Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?

Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?

Ni Matatizo Gani Yanayoweza Kutokea?

SI JAMBO linalopatana na akili kutarajia kwamba ndoa haitakuwa na matatizo. Hata wenzi wanaofaana kabisa hawatapatana katika kila jambo. Kwa hiyo, matatizo fulani hayaepukiki. Kama vile tu kutu iliyo chini ya rangi inavyoweza kuharibu chuma kilichopakwa rangi, mambo kadhaa yanaweza kuharibu ndoa. Ili tujue mambo tunayoweza kufanya ili kuboresha ndoa, acheni kwanza tuchunguze baadhi ya matatizo yanayoweza kutokea.

Nyakati Zenye Kufadhaisha Sana

Biblia ilitabiri kwamba watu wengi wanaoishi nyakati zetu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:2-4) Tabia hizo zinaweza kuongeza kutoelewana, kutowasiliana, na kusema bila kufikiri, jambo ambalo hufanyika kwa urahisi kwa sababu ya kutokuwa wakamilifu.

“Kwa waliofunga ndoa hiki si kipindi rahisi,” anasema mchunguzi mmoja. “Kwa upande mmoja . . . , tuna habari nyingi sana ambazo zinaweza kuimarisha ndoa zetu . . . Kwa upande mwingine, tunakabili uvutano mwingi wa kijamii na kiuchumi ambao unafanya iwe vigumu kuwa na ndoa nzuri.”

Matarajio Yasiyo Halisi

“Matarajio yasiyo halisi,” anasema mtaalamu mmoja wa ndoa, “ni moja kati ya visababishi vikubwa vya kutoridhika katika ndoa.” Watu wengi waliofunga ndoa hutamauka wanapogundua kwamba maisha ya ndoa si kama walivyoyatarajia na mwenzi wao ni tofauti na walivyofikiri atakuwa. Wanatamaushwa sana na kasoro za mwenzi wao ambazo hawakuwa wameziona au udhaifu ambao ni mkubwa kuliko walivyotarajia.

Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba ndoa inaweza kusababisha “uchungu na huzuni.” (1 Wakorintho 7:28, The New English Bible) Kwa nini? Sababu moja ni kwamba muda si muda uhusiano kati ya watu wawili wasio wakamilifu utafunua kasoro zao.

Kwa kuongezea, watu wengi huwa na matarajio yasiyo halisi kwamba ndoa yao itakuwa na furaha bila kufanya jitihada zozote. Kwa kuwa wamepofushwa na wazo la kwamba watakuwa na ndoa yenye furaha mara moja, wanapuuza madaraka na bidii inayohitajiwa kusitawisha ndoa yenye furaha. Wanapogundua kwamba ndoa si kama walivyokuwa wamedhania, huenda wakachanganyikiwa na kukata tamaa. Kwa kawaida, kadiri wanavyokuwa na matarajio mengi yasiyo halisi ndivyo wanavyokatishwa tamaa hata zaidi.

Tatizo la Kuwasiliana

Ni makosa gani ya kuwasiliana yanayoweza kuepukwa ili kuwa na uhusiano wa ndoa wenye nguvu? Wenzi fulani wa ndoa huwa na zoea la kusikia bila kusikiliza kwa makini na kuzungumza bila kuwasiliana. Badala ya mazungumzo machangamfu na yenye upendo, wanazungumzia tu mambo ya lazima. Huenda ugomvi usiokoma kuhusu kitu chochote ukachukua mahali pa mazungumzo ya waziwazi kutoka moyoni. Ugomvi hutokea kwa sababu ya kumwelewa yule mwingine vibaya na mwenzi mmoja anaposhambuliwa kwa maneno anaamua kunyamaza.

Kwa kusikitisha, watu wengi hawaoni tabia nzuri za mwenzi wao wa ndoa au wakiziona hawawaambii wenzi wao kwamba wanazithamini. Isitoshe, kwa kuwa siku hizi huenda wenzi wote wakafanya kazi ya kuajiriwa, wanawake wengi walioolewa hukasirika kwa sababu wanaachiwa kazi zote za nyumbani. Pia, wake wengi huhisi kwamba mahitaji yao ya kihisia yanapuuzwa.

Unaweza kufanya nini ili ndoa yako ifanikiwe? Fikiria mashauri yafuatayo kutoka katika Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Wenzi fulani wa ndoa husikia bila kusikiliza kwa makini na kuzungumza bila kuwasiliana

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Watu wengi huwa na matarajio yasiyo halisi kwamba ndoa yao itakuwa na furaha bila kufanya jitihada zozote