Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makanisa Yalipofika Tahiti

Makanisa Yalipofika Tahiti

Makanisa Yalipofika Tahiti

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI TAHITI

MWISHONI mwa karne ya 18, watu barani Ulaya walianza kupendezwa na kueneza injili. Huko Uingereza, William Carey, ambaye baadaye alikuwa mmishonari, aliwachochea Waprotestanti kwa kuwahimiza waeneze injili katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa, kutia ndani Tahiti. Carey alichochewa na agizo la Yesu kwa wafuasi wake la kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. (Mathayo 28:19, 20) Mnamo 1802, katika kitabu chake kilichouzwa sana, Le Génie du christianisme, (Kipaji cha Ukristo) mwandishi Mfaransa, François-Auguste-René de Chateaubriand, aliwachochea Wakatoliki wawe wamishonari wenye bidii.

Punde si punde, mashirika ya wamishonari Wakatoliki na Waprotestanti yalianzishwa. Mnamo 1797, Shirika la Wamishonari la London lilituma wamishonari 29 huko Tahiti. Mwaka wa 1841, Wakatoliki wa kikundi kilichoitwa Makasisi wa Picpus waliwasili Tahiti, na miaka mitatu baadaye Kanisa la Mormon liliwatuma wamishonari pia. Hata hivyo muda si muda, wageni hao waliacha kuwafundisha watu Biblia na kujiingiza katika siasa na biashara. Kwa nini waliacha lengo lao?

Kuanzisha Urafiki na Ariʽi

Mwanzoni, watu hawakukubali mafundisho ya wamishonari Waprotestanti. Kulingana na mwandishi mmoja, “ujumbe wao ulikazia hasa moto wa mateso badala ya huruma na kupenda jirani.” Isitoshe, baada ya muda wahubiri hao walitambua kwamba hakuna mtu ambaye angethubutu kuwa Mkristo kabla ya ariʽi, au machifu, ambao pia walikuwa viongozi wa kidini kuwa Wakristo. Hivyo, wamishonari waliamua kuwakazia fikira viongozi hao.

Chifu mmoja hasa, Pomare wa Pili, aliwakaribisha wamishonari hao kwani aliona kuwa watamsaidia kiuchumi na kijeshi. Kwa upande mwingine, wao walimwona Pomare kuwa mtu atakayewasaidia kutimiza malengo yao. Isitoshe, tangu mwanzoni wamishonari walikuwa na uvutano fulani kwani walisaidia katika mawasiliano kati ya Watahiti na mabaharia ambao kwa kawaida walikuja kununua bidhaa.

Akiwa na matumaini kwamba wamishonari wangemsaidia katika malengo yake ya kisiasa na kupata silaha alizotaka, Pomare alipendezwa na ujumbe wao na katika mwaka wa 1811 akaomba kubatizwa. Mwaka uliofuata aliandika ombi lake la kutaka kubatizwa. Hata hivyo, kwa miaka minane ombi lake halikukubaliwa, kwani wamishonari waliona kuwa ni jambo la busara kuacha wakati upite ili athibitishe kwamba anaishi kupatana na viwango vya Biblia vya maadili.

Wakati huohuo, Pomare alifaulu kuwa mfalme asiyepingwa wa kisiwa cha Tahiti na visiwa jirani vinavyofanyiza Visiwa vya Society. Kwa mara nyingine, aliomba kubatizwa. Mwishowe katika 1819, wamishonari walikubali kumbatiza.

Hilo lilibadili mambo mara moja. Katika kipindi cha miaka mitano hivi, karibu wakaaji wote wa Visiwa vya Society, Visiwa vya Tuamotu magharibi, na nusu ya Visiwa vya Austral walidai kuwa Wakristo.

Katiba ya Pomare

Baada ya wakaaji wengi wa visiwa kukubali Ukristo, viwango, desturi, na sheria za zamani zilihitaji kubadilishwa. Pomare aliwaomba wamishonari wafanye hivyo. Kwa kweli, wamishonari walikuwa wametamani kwa muda mrefu sana kubadili desturi za kikabila na kupunguza mamlaka ya mfalme. Hivyo, wamishonari walikubali ombi la Pomare na wakatunga sheria mpya ambayo kulingana na kitabu kimoja, ilitia ndani “kanuni za msingi za katiba ya Uingereza, viwango vya Biblia, na desturi za mataifa ya Kikristo.” Baada ya kurekebishwa mara kadhaa, mfalme aliukubali uwe mfumo wa kwanza wa sheria iliyoandikwa ya Tahiti. Ilikuja kuitwa Katiba ya Pomare.

Visiwa jirani viliiga Katiba ya Pomare kwa kutunga mfumo kama huo wa sheria. Katiba hiyo ilikuwa na sheria ambayo ilihakikisha kwamba Sabato inafuatwa; ilitia ndani adhabu kwa makosa kama vile uzinzi, kuwa na wake wawili, wizi, na uasi; na ilitoa adhabu ya kifo kwa uuaji wa kukusudia, na uuaji wa watoto wadogo. Aina zote za burudani zenye ukosefu wa maadili katika ngono zilipigwa marufuku.

Kujiingiza Katika Siasa

Kitabu Where the Waves Fall, kinasema kwamba wamishonari Waprotestanti “walijiingiza sana katika siasa za kisiwa hicho. Mbali na kueneza injili walipanga mbinu za kivita, walikuwa washauri wa mambo ya kiuchumi, wanasiasa wenye hekima, na watungaji wa katiba na sheria.” Vivyo hivyo, wamishonari Wamormoni na Wakatoliki walisimamia mambo ya kijamii na kisiasa ya visiwa walikoishi. Akiwa kwenye kisiwa cha Tubuai ambacho ni mojawapo ya Visiwa vya Austral, mmishonari wa Mormon alidai hivi: “Serikali inaongozwa na kanisa. . . . Mimi ndiye waziri mkuu wa kisiwa hiki.” Katika Visiwa vya Gambier, Wakatoliki walikuwa na mamlaka kama hayo, kasisi mmoja alikuwa waziri wa serikali.

Mwanahistoria Claire Laux anasema kuwa badala ya kujihusisha na mambo ya kiroho pekee, wamishonari “waliamua kueneza injili kupitia siasa.” Waliona hiyo kuwa njia bora ya kupata matokeo. Kwa kufanya hivyo, wamishonari walitenda kinyume cha mwelekezo wa viongozi wao wa kidini. Lakini, hata kufikia sasa, dini na siasa bado zina uhusiano wa karibu katika visiwa vya Polinesia ya Ufaransa.

Fungu la Biashara Katika Dini

Kwa wamishonari fulani “kujiingiza katika siasa kulihusiana sana na mapendezi yao ya kibiashara,” anasema Profesa Niel Gunson wa Chuo Kikuu cha Canberra, Australia. Wamishonari walianza kufanya biashara ya kuuza, kukodisha, na hata kujenga meli za biashara. Wengine walikuwa na mashamba ya viazi, kahawa, miwa, na tumbaku.

Wamishonari walisitawi sana kibiashara hivi kwamba kwa miaka 25 walidhibiti biashara kati ya Australia na Tahiti hasa biashara ya nyama ya nguruwe na mafuta ya nazi. Hata hivyo, baadhi ya wamishonari hawakupendezwa na jambo hilo na wakaomba Shirika la Wamishonari la London liingilie kati. Wengine waliona kwamba biashara ilikuwa muhimu ili kufikia miradi ya kidini. Ingewezekanaje?

Tangu walipowasili, wamishonari walitumia ufundi wao na bidhaa walizotengeneza ili kuwavutia wakaaji wa visiwa hivyo. Wakiamini kwamba kuishi maisha ya kisasa kungewafurahisha wakaaji, wamishonari waliwahimiza wafanye kazi kwa bidii na kujipatia vitu vya kimwili, na hata waliwaambia kwamba kuwa na vitu vya kimwili ni baraka kutoka kwa Mungu.

Je, Walikuwa na Nia Nzuri?

Baadaye, mwanahistoria wa Shirika la Wamishonari la London aliandika kwamba watu wengi katika visiwa hivyo hawakuwa wakristo “kwa sababu walitaka kufanya yaliyo mema au kuwa na uhusiano pamoja na Mungu.” Gunson anasema kwamba Watahiti waligeuka kuwa Wakristo “kwa sababu tu walitaka kumpendeza Pomare wa Pili, kwa kufuata mazoea ya kidini (si imani) ya wamishonari Waingereza.”

Watahiti wengi walikuwa Wakristo kwa jina tu, na baada ya miaka michache walirudia upagani kupitia dini inayoitwa Mamaia. Ibada hiyo iliyohusisha ukosefu wa maadili ambayo pia ilifuatwa na mrithi wa kike wa kiti cha ufalme, ilichanganya sehemu za Ukristo na imani na mazoea ya dini za kitamaduni.

Kulikuwa na mabishano mengi kati ya vikundi vya Kiprotestanti vilivyotia ndani Waanglikana, Wakalvini, na Wamethodisti. Pia kulikuwa na uhasama kati ya Waprotestanti na Wakatoliki. Kitabu The Cambridge History of the Pacific Islanders kinasema hivi: “Wenyeji wa visiwa hivyo hawakuona tofauti zozote za kimafundisho kati ya dini hizo, na hawangeweza kuelewa kwa nini kulikuwa na uadui mkubwa kati ya watu waliodai kuwa ndugu.” Kwa mfano, wamishonari wawili Wakatoliki walipofika Tahiti, walirudishwa kwao mara moja kufuatia amri iliyotolewa na Mprotestanti aliyekuwa mmishonari maarufu. Kisa hicho kilitokeza uhasama kati ya Uingereza na Ufaransa ambao karibu utokeze vita. Hatimaye, Uingereza ilikubali dai la Ufaransa kwamba Tahiti iwe chini ya Ufaransa.

Matokeo Yenye Faida

Kwa upande mwingine, wamishonari kadhaa wa mapema waliwahimiza kwa bidii watu wajifunze kusoma na kuandika na walisaidia kuondoa uuaji wa watoto wachanga, ulaji wa watu, na kutoa watu dhabihu. Hata ingawa huenda wamishonari wengine walikuwa wakali sana, walijitahidi kuinua maadili ya wakaaji wa visiwa hivyo.

Zawadi moja ya pekee ambayo wamishonari waliwaachia Watahiti ni Biblia iliyotafsiriwa katika lugha yao. Isitoshe, kupitia Biblia hiyo waliwajulisha watu jina la Mungu ambalo bado linajulikana sana katika visiwa hivyo. *Zaburi 83:18.

[Maelezo ya Chini]

[Sanduku katika ukurasa wa 15]

“Ninyi Si Sehemu ya Ulimwengu”

Maneno hayo yaliyosemwa na Yesu Kristo ndiyo kanuni inayowaongoza wafuasi wake wa kweli. (Yohana 15:19) Kwa kweli, kanuni hiyo ni muhimu sana kwao hivi kwamba Yesu alisali hivi kwa Mungu: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Kwa sababu hiyo, Yesu hakujiingiza katika siasa wala kuitumia ili kupata wanafunzi. Alichukia kabisa ufuatiaji vitu vya kimwili ambavyo vinaonyesha roho ya ulimwengu. Badala yake, aliwatia watu moyo wafuatilie maisha rahisi yaliyokazia kutanguliza Ufalme. (Mathayo 6:22-24, 33, 34) Wafuasi wake wa kweli wanaiga mfano wake.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wamishonari wa kwanza wakikaribishwa, 1797

[Hisani]

The Granger Collection, New York

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mmishonari akiwa na Watahiti waliogeuzwa kuwa Wakristo, karibu 1845

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mfalme Pomare wa Pili

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tahiti na mji wake mkuu, Papeete

[Hisani]

Photo courtesy of Tahiti Tourisme

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 14]

Left: Photo by Henry Guttmann/Getty Images; right: Collection du Musée de Tahiti et de ses Îles, Punaauia, Tahiti