Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ujao wa Dunia Umo Mikononi mwa Nani?

Wakati Ujao wa Dunia Umo Mikononi mwa Nani?

Wakati Ujao wa Dunia Umo Mikononi mwa Nani?

“KUONGEZEKA kwa joto duniani kumetokeza mtihani mkubwa zaidi ambao wanadamu wamewahi kukabili,” likasema toleo la Oktoba 2007 la National Geographic. Gazeti hilo lilisema kwamba ili tutatue tatizo hilo kwa mafanikio, tunahitaji “kutenda haraka, kwa njia inayofaa, na kwa ukomavu ambao kwa kawaida sisi wanadamu hatuonyeshi.”

Je, wanadamu watatatua tatizo hilo kwa ukomavu? Kuna vipingamizi vingi: kutojali, pupa, ukosefu wa ujuzi, mapendezi ya vikundi mbalimbali, jitihada za kupata utajiri katika nchi zinazositawi, na mtazamo wa mamilioni wanaotaka kuishi maisha ya kawaida na hivyo kutumia nishati nyingi sana.

Nabii wa kale wa Mungu anachanganua uwezo wetu wa kutatua matatizo ya kimaadili, kijamii, na kiserikali. Aliandika hivi: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Historia yenye kusikitisha ya mwanadamu inathibitisha ukweli wa maneno hayo. Ingawa leo kuna maendeleo mengi ya sayansi na tekinolojia, tunakabili hatari ambazo hazikuwaziwa hapo awali. Basi tunawezaje kuwa na hakika kwamba hali zitakuwa nzuri wakati ujao?

Ni kweli kwamba mengi yamesemwa kuhusu kutatua tatizo la kubadilika kwa hali ya hewa na mambo mengine yenye kudhuru, lakini ni machache ambayo yamefanywa. Kwa mfano, mataifa yalitendaje mnamo 2007 Njia ya Kaskazini-Magharibi ilipofunguka na kutumiwa kwa mara ya kwanza? Makala katika gazeti New Scientist inajibu: “Waling’ang’ania bila aibu kujipatia maeneo ambayo wangeweza kuchimba mafuta na gesi zaidi.”

Karibu miaka 2,000 iliyopita Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba wanadamu wangefikia hatua ya ‘kuiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Ni wazi kwamba ulimwengu unahitaji kiongozi aliye na hekima na nguvu ili kutimiza mambo ambayo watu wanataka na raia ambao watajitiisha kwake. Je, kuna kiongozi wa kisiasa au mwanasayansi mnyoofu na mwenye uwezo anayeweza kutimiza hilo? Biblia inajibu: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.”—Zaburi 146:3.

Wakati Ujao wa Dunia Ni Salama!

Kuna Kiongozi mmoja tu anayeweza kutatua kwa mafanikio matatizo yanayoukabili ulimwengu. Biblia ilitabiri hivi kumhusu: “Roho ya Yehova [Mungu] itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova . . . Atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, . . . na kumuua mwovu kwa roho ya midomo yake.”—Isaya 11:2-5.

Huyo ni nani? Si mwingine ila ni Yesu Kristo ambaye kwa upendo alitoa uhai wake kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Sasa akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu, Yesu amepewa na Mungu mamlaka na nguvu za kutawala juu ya dunia.—Danieli 7:13, 14; Ufunuo 11:15.

Mojawapo ya mambo yanayomfanya Yesu astahili ni ujuzi wake mwingi kuhusu uumbaji wa Mungu ambao alipata kabla ya kuja duniani. Kwa kweli, miaka mingi sana iliyopita Mungu alipoumba ulimwengu, Yesu alikuwa ‘stadi wake wa kazi.’ (Methali 8:22-31) Hebu wazia hilo: Yesu ambaye alihusika katika uumbaji wa dunia na vitu vyote vilivyo hai, ataongoza katika kurekebisha hali iliyotokezwa na kutojali kwa wanadamu.

Ni nani watakaokuwa raia wa Kristo? Watakuwa watu ambao kwa kweli ni wapole na waadilifu wanaomjua Mungu wa kweli, Yehova, na wanamtii Yesu Kristo akiwa Mtawala. (Zaburi 37:11, 29; 2 Wathesalonike 1:7, 8) Yesu alisema kwamba “watairithi dunia,” ambayo itageuzwa kuwa paradiso.—Mathayo 5:5; Isaya 11:6-9; Luka 23:43.

Unaweza kufanya nini ili ushiriki katika kutimizwa kwa ahadi hizo za Biblia? Yesu mwenyewe anajibu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Ni kweli kwamba huenda ikaonekana dunia imo hatarini lakini hakuna shaka itaendelea kuwa makao ya wanadamu. Badala yake, wale wanaoendelea kuuvunjia heshima uumbaji wa Mungu na wanaokataa kumtii Yesu Kristo wamo hatarini. Hivyo basi, Mashahidi wa Yehova wanakutia moyo uendelee kupata ujuzi unaoongoza kwenye uzima wa milele.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

SAYANSI HAIWEZI KUTATUA MATATIZO YA DUNIA

Wakijua vema hatari zinazohusika, mamilioni ya watu wanadhuru akili na miili yao kwa kutumia dawa za kulevya, kutumia kileo vibaya, na kuvuta sigara. Kwa maoni yao, uhai si zawadi takatifu kutoka kwa Mungu. (Zaburi 36:9; 2 Wakorintho 7:1) Kwa kusikitisha, mtazamo kama huo kuelekea dunia umesababisha matatizo yake.

Basi suluhisho ni nini? Je, sayansi na elimu zinaweza kutatua matatizo hayo? Haziwezi. Tatizo la kiroho linahitaji suluhisho la kiroho. Biblia inakubaliana na wazo hilo. Hivyo, Biblia inaahidi kwamba wakati utafika ambapo wanadamu “hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote” kwa dunia kwa sababu “itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Chini ya utawala wa Kristo waadilifu watashiriki kazi ya kufanya dunia iwe paradiso