Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tumwabudu Mungu Kupitia Sanamu?

Je, Tumwabudu Mungu Kupitia Sanamu?

Maoni ya Biblia

Je, Tumwabudu Mungu Kupitia Sanamu?

“Nilifundishwa kwamba sanamu zitanifanya nihisi karibu na Mungu.”—Mack.

“Nyumba yetu ilijaa sanamu za kuchorwa. Tulifikiri hilo lilifanya nyumba yetu impendeze Mungu.”—Herta.

“Tulikuwa tukiinamia sanamu fulani. Hatukufikiria jinsi Mungu alivyohisi kuhusu jambo hilo.”—Sandra.

UNA maoni gani kuhusu maelezo hayo? Wengi wanaamini kwamba sanamu za kidini zinawasaidia kumwabudu Mungu. Je, maoni hayo ni sahihi? Swali muhimu hata zaidi ni, Mungu anahisije kuhusu jambo hilo? Hebu tuchunguze yale yanayosemwa katika Neno lake lililoandikwa, Biblia Takatifu.

Maoni ya Mungu Kuhusu Sanamu

Sanamu za kidini za kuchorwa na za kuchongwa ni mifano au ishara za kitu chochote kinachopewa ujitoaji au heshima. Zinatia ndani misalaba, vitu vilivyochongwa, picha, au umbo lililo kama kitu kilicho mbinguni au duniani. * Bendera pia zinaweza kuabudiwa.

Watu wametumia vitu kama hivyo katika ibada kwa maelfu ya miaka. Hivyo, mnamo 1513 K.W.K., alipolipatia taifa changa la Israeli zile Amri Kumi, Mungu alionyesha wazi maoni yake kuhusu sanamu za kidini. Alisema hivi: “Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala umbo lililo kama kitu chochote kilicho juu mbinguni wala kilicho chini duniani wala kilicho ndani ya maji chini ya dunia. Usiviinamie wala kushawishiwa kuvitumikia, kwa sababu mimi Yehova Mungu wako ni Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.”—Kutoka 20:4, 5.

Ona kwamba Mungu aliwakataza mambo mawili: Kwanza, watu wake hawakupaswa kujifanyia sanamu kwa ajili ya ibada, na pili, hawakupaswa ‘kuziinamia’ au kuzitumikia. Kwa nini Muumba wetu anawakataza watu wajifanyie sanamu? Sababu moja ya kutojifanyia sanamu zinazomwakilisha Mungu ni kwamba “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” Mwili wa Yehova si wa kimwili bali ni wa kiroho na anaishi katika makao ya kiroho. (Yohana 1:18; 4:24) Sababu ya kutofanya sanamu za kitu chochote ni kwamba Mungu anasisitiza apewe ‘ujitoaji kamili.’ Anasema hivi: “Sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.” (Isaya 42:8) Kwa sababu hiyo, ni kosa pia kufanya sanamu ili itusaidie katika ibada. Kiongozi Mwisraeli anayeitwa Haruni alipofanya hivyo, Yehova alichukizwa sana.—Kutoka 32:4-10.

Kwa Nini Tusiziinamie?

Biblia inasema hivi kuhusu sanamu: “Zina kinywa, lakini haziwezi kusema; zina macho, lakini haziwezi kuona; zina masikio, lakini haziwezi kusikia.” Kisha inaongeza onyo hili kali: “Wale wanaozifanya watakuwa kama hizo,” yaani, watakufa!—Zaburi 115:4-8.

Pia, kuabudu sanamu ni ukosefu wa haki. Jiulize, ‘Ningehisije ikiwa ningempa mtoto wangu zawadi ya bei ghali kisha aende na kumshukuru mtu asiyemjua au hata kitu kisicho na uhai?’ Huenda mfano huo ukakusaidia kuona jinsi Muumba na Mpaji-Uhai wetu anavyohisi wakati vitu vingine, kutia ndani sanamu zisizo na uhai, vinapopewa sifa na ibada anayostahili.—Ufunuo 4:11.

Pia, fikiria jinsi inavyodunisha kwa mwanadamu, aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu mwenyewe, kuabudu kitu kisicho na uhai! (Mwanzo 1:27) Nabii Isaya aliandika hivi kuhusu wengine waliofanya hivyo: “Wao huinamia kazi ya mikono ya mtu, kile ambacho vidole vya mtu vimetengeneza. Na mtu wa udongo huinama, na mwanadamu hushuka, nawe [Yehova Mungu] huwezi kuwasamehe.”—Isaya 2:8, 9.

Ibada ya uwongo inamchukiza Mungu hata zaidi kwa sababu kwa kweli ni ibada ya roho waovu ambao ni maadui wa Mungu. Waisraeli walipomwacha Yehova na kuanza kuabudu sanamu, “waliwatolea dhabihu roho waovu, wala si Mungu,” linasema andiko la Kumbukumbu la Torati 32:17.

Je, wafuasi wa mapema wa Yesu Kristo waliabudu sanamu au kuzitumia katika ibada? Hapana! Yohana, mtume wa Yesu aliandika hivi: “Watoto wadogo, jilindeni na sanamu.” (1 Yohana 5:21) Kitabu Early Church History to the Death of Constantine kinasema: “Huenda hakuna jambo lililowachukiza sana wanafunzi wa mapema kuliko ibada ya sanamu.”

Ibada Inayokubalika

Yesu alisema hivi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Ndiyo, Mungu anataka tumjue kibinafsi, yaani, tujue mambo anayopenda, anayochukia, viwango vyake, na kusudi lake kwa ajili yetu. (Yohana 17:3) Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu aliandika Biblia. (2 Timotheo 3:16) Pia, kwa kuwa Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu,” tunaweza kusali kwake wakati wowote, mahali popote, na bila msaada wa sanamu za kidini.—Matendo 17:27.

“Nilipoingia katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, sikuona sanamu yoyote,” anasema Sandra aliyenukuliwa mapema. “Mashahidi walitumia Biblia kunionyesha sifa za Mungu na matakwa yake. Kwa hiyo, nilijifunza kusali ili sali zangu zikubalike. Sasa ninahisi kwamba nina ujuzi sahihi wa Muumba na nina uhusiano wa karibu pamoja naye.” Ndiyo, Sandra alijifunza jinsi kweli za Biblia zinavyoburudisha na kumweka mtu huru. (Yohana 8:32) Unaweza kuhisi vivyo hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona makala “Je, Kweli Yesu Alikufa Msalabani?” katika toleo la Aprili 2006 la gazeti hili.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini tunapaswa kuepuka aina zote za sanamu katika ibada?—Zaburi 115:4-8; 1 Yohana 5:21.

▪ Mungu wa kweli anapaswa kuabudiwa jinsi gani?—Yohana 4:24.

▪ Unaweza kujifunzaje ukweli kumhusu Mungu, na unaweza kufaidikaje?—Yohana 8:32; 17:3.