Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Muziki—Zawadi Ambayo Mungu Ameupa Moyo

Muziki—Zawadi Ambayo Mungu Ameupa Moyo

Muziki—Zawadi Ambayo Mungu Ameupa Moyo

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

MUZIKI una nguvu. Unaweza kutuliwaza, kutusisimua, na kuchochea hisia zetu. Unaweza kuonyesha shangwe na huzuni yetu. Karibu katika tamaduni zote—za kale na za leo—muziki hugusa akili na moyo. Naam, kwa kweli muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Mwanzo 4:21.

Tangu tulipozaliwa, inaelekea tumekuwa tukisikia muziki fulani. Huenda mama yetu alituimbia wimbo ili kutubembeleza tulale. Tulipokuwa vijana, huenda tulianza kupendezwa na muziki uliosisimua moyo wetu. Hata tukiwa watu wazima, wengi wetu tunapenda kusikiliza muziki unaotutuliza tunapoendesha gari au tunapokuwa nyumbani mwishoni mwa siku yenye shughuli nyingi.

Maneno ya wimbo fulani huenda yakatia ndani mambo kuhusu utamaduni au historia ya nchi. Waisraeli wa kale waliadhimisha pindi fulani za pekee kwa nyimbo. (Kutoka 15:1-21; Waamuzi 5:1-31) Nabii Musa alitunga wimbo ambao ulitia ndani historia na mahimizo mazito kwa ajili ya watu. (Kumbukumbu la Torati 32:1-43) Hapana shaka kwamba nyimbo kama hizo zilikuwa njia nzuri ya kujikumbusha mambo.

Unaweza Kuimba!

Huenda ukasema, ‘Siwezi kuimba vizuri.’ Hata hivyo, fikiria kidogo kuhusu sauti yako. Kwa sababu ya ala hiyo yenye matumizi mengi, kwa kadiri fulani karibu kila mtu anaweza kuimba, iwe ana ala nyingine au la. Unachohitaji tu kufanya ni kufungua kinywa chako na kuimba. Na unapoimba, usihangaikie sana ikiwa utashinda tuzo fulani au kupigiwa makofi kwa sababu ya sauti yako. Ukifanya mazoezi, utaiboresha.

“Sauti inahusiana sana na chanzo cha hisia zetu za ndani, nayo ndiyo ala bora zaidi ya kuonyesha hisia hizo,” lasema gazeti Psychologies la Hispania. “[Kuimba] kunasisimua,” anasema Ainhoa Arteta, mwimbaji wa soprano. “Ningependekeza yeyote anayetaka kufunua hisia zake kwa kuimba afanye hivyo kwa uhuru na kwa hiari.”

Kwa sababu muziki unaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya moyo, tunapaswa kuwa wateuzi. Kwa mfano, mdundo mtamu unaweza kufunika maneno machafu ambayo yanapunguza uzito au hata kuchochea chuki, ukosefu wa maadili, au jeuri—mambo yasiyoweza kumvutia hata kidogo mtu yeyote anayependa mema. (Waefeso 4:17-19; 5:3, 4) “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa,” lasema Neno la Mungu, “kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Ndiyo, kuteua muziki ni suala zito sana. *

Muziki Mzuri Unaweza Kuwa Dawa Nzuri

“Mojawapo ya sababu zinazofanya muziki upatikane katika karibu tamaduni zote [ni] uwezo wake wa kutokeza na kudumisha afya na hali njema ya wanadamu,” chasema kitabu Principles and Practice of Stress Management. Tunapoimba, chasema kitabu kingine, mwili wetu wote unajaa sauti na kutikisika. Na kutikisika huko taratibu kunafanya tishu za mwili zitulie na kupanuka, na hilo linaweza kupunguza maumivu.

Kwa sababu hiyo, madaktari fulani wamewatia moyo wagonjwa walio na mfadhaiko wasikilize muziki unaotuliza, ambao pia unaweza kumchangamsha mtu. Katika hospitali fulani, muziki huchezwa hata katika chumba cha wagonjwa mahututi. Mara nyingi, watoto wanaozaliwa kabla ya wakati na pia wagonjwa waliofanyiwa upasuaji wanaitikia muziki unaopendeza. Kulingana na kitabu Principles and Practice of Stress Management, uchunguzi unadokeza kwamba kusikiliza muziki unaotuliza “unapunguza sana homoni zinazoleta mfadhaiko wakati wa upasuaji.”

Pia, muziki unaweza kuwafanya wanawake waja-wazito wasiwe na wasiwasi mwingi kwa kuwafanya watulie wanapokuwa na utungu na wanapozaa. Nyakati nyingine madaktari wa meno huwachezea wagonjwa walio na wasiwasi muziki wenye kutuliza ili watulie. Lakini muziki na nyimbo zinaweza kuwa na matokeo makubwa zaidi. Zinaweza kutusaidia katika njia ya kiroho.

‘Nitamsifu Mungu kwa Wimbo’

Je, ulijua kwamba asilimia kumi ya Biblia ni nyimbo? Mifano iliyo wazi zaidi ni Zaburi, Wimbo wa Sulemani, na Maombolezo. Kwa kufaa, asilimia kubwa ya marejeo mia tatu hivi ya nyimbo yanahusiana na ibada ya Mungu. “Yehova ni nguvu zangu . . . , nami nitamsifu kwa wimbo wangu,” akaandika Mfalme Daudi Mwisraeli, ambaye alikuwa na kipawa cha kuimba na kutunga muziki.—Zaburi 28:7.

Kwa kweli, Daudi alipanga wanaume 4,000 wa kabila la Lawi watumike kama wanamuziki na waimbaji huko Yerusalemu. Wanaume 288 kati yao ‘walizoezwa nyimbo kwa Yehova, wote wakiwa wajuzi.’ (1 Mambo ya Nyakati 23:4, 5; 25:7) Hapana shaka kwamba waimbaji hao walifanya mazoezi kwa bidii. Kwa kweli, muziki ulikuwa muhimu sana katika kumwabudu Mungu hivi kwamba waimbaji hawakupewa wajibu mwingine wowote ili wakazie fikira uimbaji.—1 Mambo ya Nyakati 9:33.

Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu pamoja na mitume wake walimwimbia Mungu sifa, na inaelekea waliimba Zaburi 113 mpaka 118. Kufikia wakati wa Yesu, zaburi hizo—zilizoitwa “Zaburi za Haleli”—ziliimbwa wakati wa sikukuu ya Pasaka. (Mathayo 26:26-30) Maneno “Zaburi za Haleli” yanarejelea kule kurudiwa kwa neno “Haleluya!” linalomaanisha “Msifu Yah!” “Yah” ni ufupisho wa kishairi wa jina Yehova, jina la Mungu Aliye Juu Zaidi.—Zaburi 83:18.

Pia uimbaji ulikuja kuwa sehemu ya ibada ya Kikristo. Kitabu The History of Music kinasema: “Wakristo wa mapema walikuwa na zoea la kuimba mbele ya watu na pia katika ibada ya faraghani. Wayahudi wageuzwa imani waliendeleza desturi ya masinagogi . . . Mbali na Zaburi za Kiebrania . . . , Wakristo waliendelea kutokeza nyimbo mpya.” Hata leo, Mashahidi Wakristo wa Yehova wanafurahia kumwimbia Yehova sifa, faraghani na pia kwenye mikutano yao ya Kikristo.

Kwa sababu muziki hutusaidia kufunua karibu kila hisia na kwa sababu unaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya moyo, akili, na mwili wetu, tunapaswa kuheshimu sana hiyo ‘tuzo kamilifu kutoka juu.’ (Yakobo 1:17) Naam, na tuitumie kwa kadiri tuwezavyo na kwa hekima.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Mbali na kukataa nyimbo zinazotukuza chuki, ukosefu wa maadili, na jeuri, wale wanaompenda Mungu na wanadamu wenzao wanakataa pia kusikiliza muziki unaounga mkono ibada ya sanamu, uzalendo, na uwongo wa kidini.—Isaya 2:4; 2 Wakorintho 6:14-18; 1 Yohana 5:21.