Tuna tumaini gani lingine? Tulijiletea matatizo hayo sisi wenyewe; nasi tunapaswa kuyasuluhisha.’ Wengine wanahisi kwamba wanadamu hawawezi kusuluhisha matatizo hayo na ni Mungu tu anayeweza kutuletea wakati ujao salama. Ikiwa ndivyo ilivyo, tuna uhakika gani kwamba Mungu anatujali na atatuzuia tusijiangamize wenyewe? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Je, tumaini letu pekee la wakati ujao mzuri linategemea viongozi wa kibiashara, kisiasa, kidini, na kisayansi?