Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika

“Tunajaribu sana kuwapa mwongozo mwana na binti yetu, lakini ni kama tunawakemea daima kwa sababu fulani. Nyakati nyingine hatujui ikiwa tunawafanya wajiamini au wasijiamini. Ni vigumu sana kuwa na usawaziko.”—George na Lauren, Australia.

KUMLEA kijana anayebalehe si kazi rahisi. Mbali na kukabiliana na matatizo mapya yanayotokezwa na mtoto wao, huenda wazazi wakahuzunika au kuwa na wasiwasi kwa sababu mwana au binti yao anakua. “Kutambua kwamba watoto wetu watatuacha siku moja ni wazo lenye kuhuzunisha,” anakiri Frank, baba mmoja huko Australia. “Si rahisi kukubali kwamba si wewe unayeongoza maisha yao sasa.”

Lia, aliyenukuliwa mapema katika mfululizo huu, anakubaliana na hilo. “Ni vigumu kumtendea mwanangu kama mtu mzima, kwa kuwa bado namwona tu kuwa mvulana wangu mdogo,” anasema. “Ni kana kwamba alianza shule jana tu!”

Ingawa ni vigumu kukubali hilo, ukweli ni kwamba vijana wanaobalehe si watoto tena. Wao ni watoto wanaozoezwa kuwa watu wazima na wazazi wao ni walimu na wachocheaji wao. Hata hivyo, kama George na Lauren waliotajwa hapo juu, wazazi wana uwezo wa kumsaidia kijana ajiamini au asijiamini. Wazazi wanaweza kuonyeshaje usawaziko unaofaa? Biblia ina mashauri yanayosaidia. (Isaya 48:17, 18) Acheni tuchunguze mifano fulani.

Mawasiliano Mazuri Ni Muhimu

Biblia inawaambia Wakristo wawe ‘wepesi kuhusu kusikia’ na ‘wasiwe wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Ijapokuwa shauri hilo linafaa unaposhughulika na watoto wa umri wowote ule, kusikia—au kusikiliza—ni muhimu hasa unaposhughulika na vijana wanaobalehe. Na huenda hilo likahitaji jitihada nyingi.

“Nilihitaji kuboresha ustadi wangu wa kuwasiliana na wana wangu walipokuwa matineja,” anasema Peter, baba mmoja huko Uingereza. “Wavulana wetu walipokuwa wachanga, mimi na mke wangu tuliwaambia walichopaswa kufanya, nao walitii. Lakini kwa kuwa sasa wamekua, tunahitaji kujadiliana, kuzungumza kwa undani, na kuwaacha watumie uwezo wao wa kufikiri kuchanganua mambo. Kwa ufupi, tunahitaji kuufikia moyo.”—2 Timotheo 3:14.

Ni muhimu kusikiliza hasa maoni yanapotofautiana. (Methali 17:27) Danielle anayeishi Uingereza, alijionea ukweli wa jambo hilo. Anasema hivi: “Nilikuwa na tatizo na mmoja wa binti zangu kuhusu jinsi alivyonijibu nilipomwambia afanye chochote. Lakini aliniambia kwamba sikuzote nilikuwa nikimfokea na kumwamrisha. Tulitatua tatizo hilo kwa kuketi na nikamsikiliza naye akanisikiliza kikweli. Alieleza jinsi nilivyokuwa nikizungumza naye na jinsi nilivyomfanya ahisi, nami nikamweleza maoni na hisia zangu.”

Danielle aligundua kwamba kuwa “mwepesi kuhusu kusikia” kulimsaidia kutambua kiini cha tatizo. “Sasa ninajitahidi kumtendea binti yangu kwa subira,” anasema, “nami ninajitahidi kuzungumza naye wakati ambapo sijakasirika.” Aliongeza hivi: “Uhusiano wetu unakuwa bora.”

Methali 18:13 inasema: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” Greg, baba mmoja huko Australia, alijionea ukweli wa jambo hilo. “Nyakati nyingine matatizo kati yetu na watoto wetu hutokea wakati ambapo mimi na mke wangu tunawakemea watoto wetu badala ya kuwasikiliza kwanza na kutambua jinsi wanavyohisi,” anasema. “Hata ikiwa hatukubaliani kabisa na mitazamo yao, tumeona kwamba ni muhimu sana kuwaruhusu wafunue hisia zao kabla ya kuwarekebisha au kuwashauri inavyohitajika.”

Uhuru Mwingi Kadiri Gani?

Huenda kisababishi kikubwa zaidi cha matatizo kati ya wazazi na vijana wanaobalehe kikahusiana na suala la uhuru. Kijana anapaswa kupewa uhuru mwingi kadiri gani? Kuhusu uhuru, baba mmoja alisema hivi: “Mara nyingine, mimi huhisi kwamba binti yangu akionja asali atachonga mzinga.”

Kwa wazi, kuwapa vijana uhuru usio na mipaka kutakuwa na matokeo mabaya. Kwa kweli, Biblia inaonya kwamba “mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” (Methali 29:15) Vijana wa umri wowote ule wanahitaji mwongozo thabiti, na inapohusu kutekeleza sheria za familia wazazi wanapaswa kuwa wenye upendo lakini imara. (Waefeso 6:4) Wakati huohuo, vijana wanapaswa kupewa kiasi fulani cha uhuru ili wawe tayari zaidi kufanya maamuzi ya hekima baadaye maishani.

Kwa mfano, fikiria jinsi ulivyojifunza kutembea. Mwanzoni, ulipokuwa mtoto mchanga, ulibebwa. Muda si muda, ulianza kutambaa kisha kutembea. Bila shaka, kutambaa au kutembea kunaweza kumhatarisha mtoto mdogo. Hivyo, wazazi wako walikuwa waangalifu sana na huenda walikuwekea vizuizi fulani ili usikaribie maeneo hatari, kama vile ngazi. Hata hivyo, walikuruhusu utembee peke yako na baada ya kuanguka mara kadhaa, hatimaye ulifaulu kutembea bila matatizo.

Kupata uhuru kunahusisha hatua kama hizo. Mwanzoni, kwa njia ya mfano wazazi wanawabeba watoto wao wachanga kwa kuwafanyia maamuzi. Baadaye, kadiri watoto wanavyokomaa, wazazi wanawaruhusu watambae kwa kujifanyia maamuzi fulani. Wakati huohuo wanawawekea vijana vizuizi ambavyo vinawalinda kutokana na madhara. Kadiri watoto wao wanavyokomaa, ndivyo wazazi wanavyowaruhusu “watembee” peke yao. Kisha watakapokuwa watu wazima, watakuwa na uwezo kamili wa ‘kubeba mzigo wao wenyewe.’—Wagalatia 6:5.

Kujifunza Kutokana na Mfano wa Biblia

Kwa wazi, akiwa na umri wa miaka 12, Yesu alikuwa amepewa uhuru fulani na wazazi wake, lakini hakuutumia vibaya. Badala yake, ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake na “akazidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.”—Luka 2:51, 52.

Ukiwa mzazi, unaweza kujifunza kutokana na mfano huo kwa kuwapa watoto wako uhuru zaidi kadiri wanavyoonyesha wanaweza kuutumia vizuri. Kuhusiana na hilo, fikiria yale ambayo wazazi fulani wamesema kuhusu mambo waliyojionea.

“Nilikuwa nikiingilia sana shughuli za watoto wangu. Lakini baadaye, nilianza kuwafundisha kanuni mbalimbali na kuwaacha wafanye uamuzi kupatana na yale waliyojifunza. Baada ya hapo, niliona kwamba walianza kufikiria kwa makini zaidi maamuzi yao.”—Soo Hyun, Korea.

“Nyakati zote mimi na mume wangu huwa na wasiwasi kuhusu kuwapa watoto wetu uhuru, lakini hatujaacha hilo lituzuie kuwaruhusu watumie uhuru wanaostahili kwa njia inayofaa.”—Daria, Brazili.

“Nimegundua kwamba ni muhimu kumpongeza mwana wangu ambaye ni tineja anapotumia vizuri uhuru ninaompa. Pia mimi hufanya yale ninayomwambia afanye. Kwa mfano, mimi humwambia ninakoenda na ninachofanya. Pia ikiwa nitachelewa, mimi humjulisha.”—Anna, Italia.

“Katika nyumba yetu tunasisitiza kwamba wana wetu hawana haki ya kujitegemea lakini wanapaswa kuthibitisha kwamba wanaweza kutegemeka.”—Peter, Uingereza.

Kukabili Matokeo

Biblia inasema hivi: “Ni jambo jema kwa mwanamume kuchukua nira wakati wa ujana wake.” (Maombolezo 3:27) Mojawapo ya njia bora ya kijana kujichukulia nira ya wajibu ni kujionea mwenyewe ukweli wa taarifa hii: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.

Wakiwa na nia nzuri, huenda wazazi fulani wakawakinga vijana wao kutokana na matokeo ya matendo yasiyo ya hekima. Kwa mfano, tuseme kwamba kwa kununua vitu asivyohitaji mvulana fulani anajiingiza katika deni. Atajifunza nini ikiwa Baba na Mama watalipa deni hilo? Kwa upande mwingine, mvulana huyo angejifunza nini ikiwa wazazi wake wangemsaidia kupanga jinsi atakavyojilipia deni hilo?

Wazazi hawafaidi watoto wao hata kidogo wanapowakinga kutokana na matokeo ya tabia zao za kutokuwa waangalifu. Badala ya kuwatayarisha kwa ajili ya maisha ya utu uzima, kufanya hivyo kunawafundisha kwamba nyakati zote kutakuwa na mtu wa kuwaondoa matatani, kuwatatulia matatizo wanayojiletea, na kuwafunikia makosa yao. Inafaa zaidi kuwaacha vijana wavune walichopanda na wajifunze kutatua matatizo yao. Hiyo ni sehemu muhimu ya ‘kuzoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’—Waebrania 5:14.

“Mtu Anayebadilika na Kukomaa”

Hapana shaka kwamba wazazi wa vijana wanaobalehe wana kazi ngumu. Nyakati fulani, huenda watafadhaika na kutokwa na machozi wanapojitahidi kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Mwishowe, kulea watoto kwa mafanikio hakumaanishi kuwadhibiti, bali kunamaanisha kuwafundisha na kukazia kanuni zinazofaa mioyoni mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Bila shaka ni rahisi kusema hivyo kuliko kutenda. “Tunashughulika na mtu anayebadilika na kukomaa,” anasema Greg, aliyenukuliwa mapema. “Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kuendelea kumfahamu mtu huyo mpya na kujirekebisha ili kupatana naye.”

Jitahidi kufuata kanuni za Biblia zilizozungumziwa katika makala hii. Uwe na usawaziko kuhusu yale unayotazamia kutoka kwa watoto wako. Lakini usimwachie kamwe mtu mwingine wajibu wako wa kuwa kielelezo kikuu maishani mwao. Biblia inasema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”—Methali 22:6.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Kupata uhuru ni kama kujifunza kutembea—unapatikana hatua kwa hatua

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Kabla ya kuwa kijana, Yesu alipewa uhuru fulani

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

“Kusisitiza Mamlaka Yako”

Hata ingawa kijana wako anaweza kukasirishwa na sheria unazoweka hilo halimaanishi kwamba unapaswa kulegeza mamlaka yako. Kumbuka, vijana wanaobalehe hawana ujuzi maishani na bado wanahitaji mwongozo.—Methali 22:15.

Katika kitabu chake New Parent Power! John Rosemond anaandika hivi: “Ni rahisi kwa wazazi kukubali washinikizwe na msukosuko wa kihisia wa watoto wao na kuanza kuwapa uhuru zaidi kuliko wanavyostahili ili kuepuka magombano. Lakini wazazi hawapaswi kamwe kufanya hivyo. Huo ndio wakati wa kusisitiza mamlaka yao, si wakati wa kuwaachilia watoto wapuuze mamlaka hiyo. Ingawa hapana shaka watapinga wazo hilo, huo pia ndio wakati wa watoto kutambua kwamba wazazi wao wako tayari kushika usukani.”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kuwapa Uhuru Zaidi

Mara nyingi vijana hutaka uhuru mwingi kuliko wanavyostahili. Wakati huohuo, wazazi fulani huwapa uhuru mdogo kuliko wanavyoweza. Usawaziko unaweza kupatikana jinsi gani? Kwanza huenda ukataka kuchunguza orodha iliyo hapa chini. Mwana au binti yako ni mwenye kutegemeka katika mambo gani?

□ Kuchagua marafiki

□ Kuchagua mavazi

□ Kutumia pesa vizuri

□ Kurudi nyumbani kwa wakati uliowekwa

□ Kumaliza kazi za nyumbani

□ Kumaliza kazi za shule

□ Kuomba msamaha unapokosea

□ Mengine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Ikiwa tayari kijana wako anaonyesha ukomavu katika baadhi ya mambo yaliyo hapo juu, kwa nini usifikirie njia fulani za kumpa uhuru zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Waruhusu wafunue hisia zao kabla ya kuwarekebisha au kuwashauri inavyohitajika

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wazazi wanapaswa kuwazoeza watoto wao kuwa wenye kutegemeka