Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafu Wataishi Tena!

Wafu Wataishi Tena!

Wafu Wataishi Tena!

KATIKA sinema miaka kadhaa iliyopita, kijana mmoja alionyeshwa akisimama kando ya kaburi la mpendwa wake. “Sikuzote Mama alisema kufa ni sehemu ya maisha,” akasema. Kisha kamera ilipoelekezwa kwenye kaburi, akaongezea: “Afadhali haingekuwa hivyo.”

Maneno kama hayo huonyesha hisia za mabilioni ya watu ambao wamewapoteza wapendwa wao katika kifo. Ni adui mbaya kama nini! Hata hivyo, Mungu anaahidi hivi: “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26) Lakini kwa nini tunakufa licha ya kwamba tuna uwezo wa kuishi milele? Kifo kitaangamizwaje?

Kwa Nini Tunazeeka na Kufa?

Biblia inasema hivi kumhusu Yehova Mungu, Muumba wetu: “Kazi zake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 83:18) Mtu wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mkamilifu na alikuwa na uwezo wa kuishi milele katika Edeni, iliyokuwa Paradiso duniani ambapo Mungu aliwaweka. (Mwanzo 2:7-9) Kwa nini Adamu alipoteza makao yake ya Paradiso, akazeeka, na kufa?

Kwa ufupi: Adamu hakutii sheria ya kutokula tunda kutoka kwa mti fulani. Mungu alikuwa amemwambia Adamu waziwazi kuhusu adhabu ya kufanya hivyo, aliposema: “Utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Adamu alijiunga na mke wake, Hawa, kutotii amri hiyo, hivyo Mungu akawafukuza kutoka Edeni. Kuna sababu muhimu kwa nini Mungu alitenda hivyo. Biblia inasema: “Ili [Adamu] asije akanyoosha mkono wake achukue matunda kutoka pia katika mti wa uzima [ulio bustanini] na kula na kuishi [milele].”—Mwanzo 3:1-6, 22.

Adamu na Hawa walikufa kwa sababu ya kutotii, lakini kwa nini wazao wao huzeeka na kufa? Kwa sababu walirithi dhambi kutoka kwa Adamu, na dhambi imetokeza kutokamilika na kifo kwa wazao wao wote. Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Inawezekana Kuishi Tena

Kama tulivyosoma awali, ‘kifo kitaangamizwa,’ naam, kitaondolewa milele! (1 Wakorintho 15:26) Kitaondolewaje? Biblia inaeleza hilo ikisema: “Kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Waroma 5:18) Ni nini linalotuwezesha tuwe na msimamo wa uadilifu mbele ya Mungu na kufurahia uzima wa milele?

Ni maandalizi ya kuondoa kabisa dhambi ambayo wanadamu wote walirithi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Biblia inaeleza: “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Yesu alisema hivi kuhusu maandalizi hayo ya kuwatangaza watu kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Fikiri kuhusu kina cha upendo wa Mungu kwa ajili yetu, pia ule wa Mwana wake, Yesu Kristo, ambaye aliteseka sana kwa ajili yetu. Mtume Paulo aliandika: ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Wagalatia 2:20) Hata hivyo, kwa nini Yesu ndiye mwanadamu pekee ambaye ‘angetoa nafsi yake kuwa fidia’ kwa ajili yetu na hivyo kutuokoa kutokana na matokeo ya dhambi yanayosababisha kifo?—Mathayo 20:28.

Yesu ndiye mtu pekee ambaye angeweza kutoa nafsi yake kuwa fidia kwa sababu yeye ndiye mwanadamu pekee ambaye hakurithi dhambi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa nini? Kwa sababu uhai wa Yesu ulihamishwa kimuujiza kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, aliyekuwa bikira. Kwa hiyo, kama malaika alivyomwambia Maria, mwana wake alikuwa ‘mtakatifu, Mwana wa Mungu.’ (Luka 1:34, 35) Hiyo ndiyo sababu Yesu anaitwa “Adamu wa mwisho” na ndiyo sababu hakurithi dhambi kutoka kwa “mtu wa kwanza Adamu.” (1 Wakorintho 15:45) Akiwa mwanadamu asiye na dhambi, Yesu angeweza kujitoa akiwa “fidia inayolingana,” yaani, uhai wake ulilingana na ule wa mtu wa kwanza aliyekuwa mkamilifu na asiye na dhambi.—1 Timotheo 2:6.

Kupitia maandalizi ya fidia, Mungu ametuwezesha tupate kile ambacho Adamu wa kwanza alipoteza, yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, ili wapokee baraka hiyo, wanadamu wengi watahitaji kuishi tena. Hilo ni taraja zuri kama nini! Lakini je, kweli jambo hilo linawezekana?

Msingi wa Kuamini

Je, ni vigumu sana kuamini kwamba Yehova Mungu ambaye aliumba uhai ana uwezo wa kumuumba upya mtu aliyeishi hapo awali? Hebu fikiria uwezo wa kutunga mimba ambao Mungu alimpa mwanamke wa kwanza. “Adamu akalala na Hawa,” na miezi tisa hivi baadaye, wakazaa mtoto aliyefanana kabisa nao. (Mwanzo 4:1) Jambo lililotendeka katika tumbo la uzazi la Hawa ili kuumba sehemu zote za mtoto huyo na kuziunganisha bado huonwa kuwa muujiza ambao wanadamu hawawezi kuuelewa!—Zaburi 139:13-16.

Watu hawaoni kuzaliwa kwa mtoto kuwa muujiza kwa sababu jambo hilo hutendeka mara nyingi sana kila siku. Hata hivyo, watu wengi wanaona kwamba haiwezekani kumfanya mtu aliyeishi hapo awali aishi tena. Yesu alipowaambia watu waliokuwa wakiomboleza kifo cha msichana mdogo waache kulia, ‘walianza kumcheka kwa dharau’ kwa sababu walijua kwamba alikuwa amekufa. Lakini Yesu alimwambia hivi msichana aliyekufa: “‘Simama!’ Na mara yule mwanamwali akasimama akaanza kutembea.” Tunaambiwa hivi: “Mara moja [wale waliokuwapo] wakawa na shangwe kubwa.”—Marko 5:39-43; Luka 8:51-56.

Yesu alipoomba kaburi la Lazaro rafiki yake lifunguliwe, Martha dada ya Lazaro alipinga jambo hilo akisema: “Kufikia sasa lazima awe ananuka, kwa maana ni siku nne.” Hata hivyo, kulikuwa na shangwe kubwa kama nini Yesu alipomfufua Lazaro! (Yohana 11:38-44) Wengi walisikia kuhusu miujiza ya Yesu. Yohana mbatizaji alipokuwa gerezani, wanafunzi wa Yohana walimweleza kuhusu utendaji wa Yesu wakisema: “Wafu wanafufuliwa.”—Luka 7:22.

Kuishi Tena Kupitia Ufufuo

Kwa nini Yesu alifanya miujiza ya aina hiyo, ingawa watu aliowafufua walikuwa wagonjwa na kufa tena? Kwa sababu hilo lilithibitisha kwamba kile ambacho Adamu wa kwanza alipoteza, yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani, kinaweza kurudishwa na kitarudishwa. Ufufuo ambao Yesu alifanya ulionyesha jinsi ambavyo hatimaye mamilioni ya wanadamu “wataimiliki dunia” na “watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.

Inafurahisha kwamba tunaweza kuwa miongoni mwa wale walio na taraja la kuishi milele ikiwa tutajizoeza “ujitoaji-kimungu.” Biblia inasema kwamba ujitoaji kama huo, “una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” ‘Uzima huo utakaokuja’ pia huitwa “uhai ambao ni uhai wa kweli” na “uzima ulio wa kweli.”1 Timotheo 4:8; 6:19; Biblia Habari Njema.

Acheni tuchunguze jinsi uzima huo wa kweli, uzima utakaokuja katika ulimwengu mpya wenye uadilifu utakavyokuwa.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Wakawa na shangwe kubwa”