Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ana Utu Gani?

Mungu Ana Utu Gani?

Maoni ya Biblia

Mungu Ana Utu Gani?

“MUNGU ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli,” inaeleza Biblia. Maneno hayo yanatufunulia ukweli wa msingi kuhusu umbo, au utu wa Mungu—yeye ni roho! (Yohana 4:19-24) Hata hivyo, Biblia inamfafanua kuwa mtu. Jina lake ni Yehova.—Zaburi 83:18.

Wasomaji fulani wa Biblia wamechanganyikiwa kuhusu utu wa Mungu. Kwa kuwa Mungu ana mwili wa roho usioweza kuonekana, kwa nini kuna maandiko mengi katika Biblia yanayosema kwamba Mungu ana macho, masikio, pua, moyo, mikono, vidole, na miguu? * Huenda watu fulani wakakata kauli kwamba Mungu ana umbo kama la mwanadamu kwa kuwa Biblia inasema kwamba mtu aliumbwa kwa mfano wake. Kuchunguza Biblia kwa makini zaidi kunaweza kusaidia kufanya jambo hilo lieleweke.—Mwanzo 1:26.

Kwa Nini Anafafanuliwa kwa Sifa za Kibinadamu?

Ili kuwasaidia wanadamu waelewe utu wa Mungu, waandikaji wa Biblia waliongozwa na roho kutumia sifa za kibinadamu kumfafanua Mweza-Yote. Maneno yaliyotumiwa yanaonyesha jinsi ambavyo lugha ya wanadamu imepungukiwa inapomfafanua Mungu wa kweli, Yehova. Kusudi lilikuwa kutaja mambo muhimu kuhusu umbo na utu wa Mungu katika njia ambayo wanadamu wanaweza kuelewa. Hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kuyaona maneno hayo kuwa halisi kwa kuwa hatufanyi hivyo na maneno mengine katika Biblia yanayomfafanua Mungu kama vile “Mwamba,” “jua,” au “ngao.”—Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 84:11.

Vivyo hivyo, ili kuonyesha wazo la kwamba mwanadamu kwa kiasi fulani ana sifa ambazo Yehova anaonyesha kikamili, Biblia inasema kwamba mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu. Ni wazi kwamba hilo halimaanishi eti wanadamu ni roho au kwamba Mungu ana umbo la kibinadamu.

Je, Mungu Ni wa Kiume au wa Kike?

Kama vile tu kumpa Mungu sifa za kibinadamu hakupaswi kuonwa kihalisi, kumtaja Mungu kuwa wa kiume hakupaswi kuonwa kuwa halisi. Viumbe wa kimwili ndio hutofautishwa kuwa wa kiume au wa kike, na hilo ni jambo lingine linaloonyesha kwamba lugha ya wanadamu imepungukiwa inapomfafanua Mungu Mweza-Yote, Yehova.

Biblia inapotumia neno “Baba” inatusaidia kuelewa kwamba Muumba wetu anaweza kulinganishwa na baba wa kibinadamu mwenye upendo, anayetunza na kujali familia yake. (Mathayo 6:9) Hiyo haimaanishi kwamba tunapaswa kumwona Mungu au hata viumbe wengine wa roho mbinguni kuwa wa kiume au wa kike. Jinsia si sehemu ya umbo lao. Kwa kupendeza, Biblia inaonyesha kwamba wale wanaoitwa kuwa warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wake hawatarajii kubaki na jinsia yao ya kibinadamu watakapotukuzwa kuwa wana wa roho wa Mungu. Mtume Paulo aliwakumbusha kwamba “hakuna mwanamume wala mwanamke” wanapokuwa wana wa roho wa Mungu waliotukuzwa. Pia wanafafanuliwa kwa njia ya mfano kuwa “bibi-arusi” wa Mwana-kondoo, Yesu Kristo. Yote hayo yanaonyesha kwamba sifa za kibinadamu zinapotumiwa kumfafanua Mungu, Mwana wake wa pekee Yesu, na viumbe wengine wa roho, hazipaswi kuonwa kuwa halisi.—Wagalatia 3:26, 28; Ufunuo 21:9; 1 Yohana 3:1, 2.

Wakielewa vizuri jukumu la kiume, waandikaji wa Biblia walitumia utu wa kiume kumfafanua Mungu. Waandikaji hao walijua kwamba mwanamume anayetenda kupatana na kanuni za Mungu angekuwa mfano unaofaa wa upendo kama wa baba unaoonyeshwa na Yehova kuelekea watoto wake wa kibinadamu.—Malaki 3:17; Mathayo 5:45; Luka 11:11-13.

Sifa Kuu ya Mungu

Ingawa yeye ni roho, Mwenye Enzi Kuu anajali, anajifafanua, na anawasiliana nasi. Utu wake wa roho si jambo linaloweza kuwazuia wanadamu wenye mioyo inayofaa ambao wanataka kujua na kuthamini upendo wake, nguvu zake, hekima yake, na haki yake, sifa ambazo zinafafanua utu wake na zinaonekana wazi katika uumbaji.—Waroma 1:19-21.

Hata hivyo, utu wa Mungu unaweza kujumlishwa na sifa yake kuu, upendo. Sifa hiyo yake ya upendo inatokeza sana hivi kwamba anasemwa kuwa upendo. (1 Yohana 4:8) Sifa hiyo hutia ndani sehemu nyingine za utu wake kama vile, rehema, kusamehe, na ustahimilivu. (Kutoka 34:6; Zaburi 103:8-14; Isaya 55:7; Waroma 5:8) Kwa kweli, Yehova ni Mungu wa upendo ambaye anatualika tumkaribie.—Yohana 4:23.

[Maelezo ya Chini]

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Mungu anaitwaje?—Zaburi 83:18.

▪ Sifa za Mungu zinaweza kuonekana wapi?—Waroma 1:19-21.

▪ Sifa kuu ya Mungu ni gani?—1 Yohana 4:8.