Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ujao Salama Chini ya Utawala wa Mungu

Wakati Ujao Salama Chini ya Utawala wa Mungu

Wakati Ujao Salama Chini ya Utawala wa Mungu

HIVI karibuni hatutahitaji kuhangaikia wakati ujao kwa kuwa Mungu atachukua mamlaka juu ya sayari yetu Dunia kwa kusimamisha serikali yake, inayoitwa Ufalme wa Mungu. Yesu Kristo alikuwa na taraja hilo zuri akilini alipowafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Ufalme wa Mungu hautashirikiana na viongozi wa kisiasa wala kuwatumia kutawala. Badala yake, utaondoa kila sehemu ya utawala wa kibinadamu, kama inavyoonyeshwa katika unabii ufuatao wa Danieli kuhusu “siku za mwisho,” kipindi ambacho tunaishi sasa. (2 Timotheo 3:1) “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za wanadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Maneno hayo hayawafariji au kuwapa tumaini watu wanaopendelea utawala wa wanadamu, lakini kwa wote wanaotamani kuwa chini ya enzi kuu ya Mungu kupitia Ufalme wake, maneno hayo yanatoa ahadi nzuri ajabu.

Wakati Ujao Mzuri!

Ufalme wa Mungu utakapotawala juu ya dunia yote, raia wake hawatagawanywa na siasa, jamii, dini, au mipaka ya kitaifa. Badala yake, watakuwa undugu wa ulimwenguni pote uliounganishwa na kweli ya kiroho na upendo wa kweli. (Yohana 13:34, 35; 17:3, 17) Naam, chini ya utawala wa Ufalme, “mwadilifu atachipuka,” na kutakuwa na “wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.”—Zaburi 72:7.

Mbali na mambo hayo, Ufalme wa Mungu utawainua wanadamu wanaojitiisha wafikie ukamilifu wa akili na mwili, utaondoa magonjwa yote, mateso, na kifo. (Ufunuo 21:3, 4) Matokeo yatakuwa nini? Sayari yetu itakuwa paradiso na hivyo kusudi la awali la Mungu lililotajwa huko Edeni litatimizwa. *Mwanzo 1:28.

Habari Njema ya Kweli

Alipokuwa akitoa ishara yenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitia ndani jambo fulani muhimu sana. (Mathayo 24:3-7) Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Kulingana na mapenzi ya Mungu, mnamo 2007 Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi katika nchi 236 waliwahubiria majirani wao ujumbe wa Ufalme, na kwa shangwe wakatumia zaidi ya saa bilioni 1.4 katika kazi hiyo. Kwa nini Mashahidi wanasadiki kabisa ahadi zilizo katika Biblia? Jibu ni rahisi. Kama makala inayofuata itakavyoonyesha, nyakati zote Mungu hutimiza neno lake.—Waroma 3:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona makala “Maoni ya Biblia: Je, Dunia Itakuwa Paradiso?” kwenye ukurasa wa 10.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Biblia inasema kwamba kutakuwa na “wingi wa amani”