Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ujao Unaotegemeka!

Wakati Ujao Unaotegemeka!

Wakati Ujao Unaotegemeka!

Umefika katika njia panda. Ishara moja inasema, “Wategemee wanadamu na ahadi zao.” Nyingine inasema, “Mtegemee Mungu na Ufalme wake.” Utafuata njia gani?

NI JAMBO la hekima kumtegemea Mungu. “Mtu anayenisikiliza,” Mungu anasema, “atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.” (Methali 1:33) Tunamsikiliza Muumba wetu kwa kufuata mafundisho yaliyo katika Biblia, tukitambua kwamba yanategemeka. (2 Timotheo 3:16) Je, kuna sababu nzuri za kuyategemea? Bila shaka! Kwa mfano, kama tulivyoona katika makala iliyotangulia katika mfululizo huu, Biblia pekee ndiyo inayoeleza kwa usahihi kwa nini wanadamu hawawezi kujitawala kwa mafanikio. Je, hukubali kwamba yale ambayo Biblia inasema yanapatana na mambo hakika?

Usahihi huohuo unaonekana pia katika unabii wa Biblia. Kwa mfano, Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na hali mbaya sana ambazo zingeonyesha kwamba hizi ndizo “siku za mwisho.” Tunaweza kujionea hali hizo. (Mathayo 24:3-7; 2 Timotheo 3:1-5) Biblia hata ilitabiri kwamba wanadamu wangeiharibu sayari yetu. Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ lasema andiko la Ufunuo 11:18.

Maneno hayo yalipoandikwa miaka 2,000 hivi iliyopita, uchafuzi wa hewa, bahari, na ardhi; kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni; na kutoweka kwa jamii za viumbe ambako kumesababishwa na wanadamu, ni baadhi ya mambo ambayo hayangewaziwa hata kidogo. Lakini sivyo ilivyo leo! Ndiyo, Mungu hawezi kusema uwongo. Kila kitu kilichoandikwa katika Neno lake hutimizwa nyakati zote. * (Tito 1:2; Waebrania 6:18) Kwa kweli, Mungu anahusianisha jina lake na kutimizwa kwa neno lake.

Jina Unaloweza Kulitegemea!

Kama vile sahihi inavyohalalisha hundi, ndivyo jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, linavyoandaa uhakikisho kuhusu ahadi zote zilizorekodiwa katika Biblia. * Mwandikaji wa Biblia ambaye Mungu alimjali kwa upendo mara nyingi alisema hivi: “Tumelitegemea jina lake takatifu.”—Zaburi 33:21; 34:4, 6.

Likihusianisha jina la Mungu na sifa yake akiwa baba mwenye kujali, Methali 18:10 linasema: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” Hali kadhalika, Waroma 10:13 linasema: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” Bila shaka, jina la kibinafsi la Mungu si hirizi inayomlinda mtu asipatwe na mabaya. Badala yake, Mungu mwenyewe ndiye anayewaokoa, na wale wanaomwitia kama andiko hilo linavyosema wanafanya hivyo kwa sababu wanamtegemea kabisa, wakijua vizuri kwamba kila mara yeye hutimiza ahadi zake. Zaburi 91:14 inasema hivi: “Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu [Yehova], mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.”

Jiulize, ‘Ninamtegemea nani—Mungu au mwanadamu?’ Mashahidi wa Yehova wamechagua kumtegemea Mungu na Ufalme wake, si kwa sababu tu wanaamini mambo bila msingi au bila kufikiri, lakini kwa sababu imani yao inategemea usadikisho wenye nguvu unaotokana na ujuzi sahihi wa Biblia. (Waebrania 11:1; 1 Yohana 4:1) Kwa sababu hiyo, hawaogopi wakati ujao bali ‘wanashangilia katika tumaini’ lililowekwa mbele yao. Wanakutia moyo uwe na tumaini jangavu kama lao.—Waroma 12:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona toleo la pekee la Novemba (Mwezi wa 11) 2007 la gazeti hili, linalozungumzia kwa urefu swali “Je, Unaweza Kuitegemea Biblia?”

^ fu. 7 Ona sanduku “Jina na Uhakikisho.”

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Kama vile sahihi inavyohalalisha hundi, ndivyo jina la Mungu linavyoandaa uhakikisho kuhusu ahadi zote zilizo katika Biblia

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

JINA NA UHAKIKISHO

Jina la Mungu, Yehova, si kibandiko tu. * Jinsi gani? Jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Kwa maneno rahisi, Mungu ana upendo, nguvu, na hekima ya kuwa chochote anachohitaji kuwa ili kutimiza kusudi na neno lake. Kwa mfano, anaweza kuwa Mwokozi wa waadilifu, Mwangamizaji wa waovu, Msikiaji wa sala, au Baba mwenye upendo—chochote anachochagua kuwa.

“Mimi ni Mungu,” asema Yehova, “Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho . . . Yeye anayesema, ‘Shauri langu mwenyewe litasimama, na kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.’” (Isaya 46:9, 10) Kwa kuwa nyakati zote Mungu hushikamana na ahadi yake na kwa kuwa jina lake, au sifa yake, inahusika, Neno lake lililoandikwa litatimia hakika. “Mungu si mwanadamu kwamba aseme uwongo.”—Hesabu 23:19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Jina Yehova linatofautiana kabisa na majina ya cheo kama vile Mweza-Yote, Muumba, Mungu, na Bwana. Jina hilo linapatikana mara elfu saba hivi katika maandishi ya awali ya Biblia Takatifu. Mungu alijipa jina hilo. Andiko la Kutoka 3:15 linasema hivi: “Jehova . . . hili ndilo jina langu milele.”—The Old Testament in Swahili (Mombasa).