Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa Ziko Taabani

Ndoa Ziko Taabani

Ndoa Ziko Taabani

“Siwezi kuvumilia tena!” Je, umewahi kusikia watu wakisema hivyo kuhusu ndoa yao? Ikiwa umefunga ndoa, je, umewahi kuhisi hivyo?

MAELFU ya watu huanza maisha ya ndoa baada ya kusitawisha uhusiano wenye upendo wakati wa uchumba, ilhali wengine huoana haraka kwa sababu ya mahaba. Katika visa vyote viwili, wao hutarajia kuwa na furaha. Mshauri mmoja anasema hivi: “Lakini wanapokuja kuniona, wengi wao wanaamini kwamba hawatapata furaha tena. Tayari wametamaushwa na wenzi wao, ndoa, upendo, na nyakati nyingine hata maisha yenyewe.” Wengi wao wako pamoja tu kwa sababu wana cheti cha ndoa na wanaishi katika nyumba moja.

Ndoa nyingine huvunjika kwa sababu ya kuongezeka kwa mfadhaiko na mahangaiko. Kazi zenye kuchosha, kazi zinazofanywa kwa zamu, na kazi zinazofanywa kwa saa nyingi huwaacha hata watu wanaopendana sana wakiwa wamechoka kihisia. Upendo na heshima zinaweza kudhoofishwa polepole na matatizo ya kiuchumi, matatizo ya kulea watoto, kuhamia nyumba nyingine, kubadilisha kazi, na matatizo ya kiafya. Kwa ufupi, mabadiliko yanayotukia kadiri wakati unavyopita yanaweza kuleta mfadhaiko unaoweza kuwatenganisha wenzi wa ndoa.

Akina mama wengi hufanya kazi mbili—kazi ya kuajiriwa na kazi za nyumbani. Hilo linaweza kuwanyima wakati wa kufanya mambo mengine isipokuwa kazi yao ya kuajiriwa na kutunza watoto. Kwa sababu ya mfadhaiko na uchovu, wenzi wengi hawana wakati wa kuwa pamoja. Hivyo, wengi huhisi kana kwamba hawawezi kudhibiti maisha yao na hilo huwafanya wakate tamaa na kujitenga. Kwa nini ndoa nyingi zina matatizo mengi? Unaweza kufanya nini ili ndoa yako ifanikiwe na iwe yenye furaha?