Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahali Niliposikia Jina Yehova Mara ya Kwanza

Mahali Niliposikia Jina Yehova Mara ya Kwanza

Mahali Niliposikia Jina Yehova Mara ya Kwanza

Limesimuliwa na Pavol Kovár

Mabomu yalipokuwa yakiangushwa, ilikuwa vigumu kwetu kukimbilia mahali petu pa kujificha. Mashambulizi yalipozidi na kufanya maficho yetu yatikisike, mfungwa mwenzangu alisali hivi kwa sauti: “Ee Yehova, tuokoe! Tafadhali tuokoe kwa ajili ya jina lako takatifu!”

ILIKUWA Januari 8, 1945 (8/1/1945), na nilikuwa mfungwa wa vita katika jiji la Linz, Austria. Kulikuwa na watu 250 hivi katika maficho hayo, na sote tuliokoka mashambulizi hayo. Tulipotoka nje, kulikuwa na uharibifu mkubwa. Kwa muda mrefu nilikumbuka sala ya kutoka moyoni ya yule mfungwa ingawa sikupata kumfahamu. Kabla sijasimulia jinsi nilivyojifunza kumhusu Yehova, acha nieleze kifupi kuhusu malezi yangu.

Nilizaliwa Septemba 28, 1921 (28/9/1921), katika nyumba moja karibu na kijiji cha Krajné, magharibi mwa Slovakia, ambayo wakati huo ilikuwa sehemu ya Chekoslovakia. Wazazi wangu walikuwa Waprotestanti, nao walishikilia dini sana. Kila Jumapili (Siku ya Yenga) asubuhi, Baba alitusomea Biblia, na Mama pamoja nasi watoto wanne tulisikiliza kwa makini. Hata hivyo, sikumbuki baba yangu akitumia jina Yehova. Maisha katika eneo letu yalikuwa ya hali ya chini, lakini tuliridhika na vitu vichache tulivyokuwa navyo.

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza mnamo 1939, watu walikuwa na hofu. Wengi walikumbuka mateso yaliyotokana na Vita vya Kwanza vya Ulimwengu miaka 20 hivi mapema. Mnamo 1942, nilijiunga na jeshi la Slovakia. Ingawa Slovakia ilikuwa ikiunga mkono Ujerumani, katika Agosti (Mwezi wa 8) 1944 kulikuwa na jaribio la kurudisha tena utawala wa kidemokrasia. Jaribio hilo liliposhindwa, nilikuwa miongoni mwa maelfu ya wanajeshi Waslovakia walioshikwa na kupelekwa katika maeneo yaliyodhibitiwa na Wajerumani. Hatimaye nilipelekwa katika kambi ndogo ya Gusen, iliyopakana na kambi ya mateso makali ya Mauthausen karibu na Linz.

Mfungwa wa Vita

Tulifanya kazi katika kiwanda cha kutengeneza ndege ambacho kilikuwa karibu na kijiji cha Sankt Georgen an der Gusen. Nilifanya kazi ya kupasua mbao. Hatukuwa na chakula cha kutosha, na mnamo Januari 1945, tulipewa chakula kidogo hata zaidi majeshi ya Nazi yalipoanza kushindwa pande zote. Tulipikiwa tu supu kidogo. Kila asubuhi, wafanyakazi kutoka kambi kuu ya Mauthausen waliwasili. Mara nyingi, askari waliwapiga na kuwaua wafungwa waliokuwa dhaifu sana wasiweze kufanya kazi. Baadaye, wafungwa wengine walitupa maiti hizo kwenye gari la kukokotwa na kuzipeleka hadi mahali pa kuteketezea maiti.

Licha ya taabu hizo zote, tulitumaini kwamba vita vitakoma karibuni. Mei 5, 1945 (5/5/1945), miezi minne baada ya mashambulizi ya mabomu niliyotaja mwanzoni mwa simulizi hili, kelele za mchafuko ziliniamsha na nikakimbia nje. Hakukuwa na askari yeyote, kulikuwa na rundo la bunduki, na malango yalikuwa wazi kabisa. Tungeweza kuona kambi ile nyingine ng’ambo ya uwanja. Wafungwa walioachiliwa walitoka huko wakikimbia kama nyuki kutoka katika mzinga uliokuwa ukiteketea. Walipokuwa huru, walilipiza kisasi kwa ukatili. Bado ninakumbuka vizuri machinjo yaliyotokea.

Wafungwa walilipiza kisasi kwa kuwapiga na kuwaua kapos, yaani, wafungwa walioshirikiana na askari wa magereza. Mara nyingi, kapos walikuwa wakatili zaidi kuliko askari wa Nazi. Nilimwona mfungwa mmoja akimpiga na kumuua kapo mmoja huku akisema hivi kwa sauti: “Alimuua baba yangu. Tulikuwa tumevumilia hali mbaya kwa muda huo wote kisha akamuua siku mbili tu zilizopita!” Kufikia jioni, uwanja ulikuwa umejaa mamia ya maiti za kapos na wafungwa wengine. Baadaye, kabla ya kuondoka, tulitembea katika kambi hiyo ili kuona mahali pa kuulia watu, hasa tanuru na vyumba vya gesi yenye sumu.

Najifunza Kumhusu Mungu wa Kweli

Nilifika nyumbani mwishoni mwa Mei 1945. Niliporudi nyumbani nilipata kwamba mbali na kujifunza jina la Mungu, jina ambalo nilisikia nikiwa kwenye handaki, wazazi wangu walikuwa Mashahidi wa Yehova. Muda mfupi baada ya kurudi nyumbani, nilikutana na Oľga, msichana aliyempenda Mungu, na mwaka mmoja baadaye tukaoana. Bidii yake kwa ajili ya kweli ya Biblia ilinichochea kuendelea kujifunza kumhusu Yehova. Katika mojawapo ya makusanyiko ya mwisho tuliyofanya kabla ya kazi yetu kupigwa marufuku na serikali mpya ya Kikomunisti mnamo 1949, mimi, Oľga, na wengine 50 hivi tulibatizwa katika Mto Váh huko Piešťany. Baada ya muda, tulipata binti wawili Oľga na Vlasta.

Ján Sebín, Shahidi aliyesaidia kupanga upya kazi ya kuhubiri baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, aliishi kwetu mara kwa mara, nami nilihubiri naye mara nyingi. Licha ya kuendelea kuteswa na Wakomunisti, tuliendelea kuhubiri. Kwa busara tulizungumza na watu kuhusu kweli za Biblia, na muda si muda tukawa na mafunzo mengi ya Biblia. Ján alipohama, mimi na mke wangu tuliendelea kujifunza na watu hao. Baadaye katika makusanyiko yetu, tulikutana na baadhi yao wakiwa na watoto na hata wajukuu wao. Hilo lilituletea shangwe kama nini!

Utumishi wa Pekee

Kufikia 1953 Mashahidi wengi waliokuwa wakielekeza kazi ya kuhubiri walifungwa gerezani. Kwa hiyo, niliombwa nihubiri eneo lililokuwa kilomita 150 hivi kutoka kwetu. Kila baada ya majuma mawili, nilipomaliza kazi ya kimwili Jumamosi (Siku ya Posho) alasiri, nilipanda gari-moshi kutoka mji wa Nové Mesto nad Váhom hadi mji wa Martin, huko kaskazini ya kati ya Slovakia. Jumamosi nilizungumza na watu kuhusu Biblia hadi usiku, na Jumapili nilifanya hivyo siku nzima. Jumapili jioni, nilipanda gari-moshi na kurudi Nové Mesto. Kwa kawaida, niliwasili usiku wa manane nyumbani kwa wenzi wa ndoa wazee ambao walinikaribisha nikae nao hadi asubuhi. Asubuhi nilienda kazini na kurudi kwa familia yangu katika kijiji cha Krajné, Jumatatu (Siku ya 1) usiku. Oľga aliwatunza binti zetu mwishoni mwa juma wakati sikuwa nyumbani.

Kisha, mnamo 1956, niliombwa niwe mwangalizi wa mzunguko, kazi ya kutembelea makutaniko katika eneo letu ili kuyaimarisha kiroho. Kwa kuwa waangalizi wengi walikuwa gerezani, niliona uhitaji wa kukubali mgawo huo. Mimi na mke wangu tulikuwa na uhakika kwamba Yehova angesaidia familia yetu.

Kulingana na sheria ya Wakomunisti, kila raia alipaswa kufanya kazi ya kimwili. Serikali iliwaona wale wasio na kazi kuwa kupe kwa jamii na iliwatupa gerezani. Kwa hiyo sikuacha kazi. Nilitumia miisho-juma miwili na familia yangu kufanya mambo ya kiroho na mambo mengine; lakini ile miisho-juma mingine, nilitembelea mojawapo ya makutaniko sita ya karibu katika mzunguko.

Kutokeza Vichapo Tukiwa Chini ya Marufuku

Waangalizi wa mzunguko walikuwa na jukumu la kufanya mipango ili kila kutaniko katika mzunguko lipate vichapo vya Biblia. Mwanzoni, magazeti yalinakiliwa kwa mkono au kupigwa chapa kwa mashini. Baadaye tulipata filamu za picha za Mnara wa Mlinzi na kuzituma kwa makutaniko. Kisha zilisafishwa na nakala kutolewa kwenye karatasi ya picha. Kwa kuwa mtu yeyote aliyenunua kiasi kikubwa cha karatasi hizo za picha angeshukiwa, wale waliozinunua walipaswa kujihadhari na kuwa wajasiri.

Štefan Hučko alipenda sana kazi hiyo na aliifanya kwa ustadi. Kwa mfano, pindi moja, Štefan alienda katika duka la kupiga picha lililokuwa mbali na mji wao ili kununua karatasi na alikuwa karibu kuondoka kwa sababu duka hilo halikuwa na karatasi zozote. Hata hivyo, alimwona mfanyakazi wa duka hilo aliyekuwa ameahidi kumwagizia karatasi hizo. Štefan alipotaka kumkaribia, alimwona polisi akiingia dukani. Wakati huohuo, yule mfanyakazi alimwona Štefan na akamwambia hivi kwa furaha: “Aisee! Tulipokea karatasi za picha ulizoagiza.”

Kwa haraka, Štefan alimjibu: “Samahani, pengine umenifananisha na mtu mwingine. Nataka tu filamu moja.”

Baada ya kurudi garini, Štefan alihisi hangeondoka bila karatasi hizo. Kwa hiyo, alivua koti na kofia yake na akajaribu kubadili sura yake, kisha akarudi dukani na kwenda moja kwa moja kwa yule mfanyakazi. “Nilikuwa hapa juma lililopita,” akamwambia, “na uliahidi kuniagizia karatasi za picha. Mlizipata?”

“Ndiyo tulizipata,” akajibu. “Lakini unajua nini, dakika chache zilizopita mwanamume anayefanana kabisa na wewe alikuwa hapa. Amini usiamini, alikuwa kama ndugu pacha wako!” Štefan alichukua haraka karatasi hizo na kuondoka, akimshukuru Yehova kwa kumsaidia kuzipata.

Katika miaka ya 1980 tulianza kutumia mashini za kutoa nakala na mashini ndogo za kuchapisha ili kutokeza vichapo vya Biblia katika vyumba vilivyokuwa chini ya ardhi na mahali pengine pa siri. Baada ya muda, idadi ya nakala za kila toleo la magazeti yetu na pia idadi ya vitabu na vijitabu ilikaribia na hata kuzidi idadi ya Mashahidi.

Ziara Zisizopendeza

Siku moja katika miaka ya 1960, niliamuriwa niripoti kwa idara ya kijeshi katika kampuni yetu. Wanaume watatu waliokuwa na mavazi ya raia waliniuliza hivi: “Umekuwa ukikutana na Mashahidi wa Yehova kwa muda gani? Wewe hukutana na nani?” Nilipokataa kuwapa majina, waliniambia kwamba watawasiliana nami baadaye. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kukutana na maofisa wa Usalama wa Kitaifa, yaani, polisi wa siri.

Muda mfupi baadaye, nilichukuliwa kazini na kupelekwa katika kituo cha polisi. Mtu fulani alinipa karatasi na kuniambia niandike majina ya Mashahidi wengine. Aliporudi baada ya saa nzima hivi, sikuwa nimeandika chochote, na nilimweleza siwezi kumpa majina yoyote. Juma lililofuata, jambo hilohilo lilitendeka. Lakini wakati huu nilipigwa, na nilipokuwa nikiondoka, nikapigwa mateke.

Baada ya hayo, sikusumbuliwa tena kwa mwaka mmoja. Kisha polisi wakatuma mtu anitembelee. Tulikuwa tumefungwa pamoja katika kambi ya mateso ya Nazi. Aliniambia hivi: “Tunapaswa kubadili mbinu za kushughulika nanyi. Tukimtupa Shahidi gerezani, anawafanya wanne wawe Mashahidi.” Serikali ilitaka angalau kudhibiti kazi yetu. Lakini niliazimia sitawapa habari zozote zitakazowawezesha kufanya hivyo.

Kwa miaka mingi, nilikuwa miongoni mwa Mashahidi waliohojiwa mara kwa mara na polisi wa siri. Nyakati nyingine walitutendea kama marafiki, lakini nyakati nyingine wangemtupa mmoja wetu gerezani. Nafurahi kwamba sikuwahi kufungwa, lakini nilihojiwa mara kwa mara na polisi hadi 1989, mwaka ambao serikali ya Kikomunisti ilianguka nchini Chekoslovakia.

Majuma machache baadaye, ofisa mwenye cheo wa Usalama wa Kitaifa kutoka Bratislava alinitembelea. Aliniomba msamaha na kusema: “Kama ningekuwa na uwezo, hamngehangaishwa.” Kisha akatoa mifuko miwili ya matunda ya mkebe kutoka katika gari lake na kunipa kama zawadi.

Yehova, Mnara Wenye Nguvu

Ingawa nilitumia miaka yangu 40 ya kwanza nikiwa Shahidi wa Yehova chini ya marufuku, nimekuwa na maisha yenye furaha na uradhi. Mambo yaliyotupata yalifanya tuwe na uhusiano wa karibu sana na waamini wenzetu. Tulithamini urafiki huo na tulitegemea uaminifu wa kila mmoja.

Machi (Mwezi wa 3) 2003, nilihuzunishwa sana na kifo cha mke wangu mpendwa, Oľga. Alikuwa mwandamani mshikamanifu muda wote wa ndoa yetu. Tulishirikiana kwa bidii katika huduma ya Kikristo miaka hiyo yote. Bado mimi ni mzee Mkristo katika kutaniko letu na ninawatafuta watu wanaostahili ambao ninaweza kuwafundisha kweli za Biblia. Jina Yehova nililosikia mara ya kwanza nikiwa katika handaki wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, limeendelea kuwa mnara wenye nguvu kwangu. *Methali 18:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 33 Ndugu Pavol Kovár alikufa Julai 14, 2007 (14/7/2007), makala hii ilipokuwa ikitayarishwa. Alikuwa na umri wa miaka 85.

[Picha katika ukurasa wa 12]

1942 nilipokuwa katika jeshi la Slovakia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Baadaye, nilifungwa huko Gusen (kwenye picha juu)

[Hisani]

© ČTK

[Picha katika ukurasa wa 12]

Baba yangu alitusomea Biblia kila Jumapili asubuhi

[Picha katika ukurasa wa 13]

Harusi yetu, 1946

[Picha katika ukurasa wa 15]

Pamoja na Oľga muda mfupi kabla hajafa