Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hisi Yako ya Kuonja

Hisi Yako ya Kuonja

Je, Ni Kazi ya Ubuni?

Hisi Yako ya Kuonja

▪ Mara tu unapotia chakula ukipendacho kinywani, hisi yako ya kuonja inaamshwa. Lakini hisi hiyo yenye kustaajabisha inafanyaje kazi?

Fikiria hili: Ulimi wako—kutia ndani sehemu nyingine za kinywa na koo lako—zina chembe za ngozi zinazoitwa vionjio. Vionjio vingi vinapatikana kwenye papillae zilizo kwenye sehemu ya juu ya ulimi. Kionjio kimoja kina chembe mia moja hivi. Kila chembe inaweza kutambua mojawapo ya ladha nne zilizopo—chachu, kali, tamu, au chungu. * Vikolezo viko katika kikundi tofauti. Vikolezo havichochei vionjio, bali huchochea chembe za kuhisi maumivu! Kwa vyovyote vile, vipokezi vya chembe za kuonja vimeunganishwa na mishipa ya hisi ambayo, inapochochewa na kemikali katika chakula, mara moja inapitisha habari hadi kwenye sehemu ya chini ya ubongo.

Hata hivyo, hisi ya kuonja haihusishi kinywa chako tu. Vipokezi milioni tano vya harufu vilivyo katika pua lako—ambavyo vinakuwezesha kunusa harufu 10,000 hivi tofauti-tofauti—hutimiza sehemu muhimu katika kuonja. Imekadiriwa kwamba karibu asilimia 75 ya kile tunachokiita ladha kwa kweli ni harufu.

Wanasayansi wametokeza pua bandia ambalo lina vipokezi vinavyoweza kunusa gesi za kemikali. Hata hivyo, mtaalamu wa mfumo wa neva John Kauer, aliyenukuliwa katika Research/Penn State, anasema hivi: “Kifaa chochote kinachoundwa na wanadamu kitakuwa duni sana kikilinganishwa na kiungo cha asili, ambacho kimebuniwa kwa njia ya ajabu na tata sana.”

Hakuna awezaye kukana kwamba hisi ya kuonja hufanya mlo ufurahishe hata zaidi. Hata hivyo, bado watafiti hawaelewi ni nini kinachowafanya watu wapendelee ladha fulani kuliko nyingine. “Wanasayansi wanaweza kuelewa utendaji wa msingi wa mwili wa mwanadamu,” lasema Science Daily, “lakini bado hisi yetu ya kuonja na ya kunusa ni fumbo.”

Una maoni gani? Je, hisi yako ya kuonja ilijitokeza yenyewe tu? Au ilibuniwa?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika miaka ya karibuni, wanasayansi fulani wameongeza umami katika orodha hiyo. Umami ni ladha ya chumvi za asidi amino. Mojawapo ya chumvi hizo ni kiungo kinachoitwa monosodium glutamate.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 26]

 

Picha ya ulimi

[Mchoro]

Papillae

[Hisani]

© Dr. John D. Cunningham/Visuals Unlimited