Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini Ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

Ninaweza Kufanya Nini Ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kufanya Nini Ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

Josh, mwenye umri wa miaka 16, amejilaza kitandani. Mama yake amesimama mlangoni. Anasema kwa ukali: “Joshua, amka! Kwani hujui leo ni siku ya mkutano?” Wazazi wa Josh ni Mashahidi wa Yehova, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni sehemu ya kawaida ya ibada yao. Hata hivyo, siku hizi Josh hana hamu ya kuhudhuria mikutano.

Analalamika: “Mama, kwani ni lazima niende?”

“Acha kulalamika na uvae nguo,” mama yake anamwambia. “Sitaki kuchelewa tena!” Kisha anageuka na kuanza kuondoka.

Kabla mama yake hajaenda mbali, Josh anasema: “Mama, nataka ujue kwamba hii ni dini yako, si lazima iwe yangu.” Anajua kwamba mama yake amesikia, kwa sababu alisimama kidogo. Kisha, bila kumjibu anaendelea kutembea.

Josh anajihisi mwenye hatia kwa sababu ya maneno aliyosema. Kwa kweli hataki kumuumiza mama yake. Kwa upande mwingine, hataki kuomba msamaha. Anaamua kumtii mama yake shingo upande.

Josh anashusha pumzi, anatoka kitandani na kuanza kuvaa. Kisha anajiambia: “Hivi karibuni nitafanya uamuzi wangu mwenyewe. Mimi si kama wengine katika Jumba la Ufalme. Pengine siwezi kuwa Mkristo!”

JE, UMEWAHI kuhisi kama Josh? Nyakati nyingine, je, inaonekana kwamba wengine wanafurahia utendaji wa Kikristo, huku wewe ukijihusisha katika utendaji huo kwa sababu tu huna la kufanya? Kwa mfano:

▪ Je, kujifunza Biblia ni kutimiza wajibu kama vile kufanya kazi ya shule?

▪ Je, unaogopa kuhubiri nyumba kwa nyumba?

▪ Je, mara nyingi unahisi umechoka unapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo?

Ikiwa jibu lako ni ndiyo kwa maswali kama hayo, usivunjike moyo. Ukifanya mabadiliko machache, unaweza kufurahia kumtumikia Mungu. Hebu tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

Tatizo la 1: Kujifunza Biblia

Kwa nini si rahisi? Huenda unahisi hupendi kujifunza. Ni vigumu kwako kuketi na kukaza fikira kwa muda mrefu. Isitoshe, una mambo mengi ya shule ya kujifunza.

Kwa nini ujifunze Biblia? Biblia imeongozwa na roho ya Mungu na pia ‘inafaa katika kufundishia ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha adili.’ (2 Timotheo 3:16, BHN) Kujifunza Biblia na kutafakari mambo unayosoma kunaweza kukufanya uelewe mambo kwa njia tofauti. Unapaswa kutambua kwamba huwezi kufanikiwa bila jitihada. Ukitaka kucheza mchezo fulani vizuri, unahitaji kujifunza sheria za mchezo huo na kufanya mazoezi. Ukitaka kuwa na afya nzuri, unahitaji kufanya mazoezi. Ukitaka kumfahamu Muumba wako, unahitaji kujifunza Neno la Mungu.

Vijana wenzako wanasema nini? “Nilipoenda shule ya upili, nilihitaji kufanya maamuzi muhimu. Vijana walikuwa wakifanya mambo mabaya ya aina zote na nilihitaji kufanya maamuzi fulani: ‘Je, ningependa kuwaiga? Je, kweli wazazi wangu wananifundisha kweli?’ Nilihitaji kujithibitishia.”—Tshedza.

“Sikuzote niliamini kwamba kile nilichojifunza ni kweli, lakini nilihitaji kujithibitishia. Nilihitaji kuifanya iwe dini yangu mwenyewe—badala ya kuwa dini ya familia.”—Nelisa.

Unachoweza kufanya. Panga funzo lako la kibinafsi kulingana na mapendezi na mahitaji yako. Chagua mwenyewe mambo utakayojifunza. Unaweza kuanzia wapi? Kwa nini usijifunze Biblia kwa undani na uchunguze mambo unayoamini, labda ukitumia kitabu kama vile Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

Mikakati. Unaweza kuanza kwa kutia alama mambo mawili au matatu hapa chini unayotaka kujifunza kwa undani kuhusu Biblia —au ukipenda, andika mambo mengine yanayokupendeza.

□ Je, kuna Mungu?

□ Ninaweza kuwaje na hakika kwamba waandikaji wa Biblia waliongozwa na roho ya Mungu?

□ Kwa nini niamini uumbaji badala ya mageuzi?

□ Ufalme wa Mungu ni nini, na ninaweza kuthibitishaje kwamba upo?

□ Ninaweza kuelezaje imani yangu kuhusu kile kinachotupata tunapokufa?

□ Kwa nini ninaweza kuwa na hakika kwamba kutakuwa na ufufuo?

□ Ninaweza kuitambuaje dini ya kweli?

□ ․․․․․

Tatizo la 2: Kuhubiri

Kwa nini si rahisi? Kuzungumza na wengine kuhusu Biblia—au kukutana na mwanafunzi mwenzako unapohubiri—kunaweza kuogopesha.

Kwa nini uhubiri? Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ (Mathayo 28:19, 20) Lakini kuna sababu nyingine za kufanya hivyo. Uchunguzi unadokeza kwamba katika maeneo fulani vijana wengi wanaamini Mungu na Biblia. Hata hivyo, vijana hao hawana tumaini hakika la wakati ujao. Kupitia kujifunza Biblia, una habari ambayo vijana wengi wa rika lako wanatafuta na wanahitaji hasa!

Vijana wenzako wanasema nini? “Mimi na rafiki yangu tulitayarisha utangulizi mbalimbali wenye matokeo, na tukajifunza jinsi ya kukabiliana na vizuia-mazungumzo na jinsi ya kufanya ziara za kurudia. Nilipojitahidi zaidi kufanya mambo hayo nilifurahia sana kuhubiri.”—Nelisa.

“Dada mmoja Mkristo amenisaidia sana! Amenizidi umri kwa miaka sita, naye huandamana nami shambani na mara nyingine hata huninunulia kiamsha-kinywa. Alinionyesha maandiko yenye kutia moyo yaliyonisaidia kurekebisha fikira zangu. Mfano wake mzuri umenichochea nitake kuwasaidia watu. Amenifanyia mengi kuliko yale ninayoweza kumfanyia!”—Shontay.

Unachoweza kufanya. Wazazi wako wakikuruhusu, tafuta mtu kutanikoni aliye na umri mkubwa kuliko wako mnayeweza kuhubiri pamoja. (Matendo 16:1-3) Biblia inasema hivi: “Chuma hunolewa kwa chuma. Ndivyo mtu anavyounoa uso wa mwingine.” (Methali 27:17) Kuna faida nyingi za kushirikiana na watu wenye umri mkubwa walio na uzoefu mwingi. “Kwa kweli, ni rahisi zaidi kushirikiana na watu wenye umri mkubwa,” anasema Alexis, mwenye umri wa miaka 19.

Mikakati. Mbali na wazazi wako, andika hapa chini jina la mtu katika kutaniko lenu anayeweza kukusaidia katika huduma.

․․․․․

Tatizo la 3: Kuhudhuria Mikutano ya Kikristo

Kwa nini si rahisi? Baada ya kushinda shuleni siku nzima, huenda ikawa vigumu sana kusikiliza hotuba zinazotegemea Biblia kwa saa moja au mbili zaidi.

Kwa nini uhudhurie mikutano? Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.”—Waebrania 10:24, 25.

Vijana wenzako wanasema nini? “Ni lazima utayarishe mikutano ya kutaniko. Mara nyingine unahitaji tu kuchochea hamu ya kujifunza. Ukijitayarisha, utafurahia mikutano kwa sababu unajua kinachozungumziwa, na hata unaweza kushiriki.”—Elda.

“Niligundua kwamba nilifurahia mikutano zaidi nilipotoa maelezo.”—Jessica.

Unachoweza kufanya. Tumia wakati kujitayarisha mapema, na ukiweza, toa maelezo. Hilo litakufanya uhisi unahusika katika mikutano hiyo.

Kwa mfano: Ni nini kinachofurahisha zaidi—kutazama michezo kwenye televisheni au kucheza uwanjani? Bila shaka, kucheza kunafurahisha zaidi kuliko kutazama tu. Mbona usifanye vivyo hivyo kuhusu mikutano ya Kikristo?

Mikakati. Andika katika nafasi iliyo hapa chini, siku unayoweza kupata dakika 30 kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya mkutano wa kutaniko.

․․․․․

Vijana wengi wamejionea ukweli wa Zaburi 34:8, ambayo inasema hivi: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” Je, inaridhisha tu kusikia kuhusu mlo mtamu? Je, si afadhali kula mlo huo wewe mwenyewe? Ndivyo ilivyo inapohusu kumwabudu Mungu. Onja na ujionee jinsi inavyoridhisha kushiriki katika utendaji wa kiroho. Biblia inasema kwamba mtu ambaye si msikiaji tu bali mtendaji wa kazi “atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini kijana anaweza kuona utendaji wa kiroho kuwa wenye kuchosha?

▪ Kati ya sehemu tatu zinazohusu ibada ambazo zimezungumziwa katika makala hii, ni ipi ambayo ungependa kufanyia kazi, na utafanyaje hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Ukitaka kuwa na afya nzuri, unahitaji kufanya mazoezi. Ukitaka kuwa na afya nzuri ya kiroho, unahitaji kujifunza Neno la Mungu