Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunapaswa Kutumia Majina ya Cheo?

Je, Tunapaswa Kutumia Majina ya Cheo?

Maoni ya Biblia

Je, Tunapaswa Kutumia Majina ya Cheo?

KATIKA shughuli zao za kila siku na walipohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, Wakristo wa karne ya kwanza walikutana maofisa mbalimbali wa serikali, wenye vyeo vya chini au vya juu. Wafuasi wa Yesu hawakutumia majina ya cheo kati yao ili kutofautisha hali au cheo chao maishani. Hata hivyo, wakati huo ilikuwa kawaida kuona watu wenye mamlaka wakiitwa kwa majina ya cheo. Maliki Mroma aliitwa “Mheshimiwa.”—Matendo 25:21.

Hivyo, walipokuwa mbele ya maofisa wa serikali, wanafunzi wa Yesu walikuwa na maoni gani kuhusu kutumia majina ya cheo? Nasi tunapaswa kuyaonaje?

Heshima, Si Kibali

Mtume Paulo aliwashauri waamini wenzake ‘wawape wote haki zao, yeye anayetaka heshima, heshima hiyo.’ (Waroma 13:7) Hilo lilitia ndani kuwaita maofisa kwa majina yao ya cheo. Siku hizi majina ya cheo kama vile Mheshimiwa hutumiwa tunapozungumza na watu wenye cheo katika serikali. Lakini huenda wengine wakauliza, ‘Ninawezaje kumwita mheshimiwa mtu ambaye ninashuku kwamba mwenendo wake si wa kuheshimika?’

Maofisa wengi wa serikali hufanya kazi yao vizuri, lakini si wote wanaoaminika. Hata hivyo, Biblia inatuhimiza tujitiishe kwa wafalme na magavana “kwa ajili ya Bwana.” (1 Petro 2:13, 14) Hivyo, kutambua kwamba Mungu amemruhusu ofisa awe na cheo cha mamlaka kutatuchochea tuwaheshimu.—Waroma 13:1.

Mwenendo wa ofisa si suala kuu katika muktadha huu. Mwenendo wake si sababu inayotufanya tumheshimu. Kumwita ofisa kwa jina lake la cheo hakumaanishi kwamba tunakubaliana na mwenendo wake. Hilo linaonyeshwa na kisa fulani katika maisha ya mtume Paulo.

Jinsi Paulo Alivyotumia Majina ya Cheo

Mtume Paulo alikamatwa huko Yerusalemu kwa sababu ya mashtaka bandia na kupelekwa kwa Feliksi, gavana wa Yudea. Akiwa ofisa wa serikali, Feliksi hakuwa na mwenendo mzuri. Mwanahistoria Mroma Tasito aliandika kwamba Feliksi “alifikiri angetenda maovu yoyote bila kuadhibiwa.” Alipendezwa zaidi na kupokea rushwa badala ya kutekeleza haki. Hata hivyo, kwa miaka miwili aliyokuwa gerezani, Paulo alimwonyesha heshima gavana huyo. Mara kwa mara walizungumza, Feliksi akitarajia kupata pesa kutoka kwa Paulo lakini hakupewa, huku Paulo akitumia nafasi hiyo kuhubiri.—Matendo 24:26.

Festo alipochukua mahali pa Feliksi, gavana huyo mpya alisikiliza kesi ya Paulo huko Kaisaria. Ili kupata kibali cha viongozi Wayahudi, Festo alipendekeza kwamba kesi ya Paulo isikizwe huko Yerusalemu. Lakini Paulo alijua kwamba kesi yake haingeamuliwa kwa haki huko, hivyo alitumia vizuri haki yake ya kuwa raia Mroma, aliposema: “Ninakata rufani kwa Kaisari!”—Matendo 25:11.

Festo hakuwa na hakika jinsi ya kumweleza Kaisari mashtaka dhidi ya Paulo, lakini alipata msaada wakati Mfalme Agripa wa Pili alipomtembelea na akasema kwamba alipendezwa kusikiza kesi hiyo. Siku iliyofuata, kwa fahari nyingi, makamanda wa kijeshi na wanaume waheshimiwa wa eneo hilo waliandamana na mfalme kwenye chumba cha baraza.—Matendo 25:13-23.

Alipoombwa azungumze, Paulo alitumia jina “Mfalme” katika utangulizi wake na akakubali kwamba Agripa alikuwa na ujuzi juu ya desturi na mabishano kati ya Wayahudi. (Matendo 26:2, 3) Wakati huo, ilijulikana wazi kwamba Agripa alikuwa na uhusiano haramu pamoja na dada yake. Kwa kweli, Paulo alijua sifa mbaya ambayo Agripa alikuwa nayo ya kuishi maisha mapotovu. Lakini bado alimpa heshima iliyomfaa mfalme.

Paulo alipokuwa akijitetea, Festo alimwambia: “Unashikwa na wazimu, Paulo!” Badala ya kukasirika, Paulo alijibu kwa utulivu na kumwita gavana huyo “Mtukufu.” (Matendo 26:24, 25) Paulo alimwonyesha heshima kwa sababu ya cheo chake. Hata hivyo, mifano hiyo inazusha swali hili, Je, heshima tunayowapa watu inapaswa kuwa na mipaka?

Heshima Yenye Mipaka

Mamlaka za serikali zina mipaka kama inavyoonyeshwa na Waroma 13:1, inayosema: “Mamlaka zilizopo zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.” Hivyo, heshima inayoonyeshwa wawakilishi wa serikali hizo ina mipaka. Yesu aliweka mipaka ya heshima inayopaswa kuonyeshwa watu wengine alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Msiitwe Rabi, kwa maana mwalimu wenu ni mmoja, lakini ninyi nyote ni ndugu. Zaidi ya hayo, msimwite mtu yeyote baba yenu duniani, kwa maana Baba yenu ni mmoja, Yule wa mbinguni. Wala msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—Mathayo 23:8-10.

Kwa hiyo, tofauti iliyopo kati ya majina ya cheo ya kidini na ya serikali inaweka mipaka kuhusu heshima tunayopaswa kuonyesha. Iwapo maofisa wa serikali watatumia majina ya cheo ya kidini, shauri la Paulo la kuonyesha heshima halitahusisha kutumia majina hayo ya cheo. Mtu anayefuata shauri la Kimaandiko atawaheshimu maofisa hao. Hata hivyo, kwa sababu ya dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, hatatumia majina ya cheo ya kidini kwa kuwa ana wajibu wa ‘kumlipa Mungu vitu vya Mungu.’—Mathayo 22:21.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Wafuasi wa Yesu walikuwa na maoni gani kuhusu wenye mamlaka serikalini?—Waroma 13:7.

▪ Je, mtume Paulo aliwaita maofisa wa serikali kwa majina yao ya cheo?—Matendo 25:11; 26:2, 25.

▪ Yesu alikataza matumizi ya majina gani ya cheo?—Mathayo 23:8-10.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Paulo alimwitaje Agripa?