Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kwa sasa, kituo rasmi cha Mashahidi wa Yehova kwenye Intaneti (www.watchtower.org) kinatoa habari katika lugha 314. Mwaka jana, kituo hicho kilitembelewa zaidi ya mara milioni 22, yaani, kwa wastani kila siku kilitembelewa mara zaidi ya 60,000.

“Mojawapo ya matatizo makubwa zaidi ulimwenguni leo ni kuhakikisha kwamba kila mtu anapata maji mengi na yaliyo safi. . . . Mara nyingi, mahali kuna uhitaji mkubwa wa maji utapata bunduki.”—BAN KI-MOON, KATIBU MKUU WA UM.

Furaha na Afya

Kwa muda mrefu imefikiriwa kwamba watu wenye furaha na mtazamo mzuri wana afya nzuri kuliko watu walio na mfadhaiko, wakali, au walio na mtazamo mbaya. Katika uchunguzi mmoja wa karibuni, wachunguzi walisema kwamba watu “wachangamfu” wana viwango vidogo vya cortisol, homoni ya mfadhaiko inayochangia magonjwa mbalimbali inapoongezeka sana kwa muda mrefu. Watu kama hao wana viwango vidogo zaidi vya “protini mbili zinazochangia mwasho kwenye viungo mbalimbali.” Kulingana Dakt. Andrew Steptoe wa University College huko London, “mtazamo wetu hautegemei tu hali tuliyorithi bali pia uhusiano wetu na wengine na kuwa na kusudi maishani.”

Kuutazama Mwezi kwa Kutumia Vifaa vya Kisasa

Kwa mamia ya miaka, Waislamu wamechunguza anga ili kuona mwezi mpya mara tu unapotokea na hivyo kutambua mwisho wa mwezi wa Ramadhani ili kuanza Sherehe ya Kufunga. Katika sehemu fulani mwezi ungetafutwa bila kutumia vifaa vyovyote na baada ya hapo kiongozi wa kidini angewatangazia waumini wenzake. Hata hivyo, katika miaka kadhaa iliyopita viongozi kadhaa wa kidini wameanza kutumia vifaa vya kisasa. Wachunguzi wa nyota kutoka Iran pamoja na viongozi wa kidini ambao hutangaza kuhusu kuonekana kwa mwezi, sasa wanatumia darubini za hali ya juu, vifaa vya kuona usiku, na hata ndege zinazobeba vifaa tata vya uchunguzi. Mwezi unapoonekana mapema, sikukuu inaweza kuanza mapema.

Uwezo wa Watoto wa Kutambua Tabia

Watoto walio na miezi sita wana “uwezo wa kutambua tabia za watu kabla ya kujua kuzungumza,” wanasema watafiti wa Chuo Kikuu cha Yale huko Marekani. Watoto wenye umri wa miezi sita hadi kumi, walitazama kifaa cha kuchezea chenye macho makubwa kikijaribu kupanda milima huku vifaa vingine vikikisaidia au kukiangusha. Watoto hao “walipewa vifaa hivyo vya kuchezea ionekane watachagua kucheza na vifaa gani,” linaeleza gazeti Houston Chronicle. “Karibu watoto wote walichagua kifaa cha kuchezea kilichosaidia badala ya kile kibaya.” Kwa hiyo, kwa kadiri fulani, “hata watoto wadogo wanajua tofauti kati ya watu wanaofaa na wale wasiofaa kucheza nao,” linasema gazeti hilo.

“Wananunua Sana Maji ya Chupa”

“Wamarekani wananunua sana maji ya chupa, kwani kila mwaka wananunua karibu chupa bilioni 30 hivi,” linasema gazeti U.S.News & World Report. Hata hivyo, wanunuzi wengi hawatambui kwamba maji mengi ya chupa yanachotwa tu katika mabomba, kwa hiyo “mtu yeyote anayeamua kunywa maji ya chupa badala ya maji ya manispaa kwa sababu ya afya anajidanganya,” linasema gazeti hilo. Katika nchi nyingi maji ya bomba huchunguzwa kuhakikisha yanafikia viwango vinavyofaa. Na yanapolinganishwa na maji “ghali sana” ya chupa, ni ‘kana kwamba maji ya bomba ni ya bure!’