Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kuna Tumaini Gani kwa Ukristo? (Februari 2007) Mambo mengi mnayosema yanapatana na Neno la Mungu, nami nakubaliana nanyi. Hata hivyo, kuna masuala mawili katika gazeti lenu ambayo yananifanya nihisi vibaya. Suala moja linahusu jinsi mnavyodunisha makanisa ya Kikristo, na suala lingine linahusu jinsi mnavyoonekana kujiinua juu ya dini nyingine. Ingependeza sana ikiwa sote tungekubaliana na tungekuwa na imani moja, lakini sivyo ilivyo. Sioni kanisa au dini yoyote kuwa bora kuliko nyingine.

S. S., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Mashahidi wa Yehova hawachukii washiriki mmoja-mmoja wa dini nyingine, wala hatujioni kuwa bora kuliko wengine. Tunatambua kwamba watu “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa kuwa tunajua hilo, tunatumia nguvu, mali, na wakati wetu mwingi kuwatembelea watu nyumbani mwao ili kuwapa kweli za Biblia, kutia ndani tumaini nzuri ajabu lililo katika Biblia. Hata hivyo, kama vile Yesu na wafuasi wake walivyozungumza kwa ujasiri ili kufunua unafiki na uwongo wa dini, Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo.

Ungejibuje? Mwanzoni nilipitia sehemu hii mara chache sana na watoto wangu wawili. Lakini sasa naiona kuwa kifaa chenye nguvu ninachoweza kutumia kupanda kweli ya Biblia katika mioyo ya watoto wangu. Isitoshe, mimi mwenyewe ninafurahia kuitumia kuimarisha imani yangu.

I. H., Jamhuri ya Cheki

Ninathamini sana sehemu hii yenye kupendeza ambayo inanipa mambo ya kujifunza katika funzo la kibinafsi. Mambo yote yamefikiriwa kwa uangalifu sana, hata yale madogo! Inanifanya nimkaribie hata zaidi Baba yangu mwenye hekima, Yehova.

A. S., Urusi

“Yehova, Tafadhali Niruhusu Nikutumikie” (Julai 2007) Imani yangu kwa Yehova iliimarishwa kwa kusoma simulizi la maisha la Danielle Hall. Akiwa mtoto mdogo, hakuogopa kuambia kila mtu shuleni kwamba alikuwa Shahidi wa Yehova. Nina hakika kwamba wanashule wengi ambao ni Mashahidi watafanya vivyo hivyo.

A. R., Madagaska

Nina umri wa miaka tisa. Mimi na mama yangu tumemaliza tu kusoma simulizi la Danielle. Simulizi hilo limenifanya nihisi kwamba nina pendeleo kwa sababu wazazi wangu wako katika kweli na si vigumu kwangu kumtumikia Yehova. Nilifurahia sana wazo la kwamba “hata tuwe wapi, Yehova yuko karibu nasi.” Pia nilithamini kwamba kila siku Danielle alipotoka shuleni, aliketi kitandani mwake na kuongea na Yehova kuhusu siku yake, kana kwamba alikuwa baba yake. Ningependa kuiga kielelezo chake!

A. D., Italia

“Vijana Huuliza . . . kwa Nini Wengine Hunitenga?” (Julai 2007) Makala hiyo ilikuwa nzuri sana kwa sababu nilihisi iliandikwa hasa kwa ajili yangu. Pia nilifurahia maswali yaliyokuwa katika makala hiyo na nafasi zilizoachwa ili mtu ajaze majibu. Asanteni. Ilinisaidia sana.

C. A., Kanada