Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje ikiwa ndugu yangu amejiua?

Nifanyeje ikiwa ndugu yangu amejiua?

Vijana Huuliza

Nifanyeje ikiwa ndugu yangu amejiua?

Maisha ya Karen yalibadilika siku ambayo baba yake alimpasha habari hizo. Aliweza tu kusema hivi: “Sheila hayupo tena.” Karen na baba yake walikumbatiana huku wakijaribu kuelewa tendo hilo lisiloeleweka hata kidogo. Dadake Karen alikuwa amejiua. *

KIJANA anapokufa, mara nyingi wafariji wenye nia nzuri huwakazia fikira wazazi wake. Wao huwauliza ndugu na dada waliofiwa, “Baba na mama wanakabilianaje na hali hii?” lakini huenda wakasahau kuuliza, “Wewe unakabilianaje na hali hii?” Kwa sababu hiyo, ndugu na dada waliofiwa wameitwa waombolezaji wanaopuuzwa.

Uchunguzi umeonyesha kwamba kifo cha ndugu au dada huwaathiri sana watoto wachanga. “Pigo kubwa kama hilo huathiri sana afya, tabia, kazi za shule, hisia ya kujiheshimu, na ukuzi wa watoto waliobaki,” anaandika Dakt. P. Gill White katika kitabu chake Sibling Grief—Healing After the Death of a Sister or Brother.

Hata vijana wenye umri mkubwa huathirika pia. Karen, aliyetajwa hapo juu, alikuwa na umri wa miaka 22 dadake mdogo alipojiua. Hata hivyo, nyakati nyingine ilionekana ni kana kwamba analemewa na huzuni. Anasema: “Sisemi kwamba nilihuzunika zaidi kuliko wazazi wangu, lakini nafikiri sikuwa na uwezo wa kukabiliana na huzuni hiyo kama wao.”

Je, wewe pia umefiwa na ndugu au dada yako? Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kama mtunga-zaburi Daudi aliyeandika hivi: “Nimeingiwa na wasiwasi, nimeinama kupita kiasi; nimetembea huku na huku kwa huzuni mchana kutwa.” (Zaburi 38:6) Unaweza kukabilianaje na huzuni hiyo?

“Laiti Ninge . . . ”

Ndugu au dada yako anapojiua, unaweza kuhisi una hatia. Pengine utajiambia hivi: ‘Laiti ningeshughulikia mambo kwa njia tofauti, labda angekuwa hai bado.’ Huenda ikaonekana kwamba kuna uthibitisho wa jambo hilo. Chris, aliyekuwa na umri wa miaka 21 ndugu yake mwenye umri wa miaka 18 alipojiua, anaamini hilo. “Mimi ndiye nilikuwa mtu wa mwisho kuzungumza naye,” anasema, “kwa hiyo nilidhani kwamba nilipaswa kujua kuna tatizo fulani. Nilifikiri kwamba kama tu ningekuwa mwenye urafiki zaidi, huenda angenifunulia hisia zake.”

Chris alihisi vibaya hata zaidi kwa sababu hakuwa na uhusiano mzuri na ndugu yake. Anakumbuka hivi kwa uchungu mwingi: “Barua aliyoacha ilisema kwamba nilipaswa kuwa ndugu mzuri zaidi. Hata ingawa najua hakuwa mzima, maneno hayo hunichoma sana.” Mara nyingi hisia kama hizo za hatia huchochewa zaidi mtu anapokumbuka jinsi walivyofokeana kwa uchungu kabla ya ndugu yake kujiua. Dakt. White, aliyenukuliwa awali alimwambia hivi mwandishi wa Amkeni!: “Watoto wengi waliofiwa na ndugu au dada yao wameniambia kwamba wanaendelea kusumbuliwa na hisia za hatia kwa sababu ya ugomvi uliotukia miezi au hata miaka mingi mapema.”

Ikiwa unahisi kwamba una hatia kwa sababu ndugu au dada yako alijiua, jiulize, ‘Je, kuna mwanadamu yeyote anayeweza kudhibiti kabisa matendo ya mwanadamu mwingine?’ Karen anasema hivi: “Matatizo ambayo mtu huyo alikuwa akijaribu kuyaepuka na hatua mbaya aliyochukua ili kuyakomesha haikuwa katika uwezo wako.”

Vipi ikiwa ni vigumu kusahau maneno machungu ambayo ulimwambia ndugu au dada yako? Biblia inaweza kukusaidia uwe na maoni yanayofaa. Inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2; Zaburi 130:3) Kwa kweli, kukazia fikira pindi ambazo ulimzungumzia au kumtendea ndugu yako kwa ukali kutakufanya uhuzunike zaidi. Hata ingawa kumbukumbu hizo zinakufanya uhisi uchungu, ukweli wa mambo ni kwamba si wewe uliyefanya ajiue. *

Kukabiliana na Huzuni

Watu huonyesha huzuni kwa njia mbalimbali. Wengine hulia hadharani, na si vibaya kufanya hivyo. Biblia inasema kwamba Daudi ‘alilia kilio kikubwa sana’ mwana wake Amnoni alipokufa. (2 Samweli 13:36) Hata Yesu ‘alitokwa na machozi’ alipoona jinsi watu walivyohuzunishwa na kifo cha Lazaro, rafiki yake.—Yohana 11:33-35.

Kwa upande mwingine, watu wengine huomboleza baada ya muda kupita, hasa kifo kikitokea ghafula. Karen anakumbuka hivi: “Ni kana kwamba hisia zangu zilikufa ganzi. Kwa muda fulani, sikuendelea na shughuli zangu za kawaida.” Itikio hilo ni la kawaida ndugu au dada anapojiua. Dakt. White alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Kujiua kunashtua sana na unapaswa kukabiliana na mshtuko huo kabla ya kukabiliana na huzuni. Wataalamu fulani wanaowashughulikia watu waliofiwa huwahimiza walie na kuomboleza wakati ambapo hawako tayari kufanya hivyo. Bado wamekufa ganzi kwa mshtuko.”

Ndugu au dada yako anapokufa inachukua muda kukubali ukweli wa mambo na hilo linaeleweka ukifikiria yaliyotukia. “Familia yetu ni kama chombo kilichovunjika kisha kikaunganishwa tena kwa gundi,” anasema Chris. “Sasa inaonekana kwamba hatuwezi kuhimili hata matatizo madogo.” Ili kukusaidia kukabiliana na hali hiyo, jaribu kufanya mambo yafuatayo:

Andika orodha ya Maandiko yenye kufariji na uyasome angalau mara moja kila siku.—Zaburi 94:19.

Zungumza na rafiki mwenye huruma. Kuzungumzia mambo kunaweza kukusaidia ukabiliane na huzuni.—Methali 17:17.

Tafakari ahadi ya Biblia ya ufufuo.—Yohana 5:28, 29.

Kwa muda fulani, huenda kuandika hisia na mawazo yako kwenye kitabu kukakusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu huzuni yako. Mbona usitumie sanduku lililo hapa chini kufanya hivyo?

Uwe na hakika kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:20) Yeye anajua vizuri zaidi kuliko mwanadamu yeyote, mambo na hali ambazo huenda zilimfadhaisha ndugu au dada yako. Pia yeye anakujua wewe—vizuri zaidi kuliko unavyojijua. (Zaburi 139:1-3) Kwa hiyo, unaweza kuwa na hakika kwamba anaelewa hali unayopitia. Huzuni inapokulemea, kumbuka maneno ya Zaburi 55:22: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”

Faraja kwa Wanaoomboleza

Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na kifo cha mpendwa, ona broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 12 Inakuwa hivyo pia kifo kinaposababishwa na ugonjwa au aksidenti. Hata kama ulimpenda sana ndugu au dada yako, huwezi kuzuia “wakati na tukio lisilotazamiwa.”—Mhubiri 9:11.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unaweza kuzungumza na nani unapolemewa na hisia?

▪ Unaweza kumsaidiaje kijana anayeomboleza?

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Kuandika mawazo yako kunaweza kukusaidia sana kukabiliana na huzuni. Ukiwa na hilo akilini, kamilisha sentensi na ujibu maswali yafuatayo.

Ninakumbuka mambo haya matatu yenye kupendeza kumhusu ndugu yangu:

1 ․․․․․

2 ․․․․․

3 ․․․․․

Laiti ningemwambia ndugu au dada yangu mambo haya alipokuwa hai:

․․․․․

Ungemwambia nini ndugu mdogo wa yule aliyekufa ambaye anajilaumu kwa sababu ya kifo cha ndugu yake?

․․․․․

Ni Maandiko gani kati ya haya yanayokufariji sana, na kwa nini?

□ “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

□ “Hakudharau wala kuchoshwa na mateso ya mwenye kuteseka; naye hakumficha uso wake, naye alipomlilia amsaidie alisikia.”—Zaburi 22:24.

□ “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [ya Yesu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.