Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Uelewaji Unavyohusika

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Uelewaji Unavyohusika

Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Uelewaji Unavyohusika

Tuseme unatembelea nchi ya kigeni na huzungumzi lugha ya wenyeji wa nchi hiyo. Hapana shaka kwamba itakuwa vigumu kuwasiliana nao—lakini hilo halimaanishi hamwezi kuwasiliana. Kwa mfano, kamusi inaweza kukusaidia kujifunza semi za msingi katika lugha hiyo. Au mtu fulani anaweza kutafsiri mazungumzo yenu ili mweze kuelewana.

NYAKATI nyingine, huenda wazazi wanaolea vijana wakahisi kwamba wamo katika hali kama hiyo. Sawa na lugha ya kigeni, huenda ikawa vigumu kuelewa tabia za vijana wanaobalehe—lakini hilo halimaanishi kwamba haziwezi kueleweka. Siri ya mafanikio ni wazazi wajaribu kuelewa hasa kinachotukia katika kipindi hicho cha ukuzi chenye msisimko na kinachotatanisha.

Kiini cha Tabia za Vijana

Kijana anapotaka kujitegemea, nyakati nyingine hilo halimaanishi kwamba anataka kuasi. Kumbuka, Biblia inasema kwamba baada ya muda, “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ili kujitayarisha kwa ajili ya majukumu mazito watakapokuwa watu wazima, vijana wanahitaji angalau uzoefu fulani wa kufanya maamuzi.

Chunguza kile ambacho huenda kikawa kiini cha tabia zilizoonwa na wazazi walionukuliwa katika makala iliyotangulia.

Lia, huko Uingereza, alisema hivi: “Kwa ghafula mwana wangu alianza kushikilia sana maoni yake na kutilia shaka zaidi mamlaka yetu.”

Kama watoto wadogo, vijana huuliza tena na tena, “Kwa nini?” Hata hivyo, huenda vijana wasitosheke na jibu fupi. Kwa sababu gani? Mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa . . . nikifikiri kama mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Vijana wanapositawisha uwezo wao wa kufikiri, wanahitaji maelezo zaidi ili “nguvu zao za ufahamu” zizoezwe.—Waebrania 5:14.

John huko Ghana, alisema hivi: “Binti zetu walianza kujihangaikia sana, hasa kuhusu sura yao.”

Iwe ukuzi wa haraka unaotukia wakati wa kubalehe utaanza mapema, kwa kuchelewa, ama utaanza kwa wakati hususa, unawafanya vijana wahangaikie sura yao kupita kiasi. Wasichana wanaweza kusisimkia umbo lao jipya au kuwa na wasiwasi kulihusu, au wanaweza pia kuwa na hisia zote mbili. Isitoshe, wanapokuwa na chunusi—na wanapoanza kutumia vipodozi—ni rahisi kuelewa ni kwa nini vijana wanatumia muda mrefu zaidi kujitazama kwenye kioo kuliko muda wanaotumia kujifunza.

Daniel, huko Filipino, alieleza: “Watoto wetu walikuwa na mwelekeo wa kuficha matendo na maoni yao na walitaka faragha zaidi. Badala ya kuwa nasi, mara nyingi walipendelea kuwa na marafiki wao.”

Kuficha siri kunaweza kuwa hatari. (Waefeso 5:12) Hata hivyo, faragha si kuficha siri. Hata Yesu alitambua umuhimu wa kutafuta “mahali pasipo na watu ili awe peke yake.” (Mathayo 14:13) Pia, kadiri vijana wanavyokua, wanahitaji faragha—na wanataka watu wazima waheshimu faragha hiyo. Kiwango fulani cha faragha kinawasaidia vijana wawaze na kuwazua. Huo ni uwezo muhimu utakaowafaa sana watakapokuwa watu wazima.

Hali kadhalika, kujifunza jinsi ya kuanzisha urafiki ni sehemu ya ukuzi. Ni kweli kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Hata hivyo, Biblia inasema hivi pia: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Kujifunza jinsi ya kuanzisha na kudumisha urafiki unaofaa ni uwezo muhimu watakaotumia hata watakapokuwa watu wazima.

Wakikabili mojawapo ya hali hizo, ingefaa wazazi wajitahidi kujipatia uelewaji ili wasielewe vibaya tabia za vijana wao. Bila shaka, mbali na uelewaji wanapaswa kuwa na hekima, yaani, uwezo wa kushughulikia hali kwa njia itakayoleta matokeo bora zaidi. Wazazi wa vijana wanaobalehe wanaweza kufanyaje hivyo?

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Vijana wanapositawisha uwezo wao wa kufikiri, wanahitaji maelezo zaidi kuhusu sheria za familia