Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Alinisaidia Kushinda Majaribu

Mungu Alinisaidia Kushinda Majaribu

Mungu Alinisaidia Kushinda Majaribu

Limesimuliwa na Vazir Asanov

Niliruka kutoka kitandani, nikaifunga Biblia kwenye kiuno, na kuvaa nguo haraka. Kabla ya kuruka kupitia dirisha, nilikusanya nguo kadhaa, nikaziweka kitandani, na kuzifunika kwa blanketi ili ionekane kana kwamba bado nilikuwa nimelala. Kisha nilikimbia kwenye Jumba la Ufalme, nikimwomba Mungu anitegemeze. Hilo lilifanyika mnamo 1991 nilipokuwa na umri wa miaka 14.

NILIZALIWA katika familia ya Kikurdi katika jiji lililo upande wa kusini wa nchi ambayo leo inaitwa Kazakhstan, wakati huo ilikuwa mojawapo ya jamhuri 15 za Muungano wa Sovieti. Wazazi wangu na watu wa ukoo walinifanya niamini kwamba ningeweza kuwa kiongozi wa kesho ambaye atawakomboa. Niliwachukia sana maadui wa Wakurdi hivi kwamba nilikuwa tayari kuua ili kuwakomboa watu wetu waliokuwa wakikandamizwa.

Mwishoni mwa miaka ya 1980, mimi, mama yangu, na ndugu yangu mdogo, tulianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, Baba alitukataza kushirikiana na Wakristo. Lakini bado niliendelea kujifunza. Haikuwa kawaida kwa Wakurdi kutotii kichwa cha familia. Nilimpenda baba yangu, lakini pia nilipenda kweli za Biblia nilizokuwa nikijifunza.

Upinzani Nyumbani na Shuleni

Wakati mmoja, mwalimu aliona nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi katika mkoba wangu wa shule na akawaeleza wazazi wangu. Kwa hasira, Baba alinigonga kwa nguvu sana mpaka nikatoka damu puani. “Je, bado unashirikiana na dini hiyo?” akauliza kwa sauti kubwa.

Baada ya hapo, Baba aliiambia familia kwamba mimi si mwanaye tena. Nilihuzunishwa sana na jambo hilo. Wakati huohuo, wengi kati ya wanafunzi wenzangu walianza kuniepuka na wengine wakanitukana hadharani. Walimu wangu walipunguza maksi zangu na mara kwa mara darasani walidhihaki imani yangu, wakijaribu kunifanya niache kumwamini Mungu.

Ingawa kulikuwa na upinzani mwingi hivyo, bado nilijaribu kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwahubiria wengine kuhusu imani yangu. Baada ya muda, Baba aligundua kwamba bado nilikuwa nikishirikiana na Mashahidi na kusoma Biblia. Jumapili (Siku ya Yenga) moja, nilianza kutafuta udhuru wa kutoka nyumbani ili nihudhurie mikutano. Mara moja, Baba aliniambia niende kitandani. Alisema hivi kwa uthabiti, “Sasa, kila Jumapili saa kama hizi unapaswa kuwa kitandani.” Alitisha kuniadhibu vikali ikiwa singetii, na nilikuwa na hakika kwamba angetimiza ahadi yake.

Huku nikilia, nilimwomba Yehova, Mungu wa kweli alainishe moyo wa Baba, lakini hakukuwa na mabadiliko yoyote. Nilikumbuka mateso ya Waisraeli nchini Misri. Matendo ya Baba yangu yalinikumbusha Farao, ambaye alikataa kuwaruhusu Waisraeli waende kumwabudu Yehova.—Kutoka 5:1, 2.

Kufanya Maamuzi

Jumapili moja niliamua kwenda mikutanoni. Moyo wangu ulipiga kwa wasiwasi nilipolala kitandani na kusali kimya-kimya kwa Yehova. Wazazi wangu walipokuja chumbani mwangu, nilijifanya nimelala. Baba alisema hivi kwa majivuno, “Ona jinsi nilivyo na mtoto mtiifu.” Alinibusu, na kutoka polepole. Niliendelea kusali kwa bidii.

Muda mfupi baada ya wazazi wangu kutoka chumbani, kama nilivyotaja mwanzoni, niliruka, nikachukua viatu vilivyokuwa chini ya kitanda, na kutoka kupitia dirisha. Saa mbili tulizokuwa mikutanoni zilipita haraka, na nilijiuliza ni nini kingetukia nitakaporudi nyumbani. Inapendeza kwamba ingawa Mama aliona nguo ndizo ziko kitandani na si mimi, hakumwambia Baba. Hata hivyo, alinionya kwamba hataendelea kumficha matendo kama hayo.

Mnamo 1992, niliwaambia wazazi wangu kwamba rafiki yangu alipaswa kuhudhuria karamu ya pekee na mimi pia nilialikwa. Kwa kweli, tukio hilo la pekee nililotaka kuhudhuria lilikuwa kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika jiji la Taraz, ambalo liko kilomita 100 hivi kutoka nyumbani huko Karatau. Nilipaswa kubatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova. Nilimwuliza Mama anipe ndoo iliyojaa mbegu za alizeti kutoka ghalani. Nilizikaanga na kuziuza sokoni. Nilitumia pesa nilizopata kwenda kwenye kusanyiko.

Niliporudi, Baba aliuliza ikiwa mimi na rafiki yangu tulikuwa tumejifurahisha. Nilimhakikishia kwamba tulikuwa tumefurahia kila kitu. Nilihisi utegemezo wa Yehova kwa kuwa Baba hakuuliza maswali zaidi. Nilipenda sana maneno ya Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

Hali Yangu ya Kiroho Yazorota

Upinzani wa Baba haukunizuia nibatizwe. Nilipoendelea kushirikiana na Mashahidi, Baba alinichapa sana, mbele ya watu na pia faraghani. Karibu kila siku niliaibishwa na kushinikizwa nikane imani yangu, na nililia mara nyingi. Wakati huo Kazakhstan ilikuwa ikikaribia kupata uhuru kutoka kwa Muungano wa Sovieti na wazazi wangu na watu wa ukoo walijaribu kunishawishi nifuatie miradi itakayonisaidia kuwa mwanasiasa. Walifikiri nilikuwa nikipoteza nafasi nzuri.

Ndugu yangu mkubwa alikuwa amefaulu katika michezo, na Baba alinitia moyo mara nyingi nifuate mfano wake. Kufikia mwisho wa mwaka wa 1994, mimi pia nilianza kujihusisha katika michezo. Kwa kuwa nilikuwa na vipawa nilianza kushinda tuzo mbalimbali na kusifiwa kwa ajili ya ustadi wangu katika mpira na mchezo wa sarakasi. Pia nilienda chuo kujifunza sheria ili niweze kutetea masilahi ya Wakurdi. Hata nilianza kupendezwa na siasa na nikafikiria kuanzisha chama cha vijana wa Kikurdi. Tangu wakati huo Baba akaanza kunisifu.

“Baba, Umeshinda”

Nilikuwa nimedhoofika kiroho na nilikuwa nimeacha kusoma Biblia na kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilijifariji kwa kujiambia kwamba nitamtumikia Yehova nitakapokuwa mtu mzima. Siku moja Baba aliniuliza kama ninashirikiana na Mashahidi wa Yehova. “Hapana Baba, umeshinda,” nikamjibu. “Sasa umefurahi?” Aliposikia hivyo, Baba alifurahi sana. Alisema hivi kwa shangwe, “Sasa wewe ni mwanangu!”

Kwa miaka miwili sikuhudhuria mikutano hata ingawa nyakati nyingine nilitaka kwenda. Lakini sikuhudhuria kwa sababu ya aibu. Nilifikiri kwamba washiriki wa kutaniko hawangeelewa hali yangu.

Wakati huohuo niliamini kwamba hakuna jambo bora zaidi kuliko kumtumikia Yehova. Mara nyingi nilijiambia hivi, ‘Kwa kweli, bado ninampenda Yehova!’ Kisha Baba akaanza kunihimiza niende chuo kikuu. Nilikubali na hata nikamwahidi kwamba ningehitimu kwa shahada za juu. Hata hivyo, moyoni mwangu nilitumaini kwamba ningewapata Mashahidi nitakapofika Almaty, jiji kubwa la kisasa kusini mwa Kazakhstan ambako chuo hicho kinapatikana.

Hali Zabadilika na Kuwa Nzuri

Muda mfupi baada ya kuanza masomo chuoni, nilikutana na Mashahidi wawili wakihubiri kwenye mtaa fulani huko Almaty. Walinikaribia na kuniuliza, “Unafikiri ni nani anayeutawala ulimwengu?”

Niliwajibu, “Ni Shetani Ibilisi, adui wa Yehova na wanadamu wote.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Niliwaeleza kwamba mimi ni Shahidi aliyebatizwa lakini asiyetenda.

Kuelekea mwishoni mwa 1996, nilianza kujifunza tena Biblia na Mashahidi. Baada ya kujifunza kwa muda, tamaa yangu ya kumtumikia Yehova ilirudi na nikaanza kushiriki katika utendaji wote wa Mashahidi huko Almaty. Katika Septemba (Mwezi wa 9) 1997, nilianza kutumika nikiwa painia, au mhudumu wa wakati wote.

Mwaka mmoja baadaye, Baba alikuja kunitembelea. Nilimkimbilia na tukakumbatiana. Aliniomba msamaha kwa jinsi alivyonitendea miaka hiyo yote. Alisema kwamba alikuwa amenielewa vibaya na alikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu imani yangu. “Ninakupenda sana Baba,” nikamwambia.

Nilifurahi kama nini Baba alipokubali vichapo vya Biblia na akaomba apewe Biblia akisema kwamba alitaka kuisoma yote! Mwaka mmoja baadaye, alinitembelea tena akiwa na Mama. Katika Jumba la Ufalme watu kutoka nchi mbalimbali waliwasalimu kwa uchangamfu na kujitambulisha. Hilo lilimpendeza sana Baba, naye akaanza kusoma vichapo vya Mashahidi kwa hamu kubwa.

Baraka Nyingi

Mnamo Septemba 2001, nilimwoa msichana mrembo sana Mrusi anayeitwa Yelena. Alibatizwa mwaka wa 1997 na akaanza kufanya upainia mnamo Mei (Mwezi wa 5) 2003. Tulifurahi sana tulipojua kwamba wazazi wangu walikuwa wameanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi na walikuwa wakifanya maendeleo ya kiroho. Kwa kweli, sikuamini hadi Baba mwenyewe aliponiambia. Alinipigia simu na kuniambia kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli!

Ninafurahi sana kwamba huku Almaty nimepata nafasi ya kujifunza Biblia na watu kutoka maeneo mengi, kutia ndani China, Iran, Pakistan, Siria, na Uturuki. Hivi karibuni, kiongozi mmoja wa kidini anayetoka Iran aliniomba nijifunze Biblia pamoja naye katika lugha yake ya mama, Kiajemi. Jenerali mmoja kutoka Afghanistan alifurahia sana aliyojifunza kumhusu Yehova. Pia nimefurahi kujifunza na mtu kutoka Siria katika lugha yangu ya mama, Kikurdi, vilevile nimejifunza na watu katika Kikazakh na Kirusi, lugha nyingine nilizotumia nilipokuwa mtoto.

Sasa, mimi na Yelena, tunaendelea kutumika katika kutaniko la Kikazakh ambalo ni mojawapo ya makutaniko zaidi ya 35 ya Mashahidi wa Yehova huko Almaty. Mwaka jana, mimi na Yelena tulipata pendeleo la kutumika kwa muda katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyojengwa hivi karibuni karibu na Almaty.

Wakati fulani nilifundishwa kuwachukia watu, lakini Yehova amenifundisha kuwapenda. Ninasadiki kwamba hatupaswi kukubali kushawishiwa kuacha kumpendeza Yehova, hata unaposhinikizwa na watu wa ukoo na marafiki wenye nia nzuri. (Wagalatia 6:9) Sasa ninafurahi kwamba mimi na mke wangu tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Mama alinionya kwamba hataendelea kumficha Baba matendo kama hayo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Jumba la Ufalme huko Karatau, nilikohudhuria nikiwa kijana

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazazi wangu ambao sasa wanapendezwa na kazi yetu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mimi na Yelena kwenye siku yetu ya harusi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Yelena, kwenye ofisi mpya ya tawi karibu na Almaty