Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kwa Nini Mtoto Wangu Amebadilika Sana?”

“Kwa Nini Mtoto Wangu Amebadilika Sana?”

“Kwa Nini Mtoto Wangu Amebadilika Sana?”

Scott na Sandra * walipigwa na butwaa binti yao mwenye umri wa miaka 15 alipoingia sebuleni. Nywele zake zilizokuwa za rangi ya dhahabu, sasa zilikuwa nyekundu! Mazungumzo yaliyofuata yaliwaacha midomo wazi.

“Je, tulikupa ruhusa ya kutia rangi nywele zako?”

“Kwa kweli, hamkusema sipaswi kufanya hivyo.”

“Mbona hukutuuliza?”

“Kwa sababu nilijua mngekataa!”

SCOTT na Sandra wanaweza kuthibitisha kwamba miaka ya kubalehe ni kipindi cha msukosuko—si kwa vijana tu bali pia kwa wazazi wao. Kwa kweli, baba na mama wengi hawako tayari kukabiliana na mabadiliko makubwa yanayotokea mtoto wao anapobalehe. “Binti yetu alibadilika bila kuonyesha dalili zozote,” anakumbuka Barbara, mama mmoja huko Kanada. “Nilijiuliza, ‘Kwa nini mtoto wangu amebadilika sana?’ Ni kana kwamba alichukuliwa tukiwa usingizini na tukaletewa mtoto tofauti!”

Kwa kweli, mambo yaliyompata Barbara yamewapata wengine pia. Fikiria yale ambayo wazazi katika sehemu mbalimbali ulimwenguni waliwaambia waandishi wa Amkeni!

“Alipofikia umri wa kubalehe, kwa ghafula mwana wangu alianza kushikilia sana maoni yake na kutilia shaka zaidi mamlaka yetu.”—Lia, Uingereza.

“Binti zetu walianza kujihangaikia sana, hasa kuhusu sura yao.”—John, Ghana.

“Mwana wangu alitaka kujifanyia maamuzi. Hakutaka kuambiwa la kufanya.”—Celine, Brazili.

“Binti yetu hakutaka tena tumkumbatie wala kumbusu.”—Andrew, Kanada.

“Wavulana wetu walianza kuwa washindani sana. Badala ya kukubali maamuzi yetu, waliyapinga na kubishana nasi kuyahusu.”—Steve, Australia.

“Binti yangu alificha hisia zake. Alijifungia katika ulimwengu wake mwenyewe, naye alikasirika nilipojaribu kumtia moyo anifunulie hisia zake.”—Joanne, Mexico.

“Watoto wetu walikuwa na mwelekeo wa kuficha matendo na maoni yao na walitaka faragha zaidi. Badala ya kuwa nasi, mara nyingi walipendelea kuwa na marafiki wao.”—Daniel, Filipino.

Ukiwa mzazi wa kijana anayebalehe, huenda ukaona kwamba baadhi ya maelezo yaliyo hapo juu yanapatana sana na hali zako. Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba jitihada zako za kumwelewa “mgeni” huyo aliye kati yenu, yaani, mwana au binti yenu zinaweza kufanikiwa. Biblia inaweza kukusaidia. Jinsi gani?

Hekima na Uelewaji

Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Jipatie hekima, jipatie uelewaji.” (Methali 4:5) Sifa hizo mbili ni muhimu unaposhughulika na kijana anayebalehe. Unahitaji uelewaji si ili tu kufahamu tabia zake bali pia kutambua yale hasa yanayompata mtoto wako. Pia unahitaji hekima ili kumsaidia kwa mafanikio kijana wako awe mtu mzima anayetegemeka.

Usifikiri kwamba mwana au binti yako hakuhitaji kwa sababu inaonekana kuwa hamna uhusiano wa karibu kama zamani. Ukweli ni kwamba, vijana wanaobalehe wanahitaji—na hata wanataka—wazazi wao wajihusishe na maisha yao katika kipindi hicho kigumu. Uelewaji na hekima zitakusaidiaje kuandaa mwongozo huo?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina katika mfululizo huu yamebadilishwa.