Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Sawa Kutumia Nguvu Ili Kujilinda?

Je, Ni Sawa Kutumia Nguvu Ili Kujilinda?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Sawa Kutumia Nguvu Ili Kujilinda?

KELELE za ghafla zinakuamsha usiku wa manane. Unasikia mtu akipiga hatua. Mtu fulani amevamia nyumba yako. Huku moyo wako ukidunda kama nyundo kifuani mwako, kwa hofu unajiuliza ufanye nini.

Hali hiyo inaweza kumpata mtu yeyote. Uhalifu—hata uhalifu wenye jeuri—hautukii katika nchi au majiji fulani tu. Kwa sababu ya hofu kubwa inayotokana na hali hiyo, watu wengi hununua silaha au kujifunza kupigana ili kujilinda. Serikali fulani zimetunga sheria ambazo zinawapa raia haki ya kutumia mbinu zinazoweza kusababisha kifo ili kujilinda. Lakini Biblia inasema nini? Je, kuna wakati ambapo mtu ana haki ya kutumia nguvu kujilinda au kulinda familia yake?

Mungu Anachukia Jeuri

Biblia inashutumu jeuri na wale wanaotenda jeuri. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.” (Zaburi 11:5) Mungu alihukumu mataifa kadhaa ya kale, kutia ndani watu wake, kwa sababu ya matendo yao ya jeuri na umwagaji wa damu. (Yoeli 3:19; Mika 6:12; Nahumu 3:1) Hata kuua bila kukusudia kwa sababu ya kutokuwa mwangalifu kulikuwa kosa zito chini ya Sheria ambayo Waisraeli walipewa.—Kumbukumbu la Torati 22:8.

Biblia inawahimiza Wakristo wafuatie amani kila siku ili kuepuka mizozo. Mara nyingi, mabishano makali ndiyo yanayosababisha mapambano ya kijeuri. Biblia inasema: “Pasipo na kuni moto huzimika, na pasipo na mchongezi ugomvi hutulia.” (Methali 26:20) Kwa kawaida, upole hupunguza hasira na kuzuia makabiliano ya kijeuri. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

Uhai Unapokuwa Hatarini

Kufuatia amani hakumaanishi kwamba hutawahi kamwe kushambuliwa kwa jeuri. Katika historia yote, waabudu waaminifu wa Mungu wametendwa jeuri. (Mwanzo 4:8; Ayubu 1:14, 15, 17) Mtu anapaswa kufanya nini akikabiliwa na mhalifu mwenye silaha? Yesu aliagiza hivi: “Msimpinge yeye aliye mwovu.” (Mathayo 5:39) Pia alisema: “Anayechukua vazi lako la nje, usimzuilie hata lile vazi la ndani.” (Luka 6:29) Yesu hakuunga mkono wazo la kutumia silaha kulinda mali. Hivyo, mtu mwenye hekima akikabiliwa na mhalifu mwenye silaha, hatamzuilia asichukue vitu vyake vyenye thamani. Kwa kweli, uhai ni wenye thamani sana kuliko mali!

Kwa upande mwingine, vipi mhalifu anapotishia uhai wa mtu? Sheria fulani ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale inatusaidia kujibu swali hilo. Ikiwa mwizi angeshikwa mchana na kuuawa, muuaji angekuwa na hatia ya kuua. Kwa wazi ilikuwa hivyo kwa sababu mwizi hakupaswa kuhukumiwa kifo, naye angeweza kuonekana waziwazi na kuadhibiwa. Hata hivyo, ikiwa mvamizi angepigwa na kuuawa usiku, mwenye nyumba hangekuwa na hatia kwa sababu ingekuwa vigumu kwake kuona kile ambacho mvamizi huyo alikuwa akifanya na hivyo kuelewa nia yake. Kwa kufaa, mwenye nyumba angeweza kukata kauli kwamba familia yake ilikuwa hatarini na hivyo kuchukua hatua ili kuilinda.—Kutoka 22:2, 3.

Hivyo, Biblia inaonyesha kwamba mtu anaweza kujilinda au kuilinda familia yake ikishambuliwa. Huenda akakinga ngumi, akamzuia mshambuliaji kwa kumshika, au hata kumpiga ili kumwogopesha au kumzuia asiendelee kumshambulia. Nia yake ingekuwa kuzuia au kukomesha shambulizi. Kwa sababu hiyo, ikiwa mshambuliaji angeumizwa vibaya au hata kuuawa katika hali kama hizo, kifo chake hakingekuwa kitendo cha makusudi.

Ulinzi Bora

Kwa wazi, chini ya hali fulani mtu ana haki ya kutumia kiasi fulani nguvu ili kujilinda. Watu wana haki ya kujilinda na kuwalinda wapendwa wao wanaposhambuliwa au uhai wao unapokuwa hatarini. Ikiwa haiwezekani kukimbia, Biblia haituzuii kutumia nguvu kujilinda. Hata hivyo, mwendo wa hekima ungekuwa kujitahidi tuwezavyo kuepuka hali zinazoweza kutokeza jeuri.—Methali 16:32.

Biblia inatuhimiza ‘tutafute amani na kuifuatilia’ katika kila sehemu ya maisha yetu. (1 Petro 3:11) Kanuni hiyo bora inaweza kutusaidia kuishi kwa amani.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini tunapaswa kuepuka jeuri?—Zaburi 11:5.

▪ Ni hatua gani ya hekima tunayopaswa kuchukua tunapolinda mali? —Methali 16:32; Luka 12:15.

▪ Ni mtazamo gani kuhusu kupigana unaoweza kuzuia hatari?—Waroma 12:18.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Biblia inaonyesha kwamba mtu anaweza kujilinda au kuilinda familia yake ikishambuliwa